Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kweli Ni Udanganyifu?

Je, Kweli Ni Udanganyifu?

Je, Kweli Ni Udanganyifu?

“Badili kidogo tu ripoti yako ya aksidenti na kila kitu kitakuwa shwari.”

“Mashirika ya kukusanya kodi hayahitaji kujua kila kitu.”

“Jambo muhimu ni, kutoshikwa.”

“Kwa nini ulipie kitu unachoweza kupata bure?”

HUENDA ukasikia mambo kama hayo unapoomba ushauri kuhusu masuala ya pesa. Ni kana kwamba watu fulani wana “suluhisho” la kila jambo. Swali ni, Mashauri hayo yanafaa?

Udanganyifu umeenea sana leo hivi kwamba watu huona kusema uwongo na kuiba kuwa njia zinazokubalika za kuepuka adhabu, za kupata pesa, au za kujiendeleza maishani. Mara nyingi watu mashuhuri katika jamii ni wadanganyifu. Katika nchi moja ya Ulaya, visa vya udanganyifu na wizi vilizidi kwa asilimia 85 kuanzia mwaka wa 2005 mpaka 2006. Visa hivyo havitii ndani visa vingi vidogo-vidogo vya udanganyifu ambavyo watu fulani huviita makosa madogo-madogo au “dhambi ndogo-ndogo.” Yaelekea halikuwa jambo la kushangaza kwamba wafanyabiashara na wanasiasa mashuhuri katika nchi hiyo walihusika katika kashfa fulani iliyoonyesha kwamba walitumia vyeti bandia ili kujinufaisha.

Hata hivyo, licha ya kuenea sana kwa udanganyifu ulimwenguni, watu wengi wanataka kufanya yaliyo sawa. Yaelekea wewe ni mmoja wao. Huenda kwa sababu unampenda Mungu, unataka kufanya yaliyo sawa machoni pake. (1 Yohana 5:3) Labda unahisi kama mtume Paulo, aliyeandika: “Tuna uhakika kwamba tuna dhamiri nyoofu, kwa kuwa tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.” (Waebrania 13:18) Kwa sababu hiyo, tunakuomba uchunguze hali fulani zinazoweza kumtia kwenye jaribu mtu anayetaka kujiendesha kwa “unyoofu katika mambo yote.” Pia, tutachunguza kanuni za Biblia zinazoweza kutusaidia katika hali kama hizo.

Ni Nani Anayepaswa Kulipia Gharama Zinazosababishwa na Aksidenti?

Siku moja msichana anayeitwa Lisa * alipokuwa akiendesha gari alifanya makosa na gari lake likagonga gari lingine. Hakuna mtu aliyejeruhiwa, hata hivyo, magari yote mawili yaliharibika. Katika nchi anayoishi, madereva wenye umri mdogo hutozwa kiasi kikubwa cha malipo ya bima ya gari, na malipo hayo huongezeka baada ya kila aksidenti. Kwa kuwa Lisa aliandamana na Gregor, binamu yake mwenye umri mkubwa, rafiki yao aliwashauri waripoti kwamba Gregor ndiye aliyekuwa akiliendesha gari. Kwa kufanya hivyo, Lisa angeweza kuepuka kulipa kiasi kikubwa cha bima. Hilo lilionekana kuwa shauri lenye hekima. Lisa angefanya nini?

Makampuni ya bima hutumia malipo yanayotolewa na wateja wao kulipia madai ya gharama mbalimbali. Hivyo basi, kwa kufuata shauri la rafiki yake, ni kana kwamba Lisa angekuwa akiwalazimisha wateja wengine walipe kiasi kikubwa cha pesa kulipia aksidenti ambayo yeye alisababisha. Mbali na kutoa ripoti ya uwongo, atakuwa anawaibia wengine. Pia, ni wizi kutoa taarifa za uwongo ili kulipwa kiasi kikubwa cha pesa kwa sababu ya aksidenti.

Huenda watu fulani wakaogopa kufanya tendo hilo la udanganyifu kwa sababu ya adhabu za kisheria. Hata hivyo, sababu kuu ya kujiepusha na udanganyifu inapatikana katika Neno la Mungu. Mojawapo ya zile Amri Kumi inasema: “Usiibe.” (Kutoka 20:15) Akiwaandikia Wakristo, mtume Paulo alirudia amri hiyo akisema: “Mwizi asiibe tena.” (Waefeso 4:28) Kwa kutii Neno la Mungu katika mambo kama hayo ya bima, unaepuka kufanya jambo ambalo Mungu anashutumu. Unaonyesha pia kwamba unaipenda na kuiheshimu sheria ya Mungu na unawapenda na kuwaheshimu jirani zako.—Zaburi 119:97.

“Mlipeni Kaisari Vitu vya Kaisari”

Peter ni mfanyabiashara. Mhasibu wake anamshauri aombe kupunguziwa kodi ya “ununuzi” wa kifaa cha kompyuta cha bei ghali. Kwa biashara kama ya Peter, ni jambo la kawaida kununua vitu vya aina hiyo. Ijapokuwa Peter hakununua kifaa hicho, haielekei kwamba serikali itafanya uchunguzi wa jinsi ambavyo pesa hizo zilitumiwa. Kwa kupunguziwa kodi hiyo, Peter hatahitaji kulipa pesa nyingi za kodi. Afanye nini? Ni nini kitakachomsaidia kufanya uamuzi?

Mtume Paulo aliwaambia Wakristo wa siku zake: “Kila nafsi na ijitiishe kwa mamlaka zilizo kubwa . . . Wapeni wote haki zao, yeye anayetaka kodi, kodi; yeye anayetaka ushuru, ushuru.” (Waroma 13:1, 7) Wote wanaotaka kukubaliwa na Mungu hulipa kodi zote ambazo wanahitajiwa kulipa kulingana na sheria. Kwa upande mwingine, ikiwa sheria ya nchi inaruhusu watu fulani au wafanyabiashara fulani wapunguziwe kodi, hakuna ubaya kudai jambo hilo ikiwa unastahili kisheria kufanya hivyo.

Tuone kisa kingine kinachohusisha kulipa kodi. David ni seremala katika kampuni fulani. Lakini rafiki na jirani zake humwomba awatengenezee kabati na fanicha, naye hufanya hivyo baada ya kazi. Wao humlipa pesa nyingi kuliko mshahara anaopokea. Hata hivyo, anafanya kazi hiyo bila idhini ya mwajiri wake. Hivyo, hakuna anayeweka rekodi ya kazi iliyofanywa naye David halipi kodi ya matumizi. Watu wengi hawaoni ubaya wowote wa kufanya hivyo. Kwa sababu David anataka kumpendeza Mungu, anapaswa kuwa na maoni gani kuhusu kazi hiyo?

Mtu anayefanya kazi kwa njia hiyo huenda asishikwe, lakini halipi kodi ambayo serikali ina haki ya kukusanya. Yesu aliamuru: “Basi, mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, lakini Mungu vitu vya Mungu.” (Mathayo 22:17-21) Yesu alisema hayo ili kuwasaidia wasikilizaji wake wawe na maoni yanayofaa kuhusu kulipa kodi. Mamlaka za serikali, ambazo Yesu aliziita Kaisari, huyaona malipo ya kodi kuwa haki yao. Kwa hiyo, wafuasi wa Kristo huona kulipa kodi zote kuwa wajibu wa Kimaandiko.

Kuiba Mtihani

Marta, mwanafunzi wa shule ya sekondari anajitayarisha kwa ajili ya mtihani wake wa mwisho. Kwa kuwa matazamio yake ya kupata kazi nzuri yanategemea kupata alama za juu, ametumia wakati mwingi kusoma. Baadhi ya wanafunzi wenzake wamejitayarisha pia—lakini kwa njia tofauti. Watatumia vifaa za kielektroniki kama vile mashini za kupiga hesabu, na simu za mkononi, kudanganya ili kupata alama za juu. Je, Marta afanye kile ambacho “kila mtu” anafanya ili kuhakikisha kwamba anapata alama za juu?

Kwa kuwa kuiba mtihani ni jambo la kawaida, wengi hawaoni ubaya wake. Wao husema, “Bora usishikwe.” Hata hivyo, kwa Wakristo wa kweli, maoni hayo hayakubaliki. Huenda mwalimu asiwaone wanaoiba mtihani, hata hivyo, kuna yule anayewaona. Yehova Mungu anajua kile tunachofanya, naye atatuhukumu kulingana na matendo yetu. Paulo aliandika: “Hakuna kiumbe kisichokuwa wazi machoni pake, bali vitu vyote viko uchi navyo vimefunuliwa wazi machoni pake yeye ambaye tunatoa hesabu kwake.” (Waebrania 4:13) Kujua kwamba Mungu anatutazama kwa sababu anataka tufanye yaliyo sawa ni kichocheo kikubwa cha kuwa wanyoofu tunapofanya mtihani, sivyo?

Utafanya Nini?

Lisa, Gregor, Peter, David, na Marta walitambua hatari za hali walizokabili. Waliamua kutenda kwa unyoofu na hivyo kudumisha dhamiri safi na maadili mema. Utafanya nini ukikabili hali kama hizo?

Huenda wafanyakazi, wanafunzi, na majirani wako wasione ubaya wowote wa kusema uwongo, kudanganya, au kuiba. Labda wanaweza hata kukudhihaki ili kujaribu kukulazimisha kutenda kama wao. Ni nini kitakachokusaidia kufanya uamuzi unaofaa licha ya kushinikizwa kutenda kwa udanganyifu?

Kumbuka kwamba kutenda kulingana na mapenzi ya Mungu hutufanya kuwa na dhamiri safi na kupata kibali chake. Mfalme Daudi aliandika: “Ee Yehova, ni nani atakayekuwa mgeni katika hema lako? Ni nani atakayekaa katika mlima wako mtakatifu? Yeye anayetembea bila kosa na kuzoea kutenda uadilifu na kusema kweli katika moyo wake. . . . Yeye anayefanya mambo hayo hatatikiswa.” (Zaburi 15:1-5) Kuwa na dhamiri safi na urafiki pamoja na Mungu wa mbinguni ndiyo mambo yenye thamani sana kuliko faida yoyote ya kimwili inayopatikana kwa njia ya udanganyifu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

[Blabu katika ukurasa wa 12]

“Mwizi asiibe tena.”

Kuheshimu sheria za Mungu na kupenda jirani hutuchochea kuwa wanyoofu katika masuala yanayohusu bima

[Blabu katika ukurasa wa 12]

“Wapeni wote haki zao, yeye anayetaka kodi, kodi.”

Ili tukubaliwe na Mungu, tunalipa kodi zote zinazohitajiwa kisheria

[Blabu katika ukurasa wa 13]

“Vitu vyote . . . vimefunuliwa wazi machoni pake yeye ambaye tunatoa hesabu kwake.”

Ijapokuwa huenda walimu wasitushike tukiiba mtihani, tunataka kuwa wanyoofu mbele za Mungu

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 14]

Wizi Usioonekana Wazi

Rafiki yako amenunua programu ya karibuni zaidi ya kompyuta, na ungependa kuwa nayo. Ili kukusaidia usitumie pesa nyingi, anakupa nakala ya programu hiyo. Je, huo ni wizi?

Watu wanaotumia kompyuta, wanaponunua programu fulani ya kompyuta, wanakubali kufuata maagizo yaliyo katika hati ya mapatano kuhusu programu hiyo. Huenda hati hiyo ikamruhusu mnunuzi kuweka na kutumia programu hiyo katika kompyuta moja tu. Hivyo basi, kumpa mtu mwingine nakala ya programu hiyo, ni kukiuka mapatano na ni kinyume cha sheria. (Waroma 13:4) Kutoa nakala ya programu hiyo ni wizi pia kwa sababu kunamnyima mwenye haki-miliki mapato ambayo ni haki yake.—Waefeso 4:28.

Huenda wengine wakasema, ‘Hakuna atakayejua.’ Huenda ikawa hivyo, lakini tunapaswa kukumbuka maneno haya ya Yesu: “Mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.” (Mathayo 7:12) Sote tungependa kupata malipo kulingana na kazi tunayofanya, na tungependa watu waheshimu mali zetu. Kwa hiyo, tunapaswa kuwatendea wengine kwa njia hiyohiyo. Tunaepuka wizi “usioonekana wazi,” kama vile kuchukua mali za kitaaluma * ambazo si haki yetu.—Kutoka 22:7-9.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 40 Mali za kitaaluma zinatia ndani vifaa vyenye haki za kunakili kama vile muziki, vitabu, au programu za kompyuta, ziwe zimechapishwa au zimehifadhiwa katika kompyuta. Pia, alama za biashara, hataza, siri za kibiashara, na haki za matangazo, zote ziko ndani ya kikundi hicho.