Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Wanafanya Nini Huku?”

“Wanafanya Nini Huku?”

Barua Kutoka Afrika Kusini

“Wanafanya Nini Huku?”

“ENEO HATARI—WIZI NA UKAHABA.” Onyo hili limeandikwa katika ubao, kando ya barabara nyembamba ya mashambani. Tunaondoka kwenye barabara hiyo na kuingia kwenye vumbi ili kujiunga na magari mengine machache yaliyoegeshwa chini ya ubao mwingine mkubwa ambao unaelekeza watu kwenye jengo la kuchezea kamari na hoteli ya starehe ambayo haiko mbali sana. Magari ya kifahari yanapita kwa kasi yakiwa yamebeba abiria ambao wanatutazama kwa mshangao, kana kwamba wanajiuliza, ‘Wanafanya nini huku?’

Tunaegesha gari na kushuka ili kujiunga na kikundi cha watu waliovalia nadhifu na ambao wamesimama chini ya kivuli cha ubao huo. Watu katika kikundi hiki ni wa jamii na makabila mbalimbali. Jambo ambalo bado si kawaida sana kuliona huku Afrika Kusini. Tumesafiri umbali wa kilomita 100 hivi, kaskazini-magharibi ya Johannesburg, ili kuhubiri kweli za Biblia katika vijiji vilivyo hapa.

Tunafanya mkutano mfupi kando ya barabara ili kuzungumzia andiko la Biblia na kukamilisha mipango ya kuhubiri katika eneo hili. Tunatoa sala na kurudi kwenye magari yetu ili kuelekea vijijini. Eneo hili tambarare lina nyumba nyingi na vibanda vilivyojengwa bila mpangilio wowote. Vilima vikubwa vyeusi vya mabaki yanayotoka katika migodi ya platinamu vinafanya nyumba na vibanda hivi vionekane vidogo sana. Umaskini umeenea sana hapa licha ya kuwa ni eneo lenye madini yaliyo na thamani kubwa.

Mimi na mke wangu tunaanza kuhubiri nyumba kwa nyumba tukiwa pamoja na wageni wawili kutoka Ujerumani. Asilimia 33 hivi ya wakaaji wa vijiji hivi hawana kazi na hivyo, makao yao ni duni. Makao ya wengi yamejengwa kwa mabati yaliyopigiliwa kwa misumari kwenye mbao hafifu. Ili kuzuia mabati hayo yasing’oke, vifuniko vya chupa vimepigiliwa pamoja na misumari.

Tunapokaribia kila nyumba, tunamsalimu mwenye nyumba tukiwa langoni na mara nyingi tunakaribishwa na mama mwenye nyumba. Watu tunaozungumza nao wana hamu ya kutusikiliza na wanatutendea kama wageni waheshimiwa. Watoto wanatumwa kuleta viti na kuviweka chini ya mti kwa kuwa jua linalowaka linachoma mabati na kuifanya nyumba iwe na joto sana. Tunaombwa kuketi chini ya mti.

Familia yote inakusanyika na kuketi kwenye viti vidogo au masanduku. Hata watoto wadogo ambao wanacheza na vitu vya kuchezea vilivyotengenezewa nyumbani, wanaitwa waje wasikilize. Tunasoma maandiko pamoja nao na kuwaomba watoto ambao wanaenda shule, wasome sehemu fulani katika vitabu vyetu vya Biblia. Karibu kila mtu ambaye tunakutana naye anakubali vitabu vyetu kwa furaha, na wengi wanatuomba turudi tena.

Wakati wa mchana, tunapumzika kidogo na kula mkate pamoja na kinywaji baridi kabla ya kurudi ili kuwatembelea wale ambao tulikuwa tumewatembelea pindi nyingine. Kwanza, tunaenda kumwona Jimmy, mhamiaji kutoka Malawi ambaye anafanya kazi kwenye mgodi mmoja wa platinamu katika eneo hili. Tumekuwa tukimtembelea Jimmy kwa miezi kadhaa. Siku zote yeye hufurahi kutuona na tumekuwa tukizungumzia Biblia pamoja naye. Jimmy ameoa mke wa kabila moja la Afrika Kusini na wana watoto wawili wazuri. Tunatamani kumwona kwa sababu hatukumpata nyumbani wakati uliopita.

Tunapokaribia nyumba duni ya Jimmy, mara moja tunatambua kwamba kuna shida fulani. Shamba lake dogo ambalo lilipendeza sikuzote halijatunzwa, mimea yake ya mahindi imekauka, na hatuoni kuku ambao kwa kawaida huwa pale wakichakura udongo kutafuta chakula. Mlango umefungwa upande wa nje kwa mnyororo mkubwa. Mama fulani ambaye ni jirani ya Jimmy anakuja ili kuona kile kinachoendelea. Tunamuuliza aliko Jimmy. Naye anatujulisha habari zenye kushtua: Jimmy amekufa na mke wake amerudi kwa wazazi wake pamoja na watoto.

Tunauliza kilichosababisha kifo chake ingawa jambo hilo huonwa kuwa lisilo la heshima. Anatuambia, “Alikuwa mgonjwa, na kisha akafa. Siku hizi kuna magonjwa mengi. Watu wengi wanakufa.” Hataji sababu hususa ya kifo chake kwa kuwa watu hawapendi kuzungumzia mambo kama hayo. Hata hivyo, idadi inayoongezeka ya makaburi mapya katika eneo la kuzikia watu, ni uthibitisho wenye kuhuzunisha kwamba maneno ya jirani ya Jimmy ni ya kweli. Tunazungumzia tumaini la ufufuo pamoja na mama huyo kwa muda, kisha tunaondoka tukiwa na huzuni kwenda kumtembelea mtu mwingine.

Tunaenda kwenye kijiji kingine na kuendesha gari mpaka nyumba za mwisho ambako kuna rundo kubwa la mabaki ya migodi. Tunageuka na kuingia kwenye kijia kinachoelekea kwenye nyumba ya mtu fulani. Kwenye mawe yaliyo bustanini, kuna maneno yaliyoandikwa kwa rangi nyang’avu ambayo yanamaanisha kwamba kusitasita na kuahirisha jambo hupoteza wakati mwingi sana. David, * ambaye ameandika maneno hayo anainua kichwa chake akiwa nyuma ya injini ya gari lake zee, aina ya Volkswagen Beetle. Analitupia jicho jua la jioni na kisha kutabasamu sana anapotutambua, huku vibandiko vya dhahabu vilivyo kwenye meno yake ya mbele viking’aa. Anapanguza mikono yake na kutusalimu.

“Hamjambo rafiki zangu!” anatusalimu. “Sijawaona kwa siku nyingi!” Tunafurahi kumwona David tena. Anatuomba radhi kwamba hatutaweza kuzungumza sana kwa sababu tangu tulipoonana, amepata kazi katika mgodi na anahitaji kwenda huko muda mfupi baadaye. David hakosi kutabasamu muda wote wa mazungumzo yetu yenye uchangamfu. Anasema kwa furaha: “Maisha yangu yalibadilika siku ya kwanza ambayo tulikutana. Kwa kweli sijui ningekuwa wapi leo kama hatungekutana.”

Tunamuaga David tukiwa na furaha. Tunaligeuza gari na kuelekea nyumbani huku jua likianza kutua. Tunatazama kwa mara ya mwisho eneo hili tambarare ambalo kwa sasa halionekani vizuri kwa sababu ya vumbi iliyo hewani, na kuwaza kuhusu jinsi ambavyo habari njema zitawafikia wakaaji wote wa eneo hili. Tunaona ukweli wa maneno haya ya Yesu: “Kwa kweli, mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache.”—Luka 10:2.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 12 Jina limebadilishwa.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 17]

Kind permission given by the South African Post Office