Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Ambayo Yesu Alifundisha Kujihusu

Mambo Ambayo Yesu Alifundisha Kujihusu

Mambo Ambayo Yesu Alifundisha Kujihusu

“Yesu hakuwa na shaka lolote kujihusu, kuhusu mahali alipotoka, sababu iliyofanya aje duniani, au kuhusu wakati wake ujao.”—MWANDISHI HERBERT LOCKYER.

KABLA ya kukubali na kuamini mambo ambayo Yesu alifundisha, tunahitaji kumjua kwa kadiri fulani. Kwa kweli, Yesu alikuwa nani? Alitoka wapi? Alikuwa na kusudi gani maishani? Tunaposoma vitabu vya Injili, yaani, Mathayo, Marko, Luka, na Yohana, ni kana kwamba Yesu anajibu maswali hayo.

Aliishi mbinguni kabla ya kuzaliwa duniani Yesu alisema: “Kabla ya Abrahamu kuwako, mimi nimekuwako.” (Yohana 8:58) Abrahamu aliishi miaka 2,000 hivi kabla ya Yesu kuzaliwa hapa duniani. Na bado, Yesu alikuwapo kabla ya mtu huyu mwaminifu kuishi duniani. Basi, Yesu aliishi wapi wakati huo? Alieleza hivi: “Nimeshuka kutoka mbinguni.”—Yohana 6:38.

Mwana wa Mungu Yehova ana wana wengi ambao ni malaika. Hata hivyo, Yesu ni wa pekee. Alijiita “Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu.” (Yohana 3:18) Maneno hayo yanamaanisha kwamba ni Yesu peke yake aliyeumbwa moja kwa moja na Mungu. Mwana huyu mzaliwa-pekee alitumiwa na Mungu kuumba vitu vingine vyote.—Wakolosai 1:16.

“Mwana wa binadamu” Alipojirejelea, Yesu alitumia maneno hayo mara nyingi kuliko majina mengine yoyote. (Mathayo 8:20) Kwa njia hiyo, alionyesha kwamba hakuwa malaika aliyetokea katika mwili wa binadamu. Alikuwa mwanadamu kabisa. Kupitia roho takatifu, Mungu alihamisha uhai wa Mwana wake kutoka mbinguni mpaka duniani, na kuuweka katika tumbo la uzazi la bikira Maria. Hivyo, Yesu alizaliwa akiwa binadamu mkamilifu asiye na dhambi.—Mathayo 1:18; Luka 1:35; Yohana 8:46.

Masihi aliyeahidiwa Mwanamke Msamaria alimwambia Yesu hivi: “Ninajua kwamba Masihi anakuja.” Yesu akamwambia: “Mimi ninayesema nawe ndiye.” (Yohana 4:25, 26) Maneno “Masihi” na “Kristo” yanamaanisha “Mtiwa-Mafuta.” Yesu alitiwa mafuta au kuteuliwa na Mungu, ili atimize sehemu ya pekee kuhusiana na ahadi za Mungu.

Kazi yake kuu Yesu alisema: “Ni lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu . . . kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.” (Luka 4:43) Ingawa aliwafanyia watu mambo mengi mema, jambo muhimu maishani mwake lilikuwa kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme wa Mungu. Baadaye tutazungumzia mambo ambayo Yesu alifundisha kuhusu Ufalme.

Kwa kweli, Yesu alikuwa mtu wa pekee. * Kama tutakavyoona, maneno aliyosema akiwa duniani yalikuwa na maana kubwa zaidi kwa sababu alikuwa ameishi mbinguni kabla ya kuja duniani. Basi, haishangazi kwamba alihubiri ujumbe ambao ungewanufaisha mamilioni ya watu kote duniani.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Kwa habari zaidi kumhusu Yesu na sehemu yake katika kusudi la Yehova, ona sura ya 4 katika kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.