Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwamba Ulio Katika Mawingu

Mwamba Ulio Katika Mawingu

Barua Kutoka Papua New Guinea

Mwamba Ulio Katika Mawingu

NI SAA 11 asubuhi, Jumanne moja (Siku ya 2) yenye joto huko Lae, Papua New Guinea (PNG). Mimi na mke wangu tunajitayarisha kwenda huko Lengbati, eneo lililo juu ya Mlima Rawlinson katika Jimbo la Morobe ili kutembelea kikundi cha Mashahidi wa Yehova huko.

Tunasafiri kwa muda wa nusu saa hivi kwa ndege ndogo ya abiria wanne. Kwa kawaida, tunaposafiri kwa ndege ninaketi kando ya rubani, na ingawa kuna kelele ya injini, tunazungumza kwa kutumia mitambo ya mawasiliano. Ananionyesha vifaa mbalimbali vya kuongozea ndege, ananieleza jinsi kila kifaa kinavyofanya kazi, kisha anafanya mzaha kwamba ikiwa atapatwa na jambo lolote baya, mimi ndiye nitakayeendesha ndege hiyo. Mara moja ninakumbuka kisa kimoja kuhusu mhudumu mwingine anayesafiri ambaye ni Shahidi wa Yehova huku PNG. Walipokuwa wanasafiri kwa ndege, rubani alipoteza fahamu, ndege ikazunguka angani bila mwelekeo mpaka rubani aliporudiwa na fahamu na ndege ikatua. Hata hivyo, safari yetu haina matatizo yoyote.

Tunasafiri kando ya safu ya milima na kwa ghafula, tunapita katika mawingu na kupaa juu ya kilele cha mlima, kilele hicho kiko mita 100 hivi chini yetu. Mbele yetu tunaona kijiji cha Lengbati chenye nyumba nyingi zilizojengwa kwa vijiti na kuezekwa kwa nyasi nyingi. Rubani anatazama uwanja mdogo wa ndege tukiwa angani, anaangalia jinsi ulivyo na kuhakikisha kwamba watoto kutoka kijiji hicho hawachezi mpira kwenye uwanja huo. Pia, anaangalia ikiwa nguruwe wamechimba mashimo kwenye uwanja huo tangu alipotua hapo mara ya mwisho. Anazunguka na kusema, “Ni sawa; acha tujaribu kutua.” Tunazunguka angani na tunaanza kushuka ili tutue kwenye uwanja huo mdogo, ambao wanakijiji waliutengeneza juu ya mlima huo na ambao hivi karibuni walitandaza miamba ya chokaa iliyopondwa-pondwa ambayo walitoa kwenye mlima ulio karibu.

Katika safari zilizopita, nimeangalia miamba iliyovunjika ya chokaa na kujiuliza milima hiyo imekuwapo kwa muda gani. Hebu fikiria nguvu nyingi zilizosukuma miamba hiyo, ambayo ina urefu wa mamia ya kilomita kutoka baharini, kufikia kimo cha kilomita nne angani! Tunaposhuka kutoka kwenye ndege, tunasimama juu ya ule mwamba ulio katika mawingu.

Kama kawaida, wanakijiji wanakimbia kutoka kila upande wanaposikia sauti ya ndege inayotua. Rubani anapozima injini ya ndege, ninaona mwanamume mmoja kutoka kwenye umati akikaribia ndege. Mwanamume huyo ni Zung. Ni mmoja kati ya wanaume wa eneo hili ambao wamepewa mgawo wa kusimamia programu ya ufundishaji inayofanywa kila juma na Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Watu wa eneo hilo wanajua kwamba anaishi maisha safi, ya unyoofu, na ni mtu mwenye kutegemeka. Anakiri kwamba alijifunza kuwa hivyo kwa kufuata kanuni za Biblia katika maisha yake. Baada ya kusalimiana, tunatembea na Zung pamoja na Mashahidi wengine kuelekea upande wa chini wa mlima. Watoto wanatufuata, huku wakibishana kati yao kuhusu ni nani ambaye atabeba mizigo yetu.

Tunafika kwenye nyumba ndogo ya mbao iliyojengwa na Mashahidi wa eneo hili, ili mhudumu anayesafiri akae humo anapowatembelea baada ya miezi sita hivi. Ingawa PNG ni nchi yenye joto, eneo hili lina baridi sana kwa sababu liko milimani. Usiku tunapowasha taa ya mafuta, mara nyingi ninaona mawingu ambayo yalikuwa yanaelea angani wakati wa alasiri kwenye mabonde yaliyo chini, yakiingia ndani ya nyumba kupitia mianya iliyo katika sakafu ya mbao. Kuna mabadiliko katika hali ya hewa kwa sababu sasa tunavaa makoti ya kujikinga na baridi kali na suruali za jinzi ili kupata joto lakini saa chache zilizopita tulikuwa tunatokwa na jasho kwa sababu ya joto kali kwenye sehemu ya pwani.

Katikati ya miaka ya 1980, mwanamume mmoja kutoka maeneo hayo alifundishwa Biblia na Mashahidi wa Yehova huko Lae. Aliporudi huku kwenye kijiji chao, yeye pamoja na watu wengine wachache walijenga nyumba ndogo ya kukutania na waliipenda sana. Kisha kasisi wa kanisa la Kilutheri katika eneo hilo pamoja na wafuasi wake wakateketeza kabisa nyumba hiyo ya ibada. Watu hao walijivuna kwamba eneo hilo lilikuwa la dini ya Kilutheri peke yake. Ingawa upinzani umeongezeka tangu wakati huo, Mashahidi wamejenga mahali pengine pa ibada na idadi yao imeongezeka kufikia karibu watangazaji 50 wenye bidii wa habari njema. Watu fulani ambao hapo zamani walipinga kazi ya Mashahidi, sasa wanaifanya kwa bidii.

Siku hizi, mara nyingi wakaaji wa kijiji hiki wanawakaribisha Mashahidi wa Yehova, ambao wanawafundisha Biblia. Ingawa ni watu wachache tu wanaojua kusoma katika kijiji hiki, Mashahidi wengi wanaoishi katika eneo hili wamejifunza kusoma ili wawahubirie wengine ujumbe wa Biblia. Karibu watu 200 wanahudhuria mikutano katika Jumba lao la Ufalme kila juma.

Hakuna umeme katika eneo hili. Wakati wa jioni, sote tunakusanyika jikoni ili kuota moto. Tunakula pamoja, tunazungumza, na kucheka. Shangwe ya kumtumikia Yehova inaonekana wazi kwenye nyuso zenye tabasamu za marafiki wetu, zinazong’aa katika mwangaza wa moto. Kisha, usiku unapozidi kusonga, wengine kati yetu wanachukua bombom, yaani, majani yanayowaka ya mitende, ambayo wanatumia kumulika njia za vichakani wakielekea nyumbani.

Tunapoelekea nyumbani, tunafurahia kimya kilichopo. Tunasikia milio ya wadudu wadogo. Kabla ya kulala tunaangalia anga isiyo na mawingu na tunashangaa kuona nyota nyingi sana.

Juma linapita haraka na tunasubiri kwa hamu kusafiri kwa ndege siku inayofuata. Tunalala usiku mwingine wenye baridi katika mawingu ya Lengbati, kisha tunarudi kwenye joto na unyevunyevu wa pwani.