Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sinagogi—Mahali Ambapo Yesu na Wanafunzi Wake Walihubiri

Sinagogi—Mahali Ambapo Yesu na Wanafunzi Wake Walihubiri

Sinagogi—Mahali Ambapo Yesu na Wanafunzi Wake Walihubiri

“Ndipo akaenda akizunguka katika Galilaya yote, akifundisha katika masinagogi yao na kuhubiri habari njema ya ufalme.”—MATHAYO 4:23.

MARA nyingi katika masimulizi ya Injili, tunasoma kumhusu Yesu akiwa katika sinagogi. Alipokuwa Nazareti, mji ambako alilelewa, au jiji la Kapernaumu ambako alikaa, au alipokuwa kwenye miji na vijiji alivyotembelea wakati wa huduma yake yenye shughuli nyingi ya miaka mitatu na nusu, mara nyingi Yesu alichagua sinagogi ili kuhubiri na kufundisha kuhusu Ufalme wa Mungu. Wakati mmoja, alisema hivi kuhusu huduma yake: “Sikuzote nilifundisha katika sinagogi na katika hekalu, ambapo Wayahudi wote hukusanyika.”—Yohana 18:20.

Vivyo hivyo, mara nyingi mitume wa Yesu na Wakristo wengine wa mapema walifundisha kwenye masinagogi ya Wayahudi. Hivyo basi, ni hali gani zilizofanya Wayahudi waanze kuabudu katika masinagogi? Na masinagogi hayo yalikuwa yamejengwa jinsi gani wakati wa Yesu? Acheni tuyachunguze kwa makini.

Sinagogi Lilikuwa Muhimu Katika Maisha ya Wayahudi Wanaume Wayahudi walikuwa wakisafiri mara tatu kwa mwaka kwenda Yerusalemu kwa ajili ya sherehe zilizofanywa katika hekalu takatifu huko. Lakini kuhusiana na ibada yao ya kila siku, Wayahudi walienda kwenye sinagogi la kwao, iwe waliishi Palestina au katika koloni nyingi za Wayahudi zilizokuwa nje ya Palestina.

Walianza kutumia masinagogi wakati gani? Watu fulani wanafikiri kwamba sinagogi lilianza kutumiwa wakati Wayahudi walipopelekwa uhamishoni Babiloni (607-537 K.W.K.). Wakati huo hekalu la Yehova lilikuwa limeharibiwa. Au huenda ni punde tu baada ya Wayahudi kurudi kutoka uhamishoni, wakati kuhani Ezra alipowahimiza watu wake wajifunze na kuielewa vizuri zaidi Sheria ya Mungu.—Ezra 7:10; 8:1-8; 10:3.

Mwanzoni, neno “sinagogi” lilimaanisha tu “kusanyiko” au “kutaniko.” Neno hilo limetumiwa katika maana hiyo kwenye Septuajinti, yaani, tafsiri ya Kigiriki ya Maandiko ya Kiebrania. Lakini, baada ya muda neno hilo lilitumiwa kurejelea jengo ambapo watu walikutana kuabudu. Kufikia karne ya kwanza W.K., karibu kila mji ambao Yesu alitembelea ulikuwa na sinagogi; majiji yalikuwa na masinagogi kadhaa; jiji la Yerusalemu lilikuwa na masinagogi mengi. Masinagogi hayo yalikuwa yamejengwa jinsi gani?

Nyumba ya Ibada Isiyo na Madoido Mengi Wakati wa kujenga sinagogi, kwa kawaida Wayahudi walitafuta eneo lililoinuka, nao walihakikisha kwamba mwingilio (1) wa sinagogi ulielekea Yerusalemu. Inaonekana viwango hivyo vingeweza kubadilishwa, kwa kuwa nyakati nyingine wangeshindwa kuvitimiza.

Lilipomalizika, mara nyingi jengo hilo halikuwa na madoido mengi wala vitu vingi ndani. Hata hivyo, katika sinagogi kifaa kilichokuwa muhimu zaidi ni sanduku (2) la kuwekea vitabu vya kukunjwa vya Maandiko Matakatifu ambavyo vilithaminiwa sana. Wakati wa mikutano, sanduku hilo liliwekwa mahali pake, na baadaye kurudishwa mahali salama (3).

Karibu na sanduku hilo, kulikuwa na viti vya mbele (4) vilivyopangwa kuelekea kutaniko, navyo vilikaliwa na maofisa-wasimamizi wa sinagogi pamoja na wageni wowote waheshimiwa. (Mathayo 23:5, 6) Karibu na eneo la katikati la sinagogi palikuwa na jukwaa lililokuwa na kinara na kiti cha msemaji (5). Kwenye upande wa mbele, wa kushoto, na wa kulia wa jukwaa hilo, kulikuwa na viti vya washiriki wa kutaniko (6).

Kwa kawaida, gharama za kuendesha shughuli za sinagogi zililipiwa na kutaniko. Michango ya hiari iliyotolewa na wote, matajiri kwa maskini, ilitumiwa kurekebisha na kudumisha jengo hilo. Mikutano iliendeshwa jinsi gani katika sinagogi?

Ibada Kwenye Sinagogi Programu ya ibada kwenye sinagogi ilitia ndani nyimbo za sifa, sala, kusoma Maandiko, na pia kuhubiri na kufundisha. Washiriki wa kutaniko walianza programu kwa kukariri Shema, yaani, ungamo la imani la Wayahudi. Jina la ungamo hilo lilitokana na neno la kwanza la andiko ambalo lilikaririwa hivi: “Sikiliza [Shema], Ee Israeli: Yehova Mungu wetu ni Yehova mmoja.”—Kumbukumbu la Torati 6:4.

Kisha, walisoma na kufafanua sehemu ya Torati, yaani, vile vitabu vitano vya kwanza vya Biblia vilivyoandikwa na Musa. (Matendo 15:21) Pia, walisoma sehemu fulani za maandishi ya manabii, kisha wakayafafanua na kuonyesha jinsi yanavyotumika. Mara kwa mara, wasemaji wanaozuru walishughulikia sehemu hii ya usomaji, kama Yesu alivyofanya katika pindi inayotajwa kwenye Luka 4:16-21.

Kitabu cha kukunjwa ambacho Yesu alipewa kwenye mkutano huo, hakikuwa na alama za sura wala mistari kama Biblia za sasa. Kwa hiyo, tunaweza kuwazia Yesu akikunjua kitabu hicho kwa mkono wa kushoto huku akikikunja kwa mkono wa kulia hadi alipopata sehemu aliyotaka kusoma. Baada ya kusomwa, kitabu hicho kilikunjwa tena hadi sehemu ya kwanza.

Mara nyingi, usomaji huo ulifanywa katika Kiebrania cha awali na kutafsiriwa katika Kiaramu. Kwenye makutaniko ya Kigiriki, Septuajinti ilitumiwa.

Sinagogi Lilitumiwa Sana Sinagogi lilikuwa muhimu sana katika maisha ya Wayahudi, kwa kuwa jengo hilo, pamoja na majengo mengine yaliyokuwa yamejengwa karibu au yameunganishwa nalo, yalitumika kwa shughuli mbalimbali. Nyakati nyingine kesi zilisikilizwa hapo na pia mikutano ya umma na hata makusanyiko yalifanyiwa hapo. Kulikuwa na chakula kilichoandaliwa kwenye vyumba vya kulia chakula ambavyo vilikuwa vimeunganishwa na sinagogi. Mara kwa mara, wasafiri waliandaliwa mahali pa kulala katika majengo yaliyokuwa kwenye ua wa sinagogi.

Karibu katika kila mji, kulikuwa na shule kwenye ua wa sinagogi na mara nyingi, shule hiyo ilikuwa katika jengo la sinagogi. Tunaweza kuwazia chumba ambacho kimejaa wanafunzi wachanga wakijifunza kusoma herufi kubwa zilizoandikwa na mwalimu kwenye bamba la nta. Shule hizo ziliwasaidia Wayahudi wa kale wajue kusoma na kuandika, na hivyo hata watu wa kawaida wangeweza kusoma Maandiko.

Kando na hayo, sinagogi lilitumiwa hasa kwa ajili ya ibada. Basi, haishangazi kwamba mikutano ya Wakristo wa karne ya kwanza ilifanana sana na mikutano ya Wayahudi katika sinagogi. Sawa na Wayahudi, Wakristo pia walikutana ili kumwabudu Yehova kupitia sala, nyimbo za sifa, kusoma na kuzungumzia Neno la Mungu. Kuna mambo mengine pia yaliyofanana. Katika mikutano hiyo ya Wayahudi na ya Wakristo, michango ya hiari ilitolewa ili kugharimia mahitaji mbalimbali; pendeleo la kusoma na kuzungumzia Neno la Mungu katika mikutano halikuwa jukumu lililotengewa makasisi; pia mambo yalipangwa na kuelekezwa na wanaume wazee wenye madaraka.

Leo, Mashahidi wa Yehova hujitahidi kufuata kielelezo kilichowekwa na Yesu na wafuasi wake katika karne ya kwanza. Kwa hiyo, mikutano yao kwenye Jumba la Ufalme inafanana kwa njia kadhaa na mikutano iliyofanywa katika sinagogi zamani. Zaidi ya yote, Mashahidi hukutana wakiwa na lengo lilelile ambalo wale wanaoipenda kweli wamekuwa nalo sikuzote, yaani, ‘kumkaribia Mungu.’—Yakobo 4:8.

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Mfano huu wa Sinagogi umechorwa kutokana na ramani ya ujenzi ya Sinagogi la Gamla la karne ya kwanza

[Picha katika ukurasa wa 18]

Shule katika sinagogi ambapo wavulana wenye umri wa miaka 6 hadi 13 walifunzwa