Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mtimizaji wa Ahadi

Mtimizaji wa Ahadi

Mkaribie Mungu

Mtimizaji wa Ahadi

Yoshua 23:14

JE, NI vigumu kwako kuwatumaini wengine? Inahuzunisha kwamba tunaishi katika ulimwengu ambamo watu hawatumainiki. Ikiwa uliumizwa moyoni na mtu uliyemwamini—labda alikudanganya au akakosa kutimiza ahadi fulani—huenda ikawa vigumu kumtumaini tena. Lakini kuna mtu ambaye unaweza kumtumaini na hatakuvunja moyo kamwe. Andiko la Methali 3:5 linatuhimiza hivi: “Mtumaini Mwenyezi-Mungu kwa moyo wako wote, wala usitegemee akili zako.” (Biblia Habari Njema) Kwa nini Yehova anastahili kutumainiwa? Ili kujibu swali hilo, acheni tuchunguze maneno ya Yoshua aliyemtumaini Yehova kabisa kama andiko la Yoshua 23:14 linavyoonyesha.

Fikiria Yoshua aliyewaongoza Waisraeli baada ya Musa, ambaye sasa anakaribia umri wa miaka 110. Katika maisha yake marefu, amejionea matendo mengi yenye nguvu ambayo Yehova aliwafanyia Waisraeli. Kwa mfano, aliona Yehova akiwakomboa Waisraeli kimuujiza kupitia Bahari Nyekundu miaka 60 hivi mapema. Sasa, anapotafakari kuhusu mambo ambayo amejionea maishani mwake, Yoshua anawaita pamoja ‘wanaume wazee na wakuu na waamuzi na maofisa’ wa Israeli. (Yoshua 23:2) Maneno anayowaambia hayaonyeshi tu hekima inayotokana na kuishi kwa miaka mingi, bali yanaonyesha kwamba Yoshua mwenye moyo uliojaa imani anatafakari kuhusu matendo ya Yehova.

Yoshua anaeleza: “Mimi ninaenda katika njia ya dunia yote.” Maneno “njia ya dunia yote” yanamaanisha kifo. Kwa hiyo, ni kama Yoshua anasema: “Sitarajii kuishi muda mrefu zaidi.” Kwa kuwa anajua kwamba anakaribia kufa, hapana shaka Yoshua ametumia muda wa saa nyingi akiwa peke yake ili atafakari kuhusu maisha yake. Anawaaga waabudu wenzake kwa maneno gani?

Yoshua anaendelea kusema: “Halikukosa kutimia hata neno moja kati ya maneno yote mema ambayo Yehova Mungu wenu amewaambia ninyi. Yote yametimia kwenu. Halikukosa kutimia hata neno moja kati ya hayo.” Hayo ni maneno ya mtu anayemtumaini Mungu kabisa. Kwa nini? Anapotafakari kuhusu mambo yote ambayo ameyaona, Yoshua anatambua kuwa Yehova hutimiza ahadi Zake nyakati zote. * Kusudi la maneno yake ni wazi: Yoshua anataka Waisraeli wenzake wawe na imani kabisa kwamba ahadi zote za Yehova kuhusu wakati wao ujao zitatimia pia.

Kitabu kimoja kinachozungumzia Biblia kinasema hivi kuhusu Yoshua 23:14: “Taja ahadi yoyote katika Biblia; chunguza historia ya ulimwengu; muulize mtu yeyote duniani, na utapata kwamba hakuna wakati wowote ambapo Mungu alivunja wala kusahau kutimiza ahadi yake.” Kama tungeweza kufanya uchunguzi huo, tungekubaliana na maneno ya Yoshua kwamba Yehova hakosi kamwe kutimiza ahadi zake.—1 Wafalme 8:56; Isaya 55:10, 11.

Biblia inataja ahadi za Mungu ambazo zimetimia na pia nyingine ambazo zinatimia hata sasa, mbele ya macho yetu. Pia inataja ahadi nzuri za Mungu kuhusu wakati wetu ujao. * Tunakutia moyo ufanye uchunguzi kuhusu ahadi hizo. Kwa kujifunza Biblia unaweza kupata uthibitisho kwamba Mungu anatimiza ahadi zake na anastahili kutumainiwa.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Hapa kuna ahadi chache ambazo Yoshua aliona zikitimizwa. Yehova angewapa Waisraeli nchi yao wenyewe. (Linganisha Mwanzo 12:7 na Yoshua 11:23.) Yehova angewakomboa Waisraeli kutoka Misri. (Linganisha Kutoka 3:8 na Kutoka 12:29-32.) Yehova angewategemeza watu wake.—Linganisha Kutoka 16:4, 13-15 na Kumbukumbu la Torati 8:3, 4.

^ fu. 6 Kwa habari zaidi kuhusu ahadi za Mungu na wakati wetu ujao, ona sura ya 3, 7, na 8 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.