Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutafuta Ukweli Kuhusu Mbingu

Kutafuta Ukweli Kuhusu Mbingu

Kutafuta Ukweli Kuhusu Mbingu

TUMAINI la kwenda mbinguni linavutia sana! Dini kama vile Uislamu, Uhindu, Ubudha, na dini zinazodai kuwa za Kikristo zina imani mbalimbali kuhusu uhai baada ya kifo, na hata watu wengi ambao hawapendezwi na dini wanaamini jambo hilo. Kwa kawaida wanafikiria kwamba mbinguni ni mahali pazuri sana penye raha ambapo watu wanapata kitulizo kutokana na mateso na wanaungana tena na “wapendwa wao walioaga dunia.” Hata hivyo, kwa wanadamu wengi, msemo huu ni wa kweli: Kila mtu anataka kwenda mbinguni, lakini hakuna mtu anayetaka kufa ili aende mbinguni. Kwa nini?

Ikiwa tuliumbwa tukiwa na tumaini la kufa na kwenda mbinguni, je, watu wengi zaidi hawangetamani sana kufa kama vile tu mtoto anavyotamani kuwa mtu mzima au jinsi kijana anavyotazamia kwamba siku moja atafunga ndoa? Lakini watu wengi hawataki kufa.

Ingawa hivyo, wahubiri wengi wanadai kwamba baada ya maisha yetu mafupi duniani, tutaenda mbinguni. Kwa mfano, Theodore Edgar Cardinal McCarrick, askofu mkuu aliyestaafu wa Washington, D.C., alisema hivi: “Hatukuumbwa tuishi hapa. Tuliumbwa ili tuishi mbinguni.” Vivyo hivyo, aliyekuwa msimamizi wa Shirika la Kitaifa la Wainjilisti la Marekani alisema hivi: “Kusudi la maisha ni kumtukuza Mungu na kwenda mbinguni . . . kwa sababu nyumbani kwetu ni mbinguni.”

Kwa kawaida, wale wanaoamini kwamba watu wanaenda mbinguni baada ya kufa hawana habari za kutosha za kuunga mkono imani hiyo. George Barna, msimamizi wa shirika moja linalofanya utafiti kuhusu maoni ya dini, alitambua kwamba watu wengi “wanaamini kuhusu uhai na uhai baada ya kifo wakitegemea mawazo kutoka kwa vyanzo tofauti-tofauti kama vile, sinema, muziki na vitabu vya hadithi.” Kasisi mmoja wa Kanisa la Kianglikana huko Florida alisema hivi: “Hatujui jambo lolote kuhusu mbinguni, tunalojua ni kwamba Mungu anaishi mbinguni.”

Hata hivyo, Biblia ina habari ya maana sana kuhusu mbingu. Neno la Mungu linasema nini kuhusu mbingu? Je, mwanadamu aliumbwa ili aishi mbinguni? Ikiwa watu wataenda mbinguni, wataenda kufanya nini huko?

[Blabu katika ukurasa wa 3]

Kwa nini watu wengi wanataka kwenda mbinguni, lakini ni wachache wanaotaka kufa ili waende mbinguni?