Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Maoni ya Watu Kuhusu Dhambi Yamebadilika?

Je, Maoni ya Watu Kuhusu Dhambi Yamebadilika?

Je, Maoni ya Watu Kuhusu Dhambi Yamebadilika?

MIAKA michache iliyopita, watu wanaoenda kanisani walikuwa wakiwasikia mara kwa mara wahubiri wao wakitangaza kutoka jukwaani kuhusu zile zinazoitwa “dhambi saba nzito,” yaani, tamaa, ulafi, pupa, hasira, uzembe, wivu, na kiburi. Mara nyingi, mhubiri angezungumzia matokeo mabaya ya dhambi na kuwahimiza wasikilizaji wake watubu. Mwandishi mmoja anasema, “Siku hizi wahubiri wameamua kutozungumzia mambo yatakayoumiza hisia za wasikilizaji wao, badala yake wanazingatia mambo yanayowafanya wahisi ‘wametulizwa.’”

Waandishi fulani wa magazeti wameshuhudia mtazamo huohuo. Yafuatayo ni maelezo mafupi kutoka kwenye magazeti:

▪ “Mahubiri ya zamani kuhusu dhambi, toba na ukombozi hayapendwi, lakini siku hizi mahubiri kuhusu jinsi unavyoweza kujiheshimu na kujipenda ndiyo yanayopendwa sana.”—Star Beacon, Ashtabula, Ohio.

▪ “Watu hawajali wala hawaogopi kufanya dhambi.”—Newsweek.

▪ “Siku hizi hatuulizi ‘Mungu anataka nifanye nini,’ badala yake tunauliza, ‘Mungu anaweza kunifanyia nini?’”—Chicago Sun-Times.

Katika ulimwengu ambao watu wamechangamana licha ya kuwa na imani, malezi, na hata sera tofauti za kisiasa, watu huogopa kuweka viwango vya maadili. Wengi huona kuwa haifai kufanya hivyo. Kulingana nao, kushutumu matendo ya mtu mwingine ni dhambi kubwa. Wengi wanaamini hivi: ‘Kile unachoamini kuwa ni sawa kwako huenda kikakufaa wewe, hata hivyo, usijaribu kumlazimisha mtu mwingine afuate maoni yako. Siku hizi watu huishi kulingana na viwango ambavyo wamejiwekea. Hakuna mtu anayejua kabisa yaliyo sawa. Mtu yeyote hapaswi kuona viwango vyake kuwa bora kuliko vya wengine.’

Maoni hayo yamewafanya watu wabadili mtazamo wao. Neno “dhambi” halitumiki tena katika mazungumzo muhimu. Kwa wengi, neno hilo hutumiwa katika vichekesho au mizaha. Watu wanaoishi pamoja bila kufunga ndoa hawaonwi kuwa “wanaishi katika dhambi,” bali “wanaishi tu pamoja.” Wanaofanya uzinzi hawaonwi kuwa “wazinzi,” bali “wana uhusiano tu.” Wanaofanya ngono na watu wa jinsia moja hawaonwi tena kuwa “mashoga,” bali kwamba wanapendelea “mtindo mwingine tu wa maisha.”

Ni wazi kwamba mtazamo wa watu kuhusu mambo wanayoyaona kuwa ya “kawaida” na yale wanayoyaona kuwa “dhambi,” umebadilika. Lakini kwa nini mtazamo wa watu umebadilika? Je, maoni yetu kuhusu dhambi yamebadilika? Je, ni muhimu kufikiria maoni yako kuhusu suala hilo?