Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Maoni ya Watu Kuhusu Dhambi Yamebadilika?

Kwa Nini Maoni ya Watu Kuhusu Dhambi Yamebadilika?

Kwa Nini Maoni ya Watu Kuhusu Dhambi Yamebadilika?

“WATU wengi leo hawakubaliani na wazo la kwamba tuna hatia kutokana na dhambi iliyofanywa zamani na wazazi wetu wa kwanza. Hata hawakubali kwamba kuna dhambi. . . . Watu kama vile Adolf Hitler na Josef Stalin huenda walitenda dhambi, lakini sisi wengine hatuna hatia.”—The Wall Street Journal.

Kulingana na nukuu hiyo, inaonekana wazo la kwamba kuna dhambi halieleweki. Kwa nini? Ni nini kimebadilika? Hata hivyo, dhambi ni nini?

Dhambi inaweza kufafanuliwa kwa njia mbili—dhambi tuliyorithi, na mwenendo wetu wenye dhambi. Njia ya kwanza, tunazaliwa nayo, tupende tusipende, njia ya pili, inatokana na mwenendo wetu. Acheni tuchunguze kila moja ya njia hizo.

Je, Kweli Tumeathiriwa na Dhambi ya Asili?

Biblia inasema kwamba sisi sote tumerithi dhambi ya asili kutoka kwa wazazi wetu wa kwanza. Kwa hiyo, sisi sote huzaliwa tukiwa hatujakamilika. Biblia inasema: “Ukosefu wote wa uadilifu ni dhambi.”—1 Yohana 5:17.

Hata hivyo, kwa watu wengi wanaoenda kanisani, wazo la kwamba wanadamu wote huzaliwa wakiwa hawajakamilika kwa sababu ya dhambi iliyofanywa zamani na ambayo hawakushiriki, halieleweki na wala halifai. Kuhusu fundisho hilo, Edward Oakes, profesa wa theolojia anasema, “watu wengi huaibika kulizungumzia, hulikataa katakata, au kwa kiasi fulani hulikubali tu kijuujuu, ingawa kufanya hivyo, hakuathiri jinsi wanavyojiendesha maishani.”

Mambo ambayo makanisa yamefundisha kuhusu dhambi ya asili ni mojawapo ya sababu zinazofanya iwe vigumu watu kulikubali fundisho hilo. Kwa mfano, katika Baraza la Trent (1545-1563), kanisa lilimshutumu mtu yeyote ambaye alipinga kwamba watoto wachanga wanahitaji kubatizwa ili kuondolewa dhambi. Wanatheolojia hao walidai kwamba ikiwa mtoto mchanga yeyote angekufa bila kubatizwa, dhambi zake ambazo hazikuondolewa, zitamzuia asiingie kamwe mbinguni. Calvin hata alifundisha kwamba watoto wachanga ‘huzaliwa wakiwa na dhambi zao wenyewe.’ Pia alisisitiza kwamba ‘dhambi hizo ni nyingi sana hivi kwamba zinamchukiza Mungu.’

Kwa kawaida, watu wengi huona kwamba watoto wachanga ni viumbe wasio na hatia ambao hawapaswi kuteseka kwa sababu ya dhambi waliyorithi. Hivyo, ni wazi kwamba mafundisho kama hayo ya kanisa yamewafanya watu wasiamini fundisho kuhusu dhambi ya asili. Kwa kweli, viongozi fulani wa kanisa hawakuweza kuwahukumu watoto wachanga kuwa wanastahili kwenda katika moto wa mateso eti kwa sababu hawajabatizwa. Kwa maoni yao, mwisho wa watoto hao unabaki kuwa fumbo lenye kutatanisha la kitheolojia. Ingawa halikuwahi kuwa fundisho rasmi la kanisa, kwa karne nyingi Kanisa Katoliki lilifundisha kwamba nafsi za watu wasio na hatia ambao hawajabatizwa, zitaishi mahali paitwapo Limbo (sehemu ya ahera ziendako roho za watoto na watu wema wasiobatizwa). *

Sababu nyingine iliyochangia kudhoofisha imani ya watu kuhusu dhambi ya asili ni kwamba katika karne ya 19, wanafalsafa, wanasayansi, na wanatheolojia walianza kutilia shaka ikiwa masimulizi ya Biblia yanapaswa kukubaliwa kuwa sahihi kihistoria. Nadharia ya mageuzi ya Darwin imewafanya watu wengi walione simulizi la Adamu na Hawa kuwa hadithi tu. Kwa sababu hiyo, watu wengi leo huiona Biblia kuwa kitabu chenye maoni na mapokeo ya waandikaji badala ya kuiona kuwa ufunuo kutoka kwa Mungu.

Namna gani fundisho kuhusu dhambi ya asili? Bila shaka, ikiwa watu wanaoenda kanisani wameshawishiwa kuamini kwamba Adamu na Hawa hawakuwa watu halisi waliowahi kuishi, basi hakuna dhambi ya asili iliyowahi kufanywa. Hata wale wanaokubali kwamba wanadamu kwa ujumla hawajakamilika, wanaiona dhambi ya asili kuwa namna nyingine tu ya kusema wanadamu hawajakamilika.

Ikiwa hivyo ndivyo mambo yalivyo, namna gani wazo la kwamba dhambi ambazo sisi wenyewe hufanya—mbali na dhambi tuliyorithi—pia humkasirisha Mungu?

Je, Kweli Hii ni Dhambi?

Watu wanapoulizwa maoni yao kuhusu dhambi, wengi hufikiria zile Amri Kumi—amri inayokataza kuua, ukosefu wa uaminifu katika ndoa, kuwaka tamaa, kufanya ngono kabla ya ndoa, kuiba, na kadhalika. Kwa miaka mingi makanisa yalifundisha kwamba mtu akifa bila kutubu dhambi kama hizo, atateswa milele katika moto wa mateso. *

Ili mtu asiteswe motoni, Kanisa Katoliki humtaka atubu dhambi kwa kasisi, ambaye wanadai kwamba ana uwezo wa kusamehe dhambi. Hata hivyo, Wakatoliki wengi huona kuungama, kuondolewa dhambi, na kutubu kuwa mambo yaliyopitwa na wakati. Kwa mfano, utafiti uliofanywa hivi karibuni unaonyesha kwamba zaidi ya asilimia 60 ya Wakatoliki wa Italia hawaendi tena kuungama dhambi zao.

Ni wazi kwamba fundisho la zamani kuhusu dhambi zinazofanywa na watu binafsi na matokeo ya dhambi hizo—kama linavyofafanuliwa na makanisa—halijawasaidia watu kuacha kufanya dhambi. Watu wengi wanaoenda kanisani hawaamini kwamba mambo hayo yote ni mabaya. Kwa mfano, watu fulani husema kwamba ikiwa watu wazima wawili wanakubaliana kufanya ngono na hakuna mtu wa tatu anayeumizwa, hakuna ubaya.

Huenda watu hao wanafikiri hivyo kwa sababu mambo ambayo wamefundishwa kuhusu dhambi si yenye kusadikisha. Kwa kweli, si rahisi kwa wengi kuamini kwamba Mungu mwenye upendo anaweza kuwatesa watenda-dhambi milele katika moto wa mateso. Na labda hilo linaonyesha kwa kadiri fulani, sababu inayofanya watu wasiichukulie “dhambi” kwa uzito. Hata hivyo, mambo mengine pia yamechangia kubadilika kwa maoni ya watu kuhusu dhambi.

Kupuuza Utamaduni

Matukio ya karne chache zilizopita yamechangia mabadiliko makubwa katika jamii na katika mitazamo ya watu. Vita viwili vya ulimwengu, vita vingi vidogo-vidogo, na mauaji ya watu wengi yamewaacha wengi wakijiuliza ikiwa kuna haja ya kuendelea kufuata kanuni za kale. Wao huuliza: ‘Katika ulimwengu ambao umeendelea kitekinolojia je, inapatana na akili kuishi kulingana na kanuni zilizotungwa karne nyingi zilizopita na ambazo hazipatani kabisa na mambo ya kisasa?’ Wanafalsafa fulani wamekata kauli kwamba hilo haliwezekani. Wanaamini kwamba wanadamu wanapaswa kuacha baadhi ya maadili ya kale na kishirikina ili wajitahidi kufanya mabadiliko makubwa kupitia elimu.

Kufikiri kwa aina hiyo kumewafanya watu wengi wapuuze sheria za kale za maadili. Katika nchi nyingi za Ulaya, ni watu wachache wanaoenda kanisani. Watu wengi hawana dini fulani hususa, na baadhi yao hupinga vikali sheria zozote za kanisa ambazo kwa maoni yao hazifai. Wao husema, ikiwa wanadamu walitokana na mageuzi na uteuzi wa kiasili, basi hakuna haja kusema kwamba mtu amefanya dhambi kwa sababu ya kuvunja kanuni za maadili.

Katika karne ya 20, watu wengi katika nchi za Magharibi walipuuza viwango vya maadili na kusababisha mabadiliko mengi kutia ndani yale yanayoitwa mabadiliko ya mtazamo kuhusu ngono. Mambo kama vile migomo ya wanafunzi, vikundi vya kupinga utamaduni, na dawa za kuzuia mimba, yamechangia pia kukataliwa kwa maoni ya zamani kuhusu adabu. Muda si muda, kanuni za Biblia zikakataliwa. Kukawa na kizazi kipya chenye viwango vipya vya maadili na mtazamo mpya kuelekea dhambi. Kuanzia wakati huo na kuendelea, asema mwandishi mmoja, “sheria pekee iliyobaki ni sheria ya upendo”—upendo ambao unaonyeshwa kupitia mahusiano yaliyoenea sana ya ngono haramu.

Mwelekeo wa Kufuata Dini Zinazowafurahisha Watu

Gazeti la Newsweek likizungumzia hali hiyo huko Marekani, lilisema: “Makasisi wengi wanaoshindana kupata wafuasi, wanahisi kwamba hawawezi kuhubiri mambo yasiyowavutia watu.” Wanaogopa kuweka sheria kali za maadili, ili wasipoteze wafuasi wao. Watu hawapendi kuambiwa kwamba wanapaswa kusitawisha unyenyekevu, kujitia nidhamu, na kuwa wema, au kwamba wanapaswa kutii dhamiri zao zinapowasumbua na kutubu. Hivyo, makanisa mengi yameanza kufuata kile ambacho gazeti la Chicago Sun-Times, lilitaja kuwa ‘ujumbe unaoonwa kuwa wa Kikristo, lakini kwa kweli kusudi la ujumbe huo ni kuwafanya watu wajielekezee fikira na kupuuzilia mbali injili.’

Mtazamo huo umeibua aina ya makanisa ambayo yanamfafanua Mungu kulingana na maoni yao yenyewe. Badala ya kuhubiri kumhusu Mungu, makanisa hayo huzingatia watu na jinsi wanavyoweza kufanya ili waheshimiwe zaidi. Lengo kuu ni kuwaridhisha wafuasi wao. Hivyo, watu hao wana dini zisizo na mafundisho yoyote. Jarida The Wall Street Journal linauliza, “Ni nini ambacho kimechukua nafasi ya kanuni za maadili ya Kikristo? Kanuni pekee ya maadili iliyobaki ni kuwa wenye huruma sana na ‘kuwakubali wengine jinsi walivyo.’”

Hivyo basi, matokeo yamekuwa kwamba dini yoyote inayowafurahisha watu inakubalika. Kila mtu anayekubali mtazamo huo, lasema jarida The Wall Street Journal, “anaweza kuwa mfuasi wa dini yoyote ile, maadamu tu haizingatii viwango vyovyote vya maadili—dini inayowatuliza watu lakini si kuwahukumu.” Nayo makanisa yako tayari kuwakubali watu “jinsi walivyo” bila kujali viwango vyovyote vya maadili.

Huenda mambo hayo yakawakumbusha wasomaji wa Biblia unabii ulioandikwa na mtume Paulo katika karne ya kwanza. Alisema: “Kutakuwa na kipindi cha wakati ambapo hawatalivumilia fundisho lenye afya, bali, kwa kupatana na tamaa zao wenyewe, watajikusanyia walimu kwa ajili yao wenyewe ili masikio yao yafurahishwe; nao watageuza masikio yao kutoka kwenye kweli.”—2 Timotheo 4:3, 4.

Viongozi wa dini wanapopuuza dhambi, wanakataa kuwapo kwa dhambi, na ‘wanafurahisha’ masikio ya wafuasi wao kwa kuwaambia mambo wanayopenda kusikia badala ya kuwaambia kile ambacho Biblia inafundisha, wanawahatarisha sana watu. Ujumbe wa aina hiyo ni wa uwongo na ni hatari. Unapotosha mojawapo ya mafundisho ya msingi ya Ukristo. Fundisho kuhusu dhambi na msamaha lina sehemu muhimu katika habari njema ambayo Yesu na mitume wake walihubiri. Ili kupata habari zaidi kuhusu jambo hilo, unakaribishwa uendelee kusoma.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Fundisho hilo lisilo la kimaandiko limewatatanisha watu wengi, na huenda ndiyo sababu limeondolewa katika katekisimu za karibuni za Katoliki. Ona sanduku “Kanisa Labadili Fundisho Lake,” katika ukurasa wa 10.

^ fu. 14 Biblia haifundishi kwamba watu watateswa milele katika moto wa mateso. Kwa habari zaidi ona sura ya 6, “Wafu Wako Wapi?,” katika kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Blabu katika ukurasa wa 7]

Mwelekeo wa kufuata dini zenye lengo la kuwafurahisha watu huzaa matunda mabaya

[Sanduku katika ukurasa wa 6]

Dhambi? “Haituhangaishi Tena”

▪ “Suala hilo ndilo mojawapo ya vikwazo vikubwa vya kanisa leo. Hatujioni tena kuwa ‘watenda-dhambi’ wanaohitaji msamaha. Huenda dhambi ilikuwa ni tatizo wakati fulani, lakini sasa haituhangaishi tena. Kwa hiyo, ingawa kanisa linaweza kusuluhisha tatizo la dhambi, kwa Wamarekani wengi dhambi si tatizo.—angalau si tatizo kubwa.”—John A. Studebaker, Jr., mwandikaji wa mambo ya kidini.

▪ “Watu husema: ‘Nimejiwekea na kuwawekea wengine viwango vya juu vya maadili, lakini ninajua kwamba sote ni wanadamu, kwa hiyo nataka tu kufanya yale ninayoweza.’ Kuhusu suala la maadili, sisi hujitahidi kufanya yale ambayo tunaona kuwa sawa. Sisi hujitahidi kuwa majirani wema nasi huwasaidia jirani zetu kufanya mambo mbalimbali. Hata hivyo, tunapuuza uhalisi wa dhambi.”—Albert Mohler, msimamizi wa Seminari ya Theolojia ya Southern Baptist.

▪ “Leo, watu wanafurahia mambo ambayo zamani waliyaona kuwa ni yenye kuaibisha [kama zile zinazoitwa dhambi saba zilizo nzito]: wazazi wanawatia moyo watoto kuwa na kiburi kama ishara ya kujiheshimu; kikundi fulani cha wapishi nchini Ufaransa kimeliambia Kanisa Katoliki kwamba ulafi si dhambi. Wivu ndio huwafanya watu watake kuwa na vitu ambavyo watu mashuhuri wanavyo. Wafanyabiashara huwachochea watu kuwa na tamaa kupitia matangazo ya biashara, nayo hasira huonwa kuwa sawa ikiwa mtu amechokozwa. Mara nyingi mimi huamua tu kuwa mzembe.”—Nancy Gibbs, mwandikaji wa gazeti la Time.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Wengi leo huliona simulizi la Adamu na Hawa kuwa hadithi tu