Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Wafanyakazi Nyumbani”

“Wafanyakazi Nyumbani”

Jinsi Wakristo Walivyoishi Katika Karne ya Kwanza

“Wafanyakazi Nyumbani”

“Basi walipokuwa wameenda aliingia katika kijiji fulani. Hapa mwanamke fulani aliyeitwa Martha alimkaribisha nyumbani. Mwanamke huyu alikuwa pia na dada aliyeitwa Maria, ambaye, hata hivyo, aliketi miguuni pa Bwana na kuendelea kulisikiliza neno lake. Martha naye alikengeushwa na kazi nyingi. Kwa hiyo, akaja karibu na kusema: ‘Bwana, hujali kwamba dada yangu ameniacha peke yangu kushughulikia mambo? Kwa hiyo, mwambie aje anisaidie.’ Bwana akamjibu akamwambia: ‘Martha, Martha, wewe unahangaika na kusumbuka juu ya mambo mengi. Ingawa hivyo, mambo machache ndiyo yanayohitajiwa, au moja tu. Yeye, Maria alichagua fungu jema, nalo halitaondolewa kwake.’”—LUKA 10:38-42.

BILA shaka, Martha alikuwa mwanamke mwenye bidii. Ni wazi kwamba alithaminiwa sana na wengine. Wayahudi wa karne ya kwanza walipima thamani ya mwanamke kulingana na bidii yake ya kufanya kazi za nyumbani na uwezo wake wa kutimiza mahitaji ya familia yake.

Wanawake Wakristo walioishi katika karne ya kwanza walihimizwa pia wawe “wafanyakazi nyumbani.” (Tito 2:5) Lakini pia walikuwa na pendeleo na daraka la kuwafundisha wengine kuhusu imani yao ya Kikristo. (Mathayo 28:19, 20; Matendo 2:18) Mwanamke Myahudi aliyeishi katika karne ya kwanza alipaswa kushughulikia ‘kazi gani nyingi’? Na tunajifunza nini kutokana na maneno ambayo Yesu alimwambia Maria?

Alikuwa na “Kazi Nyingi” Mke Myahudi alianza kufanya kazi asubuhi, labda kabla ya jua kuchomoza. (Methali 31:15) Baada ya kupikia familia yake chakula chepesi, huenda aliwapeleka watoto wake wa kiume kwenye shule ya sinagogi. Binti zake walibaki nyumbani ili wafundishwe jinsi ya kuwa wake wema.

Kisha, mama na binti zake, walianza kufanya kazi za nyumbani kama vile, kujaza taa mafuta (1), kufagia nyumba (2), na kukamua mbuzi wa familia (3). Halafu, wangeoka mkate wa siku hiyo. Kwanza, binti zake wangepepeta nafaka ili kuondoa uchafu (4), kisha wangesaga nafaka hizo kwa jiwe la kusagia ili kupata unga (5). Mama alichukua unga huo na kuuchanganya na maji na chachu. Kisha alikanda unga huo (6) na kuuacha mchanganyiko huo uvimbe huku akiendelea na kazi nyingine. Wakati huohuo, binti zake walikuwa wakipigapiga maziwa ya mbuzi ili yawe jibini (7).

Asubuhi hiyohiyo, huenda mama angeenda pamoja na binti zake sokoni. Akiwa sokoni, mama angenunua vyakula alivyohitaji huku akifurahia harufu ya vikolezo. Pia, kulikuwa na milio ya wanyama na sauti za watu waliokuwa wakiomba kupunguziwa bei (8). Huenda pia alinunua mboga na samaki waliokaushwa. Ikiwa alikuwa Mkristo, labda alitumia nafasi hiyo kuzungumza na watu wengine sokoni kuhusu imani yake.—Matendo 17:17.

Akiwa njiani, mama aliyethamini mambo ya kiroho angetumia nafasi hiyo kuwasaidia watoto wake wajifunze na kuthamini kanuni za Kimaandiko. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Huenda pia alizungumza na binti zake kuhusu kanuni ambazo zingewasaidia kutumia pesa kwa hekima.—Methali 31:14, 18.

Kazi nyingine ambayo wanawake walifanya kila siku ni kuteka maji kwenye kisima (9). Waliteka maji ambayo yangetumiwa na familia, na huenda walizungumza na wanawake wengine waliokuja kisimani. Waliporudi nyumbani, mama na binti zake walianza kuoka mikate. Kwanza, waliukata vipande-vipande unga uliokandwa na kuusukuma, kisha waliutia ndani ya jiko la kuokea (10), ambalo kwa kawaida lilikuwa nje ya nyumba. Walifurahia harufu nzuri ya mikate iliyokuwa ikiokwa huku wakizungumza.

Kisha walienda kufua nguo kwenye kijito kilichokuwa karibu (11). Kwanza, wanawake hao walifua nguo hizo vizuri kwa sabuni iliyotengenezwa kwa chumvi au majivu ya mimea fulani. Baada ya kusuuza nguo na kuzikamua, wanawake hao walizianika kwenye vichaka na mawe makubwa ili zikauke.

Baada ya kurudi nyumbani na nguo hizo, huenda mama na binti zake walipanda juu ya paa tambarare la nyumba yao ili kushona nguo (12) zozote zilizoraruka kabla ya kuziweka ndani ya makabati. Baadaye, labda wasichana walifundishwa kufuma vitambaa na kushona tarizi (13). Muda si muda, wanawake hao wangeanza kupika chakula cha jioni (14). Wayahudi walikuwa na desturi ya kuonyesha ukarimu, hivyo, familia ilikuwa tayari kushiriki na mgeni yeyote chakula chao kilichotia ndani mkate, mboga, jibini, samaki waliokaushwa, na maji baridi.

Usiku kabla ya kulala, huenda watoto waliochubuka au kujikata walipakwa mafuta. Kisha, kwa mwangaza hafifu wa taa, huenda wazazi waliwasomea watoto wao simulizi fulani kutoka katika Maandiko na kusali pamoja nao. Katika kimya cha usiku, mume angekuwa na sababu nzuri ya kumwambia mke wake maneno haya yanayojulikana sana: “Mke mwenye uwezo, ni nani anayeweza kumpata? Thamani yake inapita sana ile ya marijani.”—Methali 31:10.

Kuchagua “Fungu Jema” Bila shaka, wanawake wenye bidii katika karne ya kwanza walikuwa na “kazi nyingi.” (Luka 10:40) Vivyo hivyo leo, wanawake, hasa akina mama wana shughuli nyingi. Maendeleo ya kiteknolojia leo yamerahisisha kazi fulani za nyumbani. Lakini hali fulani zinawalazimisha akina mama wengi kutunza familia zao na pia kufanya kazi za kuajiriwa.

Hata ingawa wanawake wengi Wakristo leo wanakabili matatizo mengi, wanamwiga Maria, aliyetajwa mwanzoni. Wanathamini sana mambo ya kiroho. (Mathayo 5:3) Wanazitunza vizuri familia zao kama Maandiko yanavyowahimiza. (Methali 31:11-31) Lakini pia wanaishi kulingana na kanuni ambayo Yesu alimwambia Martha. Bila shaka, Martha alithamini kikumbusho hicho kwa sababu alikuwa mwanamke aliyependa mambo ya kiroho. Wanawake Wakristo hawaruhusu madaraka yao ya nyumbani yawazuie kujifunza kumhusu Mungu (15) au kuzungumza na wengine kuhusu imani yao. (Mathayo 24:14; Waebrania 10:24, 25) Hivyo, wanachagua “fungu jema.” (Luka 10:42) Kwa sababu hiyo, wanathaminiwa sana na Mungu, na Kristo, na familia zao.—Methali 18:22.