Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Maisha Yako Yanaongozwa na Nyota?

Je, Maisha Yako Yanaongozwa na Nyota?

Je, Maisha Yako Yanaongozwa na Nyota?

KATIKA usiku usio na mawingu, mbali na mianga ya wanadamu, mbingu zinaonekana kama kitambaa cheusi tititi ambacho kimepambwa kwa vipande vingi vidogo vya almasi vinavyometameta. Ni katika miaka 350 tu iliyopita ambapo mwanadamu ameanza kutambua jinsi nyota zilivyo kubwa na jinsi zilivyo mbali kutoka sayari yetu ya Dunia. Tumeanza tu kuelewa kuhusu nguvu nyingi ambazo zinafanya kazi kotekote katika ulimwengu.

Tangu zamani, wanadamu wamechunguza miendo hususa ya nyota na sayari katika mbingu za usiku na pia mahali tofauti-tofauti ambapo nyota na sayari hizo zinakuwa kulingana na majira. (Mwanzo 1:14) Wengi wanahisi kama Mfalme Daudi wa Israeli ambaye aliandika hivi yapata miaka 3,000 iliyopita: “Ninapoziona mbingu zako, kazi za vidole vyako, mwezi na nyota ambazo umetayarisha, mwanadamu anayeweza kufa ni nini hivi kwamba umweke akilini?”—Zaburi 8:3, 4.

Hata hivyo, iwe tunajua au hatujui, miendo ya nyota na sayari ina uvutano wa moja kwa moja katika maisha yetu. Dunia huzunguka jua ambalo ni nyota inayotusaidia kujua urefu wa siku na mwaka. Mwezi ni “kwa ajili ya nyakati zilizowekwa,” au ‘kutupimia majira.’ (Zaburi 104:19; Biblia Habari Njema) Nazo nyota ni mwongozo unaotegemeka katika usafiri, na hata wanaanga wanaweza kutumia nyota wanapoongoza vyombo vyao vya angani. Kwa hiyo, wengi wangependa kujua kama nyota zinaweza kufanya mengi zaidi ya kutuonyesha wakati na majira, na kutusaidia tuthamini kazi za uumbaji za Mungu. Je, nyota zinaweza kutusaidia kujua wakati ujao au kutuonya kuhusu misiba?

Unajimu Ulianzishwa Wapi na kwa Kusudi Gani?

Unajimu, ambao ni zoea la kutazama mbingu ili kutafuta ishara za kuongoza maisha yetu duniani, ulianzia Mesopotamia ya kale, yaelekea katika miaka ya 2000 K.W.K. Wanajimu wa kale walitazama mbingu kwa makini. Elimu ya nyota ilianzishwa na juhudi zao za kuchora miendo ya nyota na sayari, kujua mahali kila nyota ilipo, kutengeneza kalenda, na kutabiri kupatwa kwa jua au mwezi. Lakini wanajimu hawachunguzi tu uvutano wa mwezi na jua katika mazingira yetu. Wanajimu wanadai kwamba mpangilio wa jua, mwezi, sayari, nyota, na makundi ya nyota, una uvutano juu ya matukio makuu duniani na pia juu ya maisha ya kila mtu. Katika njia zipi?

Wanajimu fulani wanatazama nyota na sayari ili wajue mambo au hatari za wakati ujao. Na watu wanaouelewa wanaweza kuutumia ujuzi huo na kunufaika nao kwa njia mbalimbali. Wengine wanahisi kuwa unajimu unaonyesha kile ambacho kimeamuliwa mapema tufanye, au kwamba unajimu unaweza kutusaidia kujua wakati unaofaa wa kushiriki katika utendaji fulani au kuanza kufanya mambo fulani. Inasemekana kwamba habari hizi zinaweza kujulikana kwa kutazama mpangilio wa nyota au sayari fulani na kuchunguza uhusiano kati ya nyota na sayari hizo na pia uhusiano wake na dunia. Inasemekana kuwa uvutano wa nyota na sayari juu ya maisha ya mtu binafsi unategemea mpangilio wake wakati wa kuzaliwa kwa mtu huyo.

Wanajimu wa kale walifikiri kuwa dunia ndiyo kitovu cha ulimwengu, na kwamba sayari na nyota zilikuwa zimefungiwa katika miviringo ya kimbingu ambayo iliizunguka dunia. Pia walifikiri kwamba jua linasafiri angani kati ya makundi ya nyota likifuata njia fulani hususa katika mzunguko wa kila mwaka. Waliigawanya njia hii ya jua ya kila mwaka katika sehemu au maeneo 12. Sehemu hizo zote zilikuwa na makundi ya nyota, na kila sehemu ilipewa jina kulingana na kundi la nyota ambamo jua lilipitia. Sehemu hizo zikawa zile ishara 12 za nyota na kuitwa “nyumba za mbinguni,” kwa sababu zilionwa kuwa makao ya miungu hususa. Hata hivyo, wanasayansi waligundua baadaye kuwa jua haliizunguki dunia bali dunia ndiyo inayozunguka jua. Uvumbuzi huo ulithibitisha kuwa unajimu si sayansi yenye kutegemeka.

Kutoka Mesopotamia ulikoanzia, unajimu ulienea hadi karibu sehemu zote za dunia na ukatumiwa kwa njia moja au nyingine katika maeneo yote yenye ustaarabu mkubwa duniani. Baada ya Uajemi kushinda Babiloni, unajimu ulienea hadi Misri, Ugiriki, na India. Kutoka India, wamishonari Wabudha waliueneza hadi Asia ya Kati, China, Tibet, Japani, na Asia ya Kusini-Mashariki. Ingawa haijulikani jinsi ambavyo unajimu uliwafikia Wamaya, waliutumia sana kwa njia inayofanana na ile ya Wababiloni. Yaonekana kuwa unajimu uliopo leo ulianzishwa huko Misri wakati wa utawala wa Ugiriki, na umeathiri sana maoni ya Wayahudi, Waislamu, na watu wa dini zinazojidai kuwa za Kikristo.

Taifa la Israeli pia liliathiriwa na unajimu hata kabla ya kupelekwa uhamishoni huko Babiloni katika karne ya saba K.W.K. Biblia hutueleza kuhusu jitihada za Mfalme mwaminifu Yosia za kukomesha zoea la kutoa dhabihu “kwa jua na kwa mwezi na kwa makundi-nyota ya unajimu na kwa jeshi lote la mbinguni.”—2 Wafalme 23:5.

Chanzo cha Unajimu

Unajimu unategemea uelewaji usio sahihi hata kidogo kuhusu muundo wa ulimwengu na miendo ya nyota na sayari. Hivyo, unajimu hautokani na Mungu. Kwa kuwa msingi wa unajimu si wa kweli, basi hauwezi kuwa chanzo sahihi cha habari kuhusu wakati ujao. Matukio mawili ya kihistoria yenye kusisimua yanaonyesha kwamba unajimu hautegemeki.

Wakati wa utawala wa Mfalme Nebukadneza wa Babiloni, makuhani na wanajimu walishindwa kufasiri ndoto ya mfalme. Danieli, nabii wa Mungu wa kweli, Yehova, alionyesha sababu zilizofanya washindwe kufasiri ndoto hiyo aliposema: “Siri ambayo mfalme anauliza, watu wenye hekima, wala wafanya-mazingaombwe, wala makuhani wenye kufanya uchawi wala wanajimu hawawezi kumwonyesha mfalme. Hata hivyo, kuna Mungu mbinguni ambaye ni Mfunuaji wa siri, naye amemjulisha Mfalme Nebukadneza mambo yatakayotokea katika siku za mwisho.” (Danieli 2:27, 28) Danieli alimtumaini Yehova Mungu ambaye ni “Mfunuaji wa siri”—bali si jua, mwezi, au nyota—na akamweleza mfalme maana ya kweli ya ndoto yake.—Danieli 2:36-45.

Makadirio hususa kabisa ya unajimu ya Wamaya hayakuzuia kuanguka kwa ustaarabu wao katika karne ya tisa W.K. Kushindwa huku kunaonyesha kuwa unajimu ni udanganyifu ambao hauwezi kutabiri chochote kwa usahihi na kwamba kusudi lake ni kuwazuia watu wasitafute ujuzi sahihi kutoka kwa Mungu kuhusu wakati ujao.

Kujua kwamba msingi wa unajimu si wa kweli kunatuwezesha kujua ni nani aliye chanzo chake. Yesu alisema hivi kumhusu Ibilisi: “Hakusimama imara katika kweli, kwa sababu kweli haimo ndani yake. Anaposema uwongo, yeye husema kulingana na mwelekeo wake mwenyewe, kwa sababu yeye ni mwongo na ndiye baba ya uwongo.” (Yohana 8:44) Shetani anajifanya kuwa “malaika wa nuru,” na mashetani wake wanajifanya kuwa “wahudumu wa uadilifu.” Kwa kweli, hao ni viumbe ambao kusudi lao ni kuwapotosha na kuwadanganya watu. (2 Wakorintho 11:14, 15) Neno la Mungu linafunua wazi kwamba ‘matendo yenye nguvu na ishara za uwongo na mambo ya ajabu,’ ni “utendaji wa Shetani.”—2 Wathesalonike 2:9.

Kwa Nini Uepuke Unajimu?

Unajimu unategemea mambo ya uwongo, na hivyo, ni chukizo kwa Mungu wa kweli, Yehova. (Zaburi 31:5) Kwa hiyo, Biblia inaushutumu na inawahimiza watu wajiepushe nao. Katika Kumbukumbu la Torati 18:10-12, Mungu anasema hivi waziwazi: “Asipatikane ndani yako yeyote . . . anayetafuta ishara za bahati au mlozi, . . . yeyote anayetafuta shauri kwa mwenye kuwasiliana na pepo au mjuzi wa kubashiri matukio au yeyote anayeuliza habari kutoka kwa wafu. Kwa maana kila mtu anayefanya mambo hayo ni chukizo kwa Yehova.”

Nguvu za kufanya unajimu zinatoka kwa Shetani na mashetani wake, hivyo, kujihusisha na unajimu kunamweka mtu chini ya uvutano wao. Kama vile ambavyo kuvuta bangi kunaweza kumfanya mtu awe mtumwa wa walanguzi wa dawa za kulevya, kujihusisha na unajimu kunaweza kumfanya mtu atawaliwe na yule mdanganyifu mkuu, Shetani. Hivyo basi, wale wanaompenda Mungu na kweli, wanapaswa kuukataa kabisa unajimu na badala yake kutii shauri hili la Biblia: “Chukieni yaliyo mabaya, pendeni yaliyo mema.”—Amosi 5:15.

Unajimu umeenea sana kwa sababu watu wanatamani kujua mambo ya wakati ujao. Je, inawezekana kujua mambo hayo? Ikiwa ndivyo, tunaweza kuyajua jinsi gani? Biblia inasema kwamba hatuwezi kujua ni nini ambacho kitampata kila mmoja wetu kesho, mwezi ujao, au mwaka ujao. (Yakobo 4:14) Hata hivyo, Biblia inatufunulia mambo ambayo yatawapata wanadamu kwa ujumla wakati ujao. Inatuambia kwamba karibuni, Ufalme utakuja, kama tunavyoomba katika Sala ya Bwana. (Danieli 2:44; Mathayo 6:9, 10) Pia inatuambia kwamba kuteseka kwa binadamu kutaisha hivi karibuni na hatutasumbuka tena. (Isaya 65:17; Ufunuo 21:4) Badala ya kuamua mapema mambo yatakayompata kila mtu, Mungu anawaalika watu kila mahali wajifunze kumhusu, na kuhusu yale atakayofanya kwa faida yao. Tunajuaje hilo? Biblia inaeleza wazi kwamba mapenzi ya Mungu ni “watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.”—1 Timotheo 2:4.

Mbingu zenye fahari na vitu vyote vilivyomo havikuwekwa humo ili kuongoza maisha yetu. Badala yake, vinaonyesha nguvu za Yehova na Uungu wake. (Waroma 1:20) Vinaweza kutuchochea tukatae uwongo na kumtumaini Mungu na Neno lake, Biblia, ili kupata mwongozo na mwelekezo unaotegemeka wa kufanikisha maisha yetu. “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.”—Methali 3:5, 6.

[Blabu katika ukurasa wa 19]

Wamaya waliutumia sana unajimu

[Blabu katika ukurasa wa 20]

Makadirio hususa ya unajimu ya Wamaya hayakuzuia kuanguka kwa ustaarabu wao

[Blabu katika ukurasa wa 20]

“Kuna Mungu mbinguni ambaye ni Mfunuaji wa siri, naye amejulisha . . . mambo yatakayotokea katika siku za mwisho”

[Picha katika ukurasa wa 19]

Kituo cha kuchunguzia anga cha El Caracol, Chichén Itzá, Yucatán, Mexico, 750-900 W.K.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 19]

Pages 18 and 19, left to right: Stars: NASA, ESA, and A. Nota (STScI); Mayan calendar: © Lynx/Iconotec com/age fotostock; Mayan astronomer: © Albert J. Copley/age fotostock; Mayan observatory: El Caracol (The Great Conch) (photo), Mayan/Chichen Itza, Yucatan, Mexico/Giraudon/The Bridgeman Art Library