Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Utatenda kwa Ushikamanifu”

“Utatenda kwa Ushikamanifu”

Mkaribie Mungu

“Utatenda kwa Ushikamanifu”

2 SAMWELI 22:26

TUNASIKIA uchungu sana wakati mtu ambaye tunamwamini anapotukatisha tamaa au anakosa kutimiza ahadi zake. Kukatishwa tamaa ni jambo la kawaida katika ulimwengu huu wenye watu wengi wasio washikamanifu. (2 Timotheo 3:1-5) Je, kuna mtu yeyote ambaye ataendelea kuwa mshikamanifu kabisa kwetu? Ebu tuchunguze maneno ya Daudi aliyekuwa mfalme wa taifa la kale la Israeli.

Daudi alikatishwa tamaa mara nyingi na watu waliokosa ushikamanifu kabisa. Alifukuzwa na kuteswa bila sababu nzuri na Sauli, mfalme wa kwanza wa Israeli, ambaye alimwonea wivu. Pia, Mikali aliyekuwa mke wa Daudi, hakuendelea kuwa mshikamanifu kwa mume wake, bali ‘alianza kumdharau moyoni mwake.’ (2 Samweli 6:16) Ahithofeli, mshauri ambaye Daudi alimtegemea sana, alimsaliti na akaunga mkono uasi dhidi ya Daudi. Ni nani aliyeongoza uasi huo? Si mwingine ila Absalomu, mwana wa Daudi! Baada ya kukatishwa tamaa mara nyingi hivyo, je, Daudi alikata kauli kwamba hakuna mtu hata mmoja ambaye ni mshikamanifu kabisa?

Maneno ya Daudi katika andiko la 2 Samweli 22:26 yanajibu swali hilo. Daudi aliyekuwa na imani imara aliimba hivi kumhusu Yehova Mungu: “Kwa mtu mshikamanifu utatenda kwa ushikamanifu.” Daudi alikuwa na hakika kwamba hata kama wanadamu wangemkatisha tamaa kabisa, Yehova angeendelea kuwa mshikamanifu kwake.

Na tuchunguze maneno ya Daudi kwa makini zaidi. Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “-tenda kwa ushikamanifu” linaweza pia kutafsiriwa “-tenda kwa fadhili zenye upendo.” Ushikamanifu wa kweli unategemea upendo. Yehova ni mshikamanifu kwa wale ambao ni washikamanifu kwake kwa sababu anawapenda. *

Ona pia kwamba ushikamanifu si hisia tu bali ni sifa inayomsukuma mtu atende. Daudi alijionea kwamba Yehova hutenda kwa ushikamanifu. Daudi alipokabili hali ngumu sana maishani mwake, Yehova alimlinda na kumwongoza kwa ushikamanifu mfalme huyo mwaminifu. Naye Daudi alimshukuru Yehova kwa kuwa alitambua kwamba Yeye ndiye aliyemwokoa “kutoka katika mkono wa adui zake wote.”—2 Samweli 22:1.

Maneno ya Daudi yanamaanisha nini kwetu? Yehova habadiliki-badiliki wala kugeuka-geuka. (Yakobo 1:17) Anaendelea kushikilia kanuni zake na kutimiza ahadi zake. Katika zaburi nyingine, Daudi aliandika hivi: “Yehova . . . hatawaacha washikamanifu wake.”—Zaburi 37:28.

Yehova anathamini ushikamanifu na utii wetu, na anatuhimiza tumwige kwa kuwatendea watu wengine kwa ushikamanifu katika shughuli zetu zote pamoja nao. (Waefeso 4:24; 5:1) Tunaweza kuwa na hakika kwamba hatatuacha kamwe iwapo tutakuwa washikamanifu katika njia hizo zote. Hata kama watu wanatukatisha tamaa kadiri gani, bila shaka Yehova atatutendea kwa ushikamanifu, na hivyo kutusaidia kukabili majaribu yoyote yale ambayo huenda tukapata. Je, umechochewa kumkaribia zaidi Yehova, Mungu wetu “Mshikamanifu”?—Ufunuo 16:5.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Andiko la 2 Samweli 22:26 linalingana na Zaburi 18:25. Zaburi hii imetafsiriwa hivi katika Biblia moja: “Kwa mtu mshikamanifu, Wewe utakuwa mwenye upendo mwingi.”—The Psalms for Today.