Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mashahidi wa Yehova Wanashiriki Katika Ibada za Dini Nyingine?

Je, Mashahidi wa Yehova Wanashiriki Katika Ibada za Dini Nyingine?

Wasomaji Wetu Wanauliza . . .

Je, Mashahidi wa Yehova Wanashiriki Katika Ibada za Dini Nyingine?

▪ Kitabu kimoja cha marejeo (World Christian Encyclopedia) kinasema kwamba kuna “dini kubwa 10,000 hivi duniani.” Kwa kuwa vita vya kidini vimesababisha uchungu mwingi sana, wanadini wengi wanaamini kwamba ushirikiano kati ya dini mbalimbali unaweza kuleta amani na umoja duniani.

Biblia inawahimiza watu wakae kwa umoja. Mtume Paulo alilinganisha kutaniko la Kikristo na mwili wa binadamu, ambao viungo vyake vyote ‘vimeunganishwa pamoja kwa upatano na kufanywa vishirikiane.’ (Waefeso 4:16) Mtume Petro pia aliwahimiza waamini wenzake hivi: “Ninyi nyote iweni na akili zinazopatana.”—1 Petro 3:8.

Wakristo wa karne ya kwanza waliishi katika ulimwengu wenye desturi na dini nyingi mbalimbali. Hata hivyo, Paulo alipoandika kuhusu wafuasi wa dini mbalimbali kushirikiana katika ibada, aliuliza hivi: “Mtu mwaminifu ana fungu gani na asiye mwamini?” Kisha akawahimiza Wakristo ‘watoke katikati yao.’ (2 Wakorintho 6:15, 17) Ni wazi kwamba Paulo aliwahimiza Wakristo wasishiriki katika ibada za watu wengine. Kwa nini alifanya hivyo?

Mtume Paulo alieleza kwamba haingefaa Mkristo wa kweli kushiriki katika ibada ya mtu ambaye si Mkristo. Hilo lingekuwa kama kufungwa nira isivyofaa. (2 Wakorintho 6:14) Imani ya yule Mkristo ingedhoofika. Paulo alikuwa na mahangaiko kama ya baba anayejua kwamba baadhi ya watoto katika eneo lao wana tabia mbaya. Kwa kuwa baba anamjali mtoto wake, hamruhusu acheze na wale watoto wenye tabia mbaya. Huenda uamuzi wake usipendwe. Hata hivyo, kwa kumtenganisha mtoto wake na watoto hao wenye tabia mbaya, anamlinda asiathiriwe na tabia zao. Hali kadhalika, Paulo alijua kwamba iwapo Wakristo wangejitenga na dini nyingine, wangelindwa wasiathiriwe na mazoea mabaya ya dini hizo.

Paulo alimwiga Yesu alipochukua msimamo huo. Yesu alijitahidi sana kuwasaidia watu wakae kwa amani, hata hivyo, hakushiriki katika ibada za dini nyingine. Wakati wa huduma ya Yesu duniani, kulikuwa na vikundi vingi vya dini kama vile Mafarisayo na Masadukayo. Vikundi hivyo vya dini viliungana ili kumpinga Yesu, na hata kupanga njama ya kumuua. Yesu naye aliwaambia wafuasi wake ‘wajihadhari na mafundisho ya Mafarisayo na Masadukayo.’—Mathayo 16:12.

Namna gani leo? Je, bado tunapaswa kutii onyo la Biblia la kutoshiriki katika ibada za dini nyingine? Ndiyo. Kwa sababu haiwezekani kuchanganya mafundisho ya dini mbalimbali kama vile isivyowezekana kuchanganya mafuta na maji kwa kuyamwaga tu katika sufuria moja. Kwa mfano, watu wa dini mbalimbali wanapoungana ili kuomba kuwe na amani, sala yao inamwendea mungu gani? Je, inamwendea Mungu wa Utatu wa dini zinazojidai kuwa ni za Kikristo? Mungu wa Wahindu anayeitwa Brahma? Budha? Au mungu mwingine?

Nabii Mika alitabiri kwamba “katika siku za mwisho” watu wa mataifa yote wangesema: “Njooni, twendeni juu kwenye mlima wa Yehova na kwenye nyumba ya Mungu wa Yakobo; naye atatufundisha njia zake, nasi tutatembea katika mapito yake.” (Mika 4:1-4) Kwa hiyo, amani na umoja zingepatikana duniani kote, si kwa sababu dini zote zingeungana kwa njia fulani, bali kwa sababu watu wote wangekubali ile dini moja ya kweli.

[Picha katika ukurasa wa 27]

Wafuasi wa dini kuu za ulimwengu wakiwa pamoja kwenye mkutano, mwaka wa 2008

[Hisani]

REUTERS/Andreas Manolis