Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

NI NINI kilichomchochea Mrastafari anyoe nywele zake ndefu na kuacha kuwachukia wazungu? Na ni nini kilichomwezesha kijana mwenye jeuri aliyewakusanyia pesa wauzaji wa dawa za kulevya abadili maisha yake? Soma masimulizi ya watu hao.

“Nilishinda chuki niliyokuwa nayo.”—HAFENI NGHAMA

UMRI: 34

NCHI: ZAMBIA

HISTORIA: MRASTAFARI

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nilizaliwa katika kambi ya wakimbizi nchini Zambia. Mama yangu alikimbia kutoka Namibia wakati wa vita, akajiunga na Chama cha Watu wa Kusini Magharibi mwa Afrika (SWAPO). Chama hicho kilikuwa kikipambana na serikali ya Afrika Kusini ambayo ilikuwa ikitawala Namibia wakati huo.

Miaka 15 ya kwanza ya maisha yangu, niliishi katika kambi kadhaa za wakimbizi. Vijana waliokuwa katika kambi za SWAPO walifundishwa kupigania uhuru wa nchi yao. Tulifundishwa mambo ya siasa na pia kuwachukia wazungu.

Nilipokuwa na umri wa miaka 11, nilitaka kupata kipaimara ili niwe Mkristo katika kanisa moja kambini ambalo lilikuwa na Wakatoliki, Walutheri, Waanglikana, na watu wa dini nyingine. Kasisi ambaye nilizungumza naye alinikataza kuchukua hatua hiyo. Kuanzia wakati huo na kuendelea, nikaacha kuamini kwamba kuna Mungu. Hata hivyo, nilipokuwa na umri wa miaka 15, nilijiunga na kikundi cha Warastafari kwa sababu nilipenda muziki wa rege na nilitamani sana kukomesha ukosefu wote wa haki kuelekea Waafrika weusi. Nilifuga nywele ndefu, nilivuta bangi, niliacha kula nyama, na pia nilipigania uhuru wa watu weusi. Hata hivyo, sikuacha maisha yangu mapotovu wala sikuacha kutazama sinema zenye jeuri. Niliendelea kutumia lugha chafu.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Mwaka wa 1995, nilipokuwa na umri wa miaka 20 hivi, nilianza kufikiria kwa uzito kuhusu maisha yangu. Nilikuwa nikisoma vitabu vyote vya Warastafari ambavyo ningeweza kupata. Baadhi ya vitabu hivyo vilizungumzia Biblia, lakini sikuelewa maelezo yake. Kwa hiyo, niliamua kujisomea Biblia.

Baadaye, rafiki yangu Mrastafari alinipa kitabu cha kujifunzia Biblia kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Nilisoma kitabu hicho pamoja na Biblia nikiwa peke yangu. Baadaye, nilikutana na Mashahidi wa Yehova nikaendelea kujifunza Biblia pamoja nao.

Nilijitahidi sana mpaka nikaacha kuvuta bangi na kunywa pombe kupindukia. (2 Wakorintho 7:1) Nilibadili njia yangu ya kuvaa, nikanyoa nywele zangu ndefu, nikaacha kutazama sinema za jeuri na ponografia (habari za ngono), halafu nikaacha kutumia lugha chafu. (Waefeso 5:3, 4) Mwishowe, hata nilishinda chuki niliyokuwa nayo kuelekea wazungu. (Matendo 10:34, 35) Ili nifanye mabadiliko hayo, nilihitaji kutupilia mbali muziki uliochochea ubaguzi wa kijamii na kuacha kabisa kushirikiana na marafiki wangu wa zamani, ambao walijaribu kunishawishi nirudie maisha yangu ya zamani.

Baada ya kufanya mabadiliko hayo, nilitafuta Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova, nikaomba kujiunga na dini hiyo. Nilianza kujifunza Biblia pamoja nao. Nilipoamua kubatizwa ili kuwa Shahidi wa Yehova, familia yangu haikufurahi. Mama yangu aliniambia nichague dini nyingine yoyote ya “Kikristo” lakini si Mashahidi wa Yehova. Mjomba wangu mmoja, ambaye alikuwa na cheo kikubwa katika serikali, alinishutumu daima kwa sababu ya uamuzi wangu wa kushirikiana na Mashahidi.

Hata hivyo, kujifunza jinsi Yesu alivyoshughulika na watu na kufuata mashauri yake kulinisaidia kuvumilia upinzani na dhihaka. Nilipolinganisha mambo ambayo Mashahidi wanafundisha na yale ambayo Biblia inasema, nilisadiki kwamba nilikuwa nimepata dini ya kweli. Kwa mfano, wanafuata amri ya Biblia ya kuwahubiria wengine. (Mathayo 28:19, 20; Matendo 15:14) Nao hawajiingizi katika siasa.—Zaburi 146:3, 4; Yohana 15:17, 18.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Kujifunza kuishi kulingana na viwango vya Biblia kumenisaidia kikweli. Kwa mfano, kila mwezi ninaokoa pesa nyingi sana kwa sababu ya kuacha kuvuta bangi. Sioti tena ndoto mbaya, na afya yangu ya kiakili na ya kimwili imekuwa bora zaidi.

Sasa maisha yangu yana mwelekeo na kusudi ambalo nilitamani sana kupata tangu nilipokuwa mtoto. Na jambo la maana hata zaidi ni kwamba sasa ninahisi nimemkaribia Mungu zaidi.—Yakobo 4:8.

“Nimejifunza kuizuia hasira yangu.”—MARTINO PEDRETTI

UMRI: 43

NCHI: AUSTRALIA

HISTORIA: MUUZAJI WA DAWA ZA KULEVYA

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Familia yangu ilihama-hama nilipokuwa nikikua. Niliishi katika miji midogo, jiji kubwa, na kwa muda fulani niliishi katika eneo la mashambani la wenyeji wa asili wa Australia. Ninakumbuka mambo mazuri niliyofanya pamoja na wajomba na binamu zangu kama vile, kuvua samaki, kuwinda, kutengeneza bumarengi (boomerang), na kuchonga vitu vingine.

Baba yangu alicheza mchezo wa kupigana ngumi na alianza kunifundisha kupigana nikiwa na umri mdogo sana. Nilikuwa mjeuri sana. Nilipokuwa kijana, nilitumia muda mwingi kunywa pombe kwenye baa. Mimi na marafiki wangu tuliwachokoza watu ili tupigane nao. Tulitumia visu na fimbo za mpira wa besiboli kushambulia kikundi cha watu 20 au zaidi.

Nilipata pesa kwa kuuza dawa za kulevya na vitu vilivyoibiwa na wafanyakazi wa bandarini. Pia, niliwakusanyia pesa wauzaji wa dawa za kulevya, na niliwatisha watu kwa kutumia bunduki na bastola ili wanipe pesa hizo. Nilikusudia kuwa muuaji wa kukodiwa. Huu ndio uliokuwa msimamo wangu, Ua ama uuawe.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Nilipokuwa mtoto nilisikia kuhusu Mashahidi wa Yehova. Nilipokuwa na umri wa miaka 20 hivi, ninakumbuka nikimuuliza mama ikiwa alijua Shahidi yeyote. Siku mbili baadaye, Shahidi anayeitwa Dixon aligonga mlango wangu. Baada ya kuzungumza naye kwa muda, alinialika kwenye mkutano wa Mashahidi wa Yehova. Nilihudhuria, na nimekuwa nikihudhuria mikutano hiyo kwa miaka zaidi ya 20 sasa. Mashahidi walijibu maswali yangu yote kwa kutumia Biblia.

Nilifurahi kujifunza kwamba Yehova anamjali kila mtu, hata watu wasiomwabudu. (2 Petro 3:9) Niligundua kwamba yeye ni Baba mwenye upendo ambaye angenitunza, hata wakati ambapo singetunzwa na mtu yeyote. Nilitiwa moyo pia kujua kwamba angenisamehe dhambi zangu ikiwa ningebadili njia zangu. Maneno ya Biblia kwenye Waefeso 4:22-24 yalinigusa moyo sana. Andiko hilo lilinitia moyo “kuuondolea mbali utu wa zamani” na “kuvaa utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu.”

Ilinichukua muda mrefu kubadili maisha yangu. Nilijitahidi kwa juma zima kutotumia dawa za kulevya, lakini nilipokuwa na marafiki wangu mwisho-juma, nilishawishiwa kutumia. Nilitambua kwamba nilihitaji kuhamia mbali na marafiki hao ili niweze kusafisha maisha yangu, kwa hiyo niliamua kuhamia jimbo lingine. Marafiki fulani walijitolea kusafiri pamoja nami, nikakubali. Tulipokuwa safarini, walianza kuvuta bangi na wakaniomba nivute. Niliwaambia kwamba nimeamua kuacha tabia hiyo, basi nilitengana nao mpakani nikaendelea na safari peke yangu. Baada ya muda mfupi, nilipata habari kwamba marafiki hao waliiba benki kwa kutumia bunduki.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Baada ya kuachana kabisa na marafiki hao, ilikuwa rahisi zaidi kwangu kufanya mabadiliko maishani. Mwaka wa 1989, nilibatizwa nikawa Shahidi. Baada ya kubatizwa, dada yangu, mama yangu, na baba yangu walijiunga nami katika kumtumikia Yehova.

Sasa nimefunga ndoa kwa miaka 17 nami nina watoto watatu wazuri sana. Nimejifunza kuizuia hasira yangu, hata ninapochokozwa. Na nimejifunza kuwapenda watu wa ‘makabila, jamii, na lugha zote.’ (Ufunuo 7:9) Nimejionea ukweli wa maneno haya ya Yesu: “Mkikaa katika neno langu, ninyi kwa kweli ni wanafunzi wangu, nanyi mtaijua kweli, nayo kweli itawaweka ninyi huru.”—Yohana 8:31, 32.

[Blabu katika ukurasa wa 19]

Ili nifanye mabadiliko nilihitaji kutupilia mbali muziki uliochochea ubaguzi

[Blabu katika ukurasa wa 20]

Mimi na marafiki wangu tuliwachokoza watu ili tupigane nao. Tulitumia visu na fimbo za mpira wa besiboli kushambulia kikundi cha watu 20 au zaidi