Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Watetezi wa Imani—Je, Walikuwa Watetezi wa Imani au Wanafalsafa?

Watetezi wa Imani—Je, Walikuwa Watetezi wa Imani au Wanafalsafa?

Watetezi wa Imani—Je, Walikuwa Watetezi wa Imani au Wanafalsafa?

KATIKA miaka ya 100 W.K., Wakristo walishtakiwa bila msingi wowote kwamba walifanya ngono na watu wa familia zao, waliwaua watoto, na kuwala watu. Hilo lilisababisha mateso makali hivi kwamba waandikaji waliojidai kuwa Wakristo waliona uhitaji wa kutetea imani yao. Baadaye waandikaji hao waliitwa watetezi wa imani, na lengo lao lilikuwa kuthibitisha kuwa dini yao si hatari ili ikubaliwe na wenye mamlaka na raia wa Milki ya Roma. Mradi huo ulikuwa hatari kwa kuwa mara nyingi wenye mamlaka na raia waliridhika tu wakati matakwa na mapendezi yao yalipotimizwa. Pia, huenda mradi huo ungechochea mateso makali zaidi, au labda Wakristo wangepunguza uzito wa ujumbe wao kwa kushinikizwa kukana imani yao. Waandikaji hao walitetea imani yao kwa njia gani? Walitoa hoja zipi? Na matokeo ya jitihada zao yalikuwa nini?

Watetezi wa Imani Katika Milki ya Roma

Watetezi wa imani walikuwa wanaume wenye elimu walioishi katika miaka ya 100 na miaka ya mapema ya 200. Waliokuwa maarufu zaidi kati yao ni Justin Martyr, Klementi wa Aleksandria, na Tertuliani. * Waliwaandikia hasa wapagani na wenye mamlaka wa Milki ya Roma ili kuwaelezea imani ya Kikristo, na mara nyingi walirejelea Biblia katika maandishi yao. Zaidi ya yote, waandikaji hao waliwapinga wale waliowatesa Wakristo, wakakanusha mashtaka yao, na kuonyesha kwamba Wakristo ni watu wema.

Hangaiko moja kuu la waandikaji hao lilikuwa kuwathibitishia wenye mamlaka kwamba Wakristo hawakuwa maadui wa maliki wala maadui wa Milki ya Roma. Tertuliani alisema, ‘Mungu wetu amemweka maliki mamlakani.’ Athenagoras naye alitetea haki ya watu wa familia ya maliki kuurithi utawala. Hivyo, walijiingiza katika siasa ya siku hizo, na wakapuuza maneno ya Yesu Kristo aliyesema: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu.”—Yohana 18:36.

Watetezi hao wa imani pia walidai kwamba kulikuwa na uhusiano fulani kati ya Milki ya Roma na Ukristo. Melito aliamini kwamba Ukristo ulichangia ufanisi wa Milki ya Roma kwa kufanya muungano na milki hiyo. Mwandikaji wa barua inayoitwa The Epistle to Diognetus, ambaye jina lake halijulikani, alisema Wakristo ni sehemu muhimu sana ya ulimwengu hivi kwamba ‘wanauunganisha ulimwengu.’ Tertuliani naye aliandika kwamba Wakristo walikuwa wakimwomba Mungu aifanikishe Milki ya Roma, na pia aahirishe mwisho wa ulimwengu. Basi, kuja kwa Ufalme wa Mungu hakukuonekana tena kuwa muhimu sana.—Mathayo 6:9, 10.

Jinsi “Ukristo” Ulivyofanywa Kuwa Falsafa

Mwanafalsafa anayeitwa Celsus aliwafafanua Wakristo kwa dharau kuwa “wafanyakazi wa hali ya chini, washona-viatu, wakulima, watu wasio na elimu, na wapumbavu.” Watetezi wa imani hawakuweza kuvumilia dharau hiyo. Waliazimia kutumia mbinu mpya ili kuwasaidia watu wawe na maoni mazuri kuwahusu Wakristo. Ili kutetea “Ukristo” walianza kutumia hekima ya ulimwengu ambayo walikuwa wameikataa hapo awali. Kwa mfano, Klementi wa Aleksandria, aliiona falsafa kuwa “elimu ya kweli ya dini.” Justin naye alidai kwamba anakataa falsafa ya kipagani, hata hivyo, alikuwa mtu wa kwanza kutumia maneno na mawazo ya wanafalsafa kuelezea mafundisho ya “Kikristo.” Pia, alisema kwamba falsafa ya aina hiyo “haina madhara na ni yenye manufaa.”

Kuanzia wakati huo waandikaji hao hawakupinga tena falsafa, bali walijitahidi kufanya mafundisho ya Kikristo kuwa falsafa bora kuliko falsafa za wapagani. Justin aliandika hivi: “Baadhi ya mafundisho yetu ni sawa kabisa na mafundisho ya washairi na wanafalsafa mnaowaheshimu, lakini kuhusu mambo mengine mafundisho yetu ni bora kwa sababu yanatokana na Mungu.” Walipoanza kutumia maneno na semi za wanafalsafa, watetezi wa imani walifanya mafundisho yaliyoonwa kuwa ya “Kikristo” yawe yenye kukubalika na kuheshimika zaidi. Watetezi wa imani walionyesha kwamba vitabu vya Kikristo vilikuwa vya kale sana kuliko vitabu vya Wagiriki, na kuwa manabii wa Biblia waliishi miaka mingi kabla ya wanafalsafa Wagiriki. Wengine wao walikata kauli kwamba wanafalsafa walinukuu maneno ya manabii. Hata walidai kwamba Plato alikuwa mwanafunzi wa Musa!

Jinsi Ukristo Ulivyopotoshwa

Mbinu hiyo mpya ilisababisha mchanganyiko wa mafundisho ya Kikristo na falsafa za kipagani. Miungu ya Wagiriki ililinganishwa na watu wanaotajwa katika Biblia. Yesu alilinganishwa na Perseusi; na mimba ya Maria ililinganishwa na mimba ya mama ya Perseusi, anayeitwa Danaë. Kama Maria, Danaë aliaminiwa kuwa bikira alipochukua mimba.

Baadhi ya mafundisho yalibadilishwa sana. Kwa mfano, katika Biblia, Yesu anaitwa “Logos,” yaani, “Neno” la Mungu, au Msemaji wa Mungu. (Yohana 1:1-3, 14-18; Ufunuo 19:11-13) Katika siku za mapema, Justin alipotosha fundisho hilo. Yeye alifanya kama wanafalsafa walivyofanya. Alikazia maana mbili za neno la Kigiriki, logos, yaani, “neno” au “uwezo wa kutumia akili.” Alisema kwamba Wakristo walipokea neno kwa kumpokea Kristo mwenyewe. Hata hivyo, maana ya pili ya neno logos ni uwezo wa kutumia akili, na wanadamu wote, hata wapagani, wanatumia akili. Kwa hiyo, alikata kauli kwamba wote wanaotumia akili ni Wakristo, hata watu kama vile Sokrate na wengineo ambao walidai kwamba hakuna Mungu au walioonwa kuwa watu wasiomwamini Mungu.

Isitoshe, kwa kujitahidi sana kuonyesha kwamba Yesu ni logos kupatana na maoni ya wanafalsafa Wagiriki, ambao pia walihusianisha neno hilo na Mungu, watetezi wa imani, kama vile Tertuliani, walitokeza wazo ambalo hatimaye lilifanya fundisho la Utatu liwe eti fundisho la Kikristo. *

Neno “nafsi” linapatikana zaidi ya mara 850 katika Biblia, kutia ndani zaidi ya mara 100 katika lugha ya Kigiriki. Mara nyingi linarejelea viumbe hai wanaoweza kufa, kama vile wanadamu na wanyama. (1 Wakorintho 15:45; Yakobo 5:20; Ufunuo 16:3) Hata hivyo, watetezi wa imani walipotosha fundisho hilo la Biblia kwa kulihusianisha na falsafa ya Plato ambaye alifundisha kwamba nafsi si sehemu ya mwili, haionekani kwa macho, na haiwezi kufa. Minusio Feliksi hata alisema kuwa fundisho la ufufuo lilitokana na fundisho la Pythagoras aliyefundisha kwamba mtu anapokufa, nafsi inahama na kuingia katika mwili mwingine. Falsafa ya Wagiriki ilikuwa imepotosha sana mafundisho ya Biblia.

Uchaguzi Mbaya

Watetezi kadhaa wa imani walitambua kwamba falsafa ingeweza kupotosha imani ya Kikristo. Hata hivyo, ijapokuwa waliwachambua wanafalsafa, bado walipenda sana mawazo na njia ya kufikiri ya wanafalsafa. Kwa mfano, Tatian aliwashutumu wanafalsafa kwa sababu hawakutimiza chochote chema, lakini wakati uleule akauita Ukristo “falsafa yetu” na kujishughulisha na makisio ya kifalsafa. Tertuliani naye alilalamika kwamba falsafa za kipagani zinapotosha mafundisho ya Kikristo. Kwa upande mwingine, alisema kuwa alitaka kufuata nyayo za “mwanafalsafa Justin aliyefia imani, na Miltiade, mwanafalsafa wa makanisa,” na wengineo. Athenagoras aliitwa “mwanafalsafa Mkristo wa Athene.” Klementi naye alikuwa na maoni kwamba “Wakristo wanaweza kutumia falsafa kwa busara ili kupata hekima na kuitetea imani.”

Labda watetezi hao wa imani walifanikiwa kwa kadiri fulani kutetea imani yao, hata hivyo, walikuwa wamefanya kosa zito. Walikuwa wamefanya kosa gani? Mtume Paulo aliwakumbusha Wakristo kwamba kati ya silaha zao za kiroho, silaha bora zaidi ni “neno la Mungu,” ambalo ‘liko hai na lina nguvu.’ Paulo alisema kuwa tunalitumia ‘kupindua mawazo na kila jambo lililo juu sana ambalo limeinuliwa kinyume cha ujuzi wa Mungu.’—Waebrania 4:12; 2 Wakorintho 10:4, 5; Waefeso 6:17.

Yesu alipokuwa pamoja na wanafunzi wake usiku wa mwisho kabla ya kuuawa, aliwaambia hivi: “Jipeni moyo! Mimi nimeushinda ulimwengu.” (Yohana 16:33) Majaribu aliyopata na dhiki alizopitia alipokuwa duniani hazikudhoofisha imani yake wala ushikamanifu wake kwa Baba yake. Vivyo hivyo, mtume Yohana aliyekuwa mtume wa mwisho kufa aliandika hivi: “Huu ndio ushindi ambao umeushinda ulimwengu, imani yetu.” (1 Yohana 5:4) Ingawa watetezi wa imani walitaka kuutetea Ukristo, walifanya uamuzi mbaya kwa kukubali mawazo na njia za kufikiri za wanafalsafa wa ulimwengu. Walipofanya hivyo, waliruhusu falsafa kama hizo ziwapotoshe, na pia waliruhusu ulimwengu uwashinde wao, na njia yao ya Ukristo. Kwa hiyo, badala ya kuitetea na kupigania imani ya kweli ya Kikristo, watetezi wa imani wa kanisa la mapema walianguka, labda bila kutambua, katika mtego wa Shetani ambaye “huendelea kujigeuza mwenyewe kuwa malaika wa nuru.”—2 Wakorintho 11:14.

Makasisi na wasomi wa dini leo wamefanya vivyo hivyo. Badala ya kutetea Ukristo wa kweli kwa kutumia Neno la Mungu, mara nyingi wanapuuza Biblia na kurejelea falsafa za ulimwengu katika mafundisho yao ili wakubaliwe na watu na wenye mamlaka pia. Badala ya kuwashauri watu wasifuate mwenendo wa ulimwengu huu usiopatana na Biblia, wamekuwa walimu wanaofanya yote wawezayo ‘kufurahisha masikio’ ya wasikilizaji wao ili kupata wafuasi. (2 Timotheo 4:3) Kama walivyofanya watetezi wa imani wa kale, walimu hao wamepuuza onyo hili la mtume Paulo: “Mjihadhari: labda kuna mtu ambaye atawachukua ninyi kama windo lake kupitia falsafa na udanganyifu mtupu kulingana na pokeo la wanadamu, kulingana na mambo ya msingi ya ulimwengu na si kulingana na Kristo.” Na anatukumbusha kwamba “mwisho wao utakuwa kulingana na matendo yao.”—Wakolosai 2:8; 2 Wakorintho 11:15.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Pia, Kwadrato, Aristides, Tatian, Apollinaris, Athenagoras, Theofilo, Melito, Minusio Feliksi, na waandikaji wengineo wasio maarufu sana, walikuwa watetezi wa imani. Ona toleo la Mnara wa Mlinzi la Mei 15, 2003, ukurasa wa 27-29, na la Machi 15, 1996, ukurasa wa 28-30.

^ fu. 13 Ili kupata habari zaidi kuhusu mafundisho ya Tertuliani, ona toleo la Mnara wa Mlinzi la Mei 15, 2002, ukurasa wa 29-31.

[Blabu katika ukurasa wa 31]

“Tunapindua mawazo na kila jambo lililo juu sana ambalo limeinuliwa kinyume cha ujuzi wa Mungu.”—2 WAKORINTHO 10:5

[Picha katika ukurasa wa 28]

Justin alisema kuwa falsafa “haina madhara na ni yenye manufaa”

[Picha katika ukurasa wa 29]

Klementi aliiona falsafa kuwa “elimu ya kweli ya dini”

[Picha katika ukurasa wa 29]

Falsafa ya Tertuliani ilifanya fundisho la Utatu likubaliwe

[Picha katika ukurasa wa 29]

Tatian aliuita Ukristo “falsafa yetu”

[Picha katika ukurasa wa 30]

Makasisi na wasomi wa dini leo wamewaiga watetezi wa imani

[Picha katika ukurasa wa 31]

Mtume Paulo alionya kuhusu falsafa na udanganyifu wa wanadamu

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 29]

Clement: Historical Pictures Service; Tertullian: © Bibliothèque nationale de France