Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Zeri ya Gileadi—Mafuta Yanayoponya

Zeri ya Gileadi—Mafuta Yanayoponya

Zeri ya Gileadi—Mafuta Yanayoponya

SIMULIZI linalojulikana sana katika kitabu cha Biblia cha Mwanzo linataja kisa cha Yosefu akiuzwa na ndugu zake kwa wafanyabiashara Waishmaeli ambao wanaelekea Misri. Msafara wa wafanyabiashara hao unatoka Gileadi na ngamia wao wamebeba zeri na bidhaa nyingine ili kuzipeleka Misri. (Mwanzo 37:25) Simulizi hili fupi linaonyesha kuwa zamani zeri ilipendwa na kuthaminiwa sana katika Mashariki ya Kati kwa sababu ya nguvu zake maalum za kuponya.

Hata hivyo, karne kadhaa baadaye, nabii Yeremia aliuliza hivi kwa huzuni: “Je, hakuna zeri katika Gileadi?” (Yeremia 8:22) Kwa nini Yeremia aliuliza swali hilo? Zeri ni nini? Je, leo kuna zeri inayotumiwa kuponya?

Zeri Katika Nyakati za Biblia

Zeri ni neno la ujumla linalorejelea umajimaji unaotokana na mimea, na ambao una harufu nzuri, mafuta, na utomvu. Mafuta ya zeri ambayo yalitumiwa mara nyingi katika uvumba na manukato, yalikuwa kati ya vitu vya anasa siku za kale huko Mashariki ya Kati. Zeri ilikuwa moja kati ya vitu vilivyotumiwa kutengeneza mafuta matakatifu yaliyotumiwa kutia mafuta, na uvumba uliotumiwa katika hema ya kukutania muda mfupi baada ya Waisraeli kutoka Misri. (Kutoka 25:6; 35:8) Pia, zeri ilikuwa kati ya zawadi nyingi ambazo malkia wa Sheba alimletea Mfalme Sulemani. (1 Wafalme 10:2, 10) Kabla ya kwenda mbele ya Mfalme Ahasuero wa Uajemi, Esta alirembeshwa na kukandwa kwa “miezi sita kwa mafuta ya zeri”—Esta 1:1; 2:12.

Ingawa mafuta ya zeri yalitoka katika maeneo mengi ya Mashariki ya Kati, zeri ya Gileadi ilitoka Nchi ya Ahadi. Eneo la Gileadi lilikuwa mashariki ya Mto Yordani. Mzee wa ukoo Yakobo, aliiona zeri kuwa kati ya “mali bora zaidi ya nchi” na hivyo akaituma Misri kama zawadi. (Mwanzo 43:11) Naye nabii Ezekieli aliorodhesha zeri kati ya bidhaa ambazo watu wa Yuda na Israeli waliwauzia watu wa Tiro. (Ezekieli 27:17) Zeri ilijulikana sana kwa nguvu zake maalum za kitiba. Vitabu vya kale vinataja mara nyingi nguvu za kuponya na za kutuliza za mafuta hayo, hasa kuhusiana na kutibu majeraha.

Zeri kwa Ajili ya Taifa Lenye Majeraha

Kwa nini basi Yeremia aliuliza, “Je, hakuna zeri katika Gileadi”? Ili kuelewa sababu ya kuuliza swali hilo, tunahitaji kujua hali katika taifa la Israeli wakati huo. Kabla ya hapo, nabii Isaya alikuwa ameeleza wazi hali mbaya ya kiroho ya taifa hilo: “Kuanzia wayo wa mguu mpaka kwenye kichwa hakuna mahali pasipo na kasoro. Majeraha na machubuko na mapigo ya hivi karibuni—hayakufinywa yatoe usaha wala kufungwa.” (Isaya 1:6) Badala ya kutambua hali yao yenye kusikitisha na kutafuta tiba, watu wa taifa hilo waliendelea katika njia yao mbaya. Yeremia aliomboleza hivi katika siku zake: “Wamelikataa neno la Yehova, nao wana hekima gani?” (Yeremia 8:9) Kama wangemrudia Yehova, angewaponya. “Je, hakuna zeri katika Gileadi?” Hilo ni swali lenye kuchochea fikira kama nini!

Katika njia nyingi, ulimwengu wa leo umejaa “majeraha na machubuko na mapigo ya hivi karibuni.” Watu wanateseka kwa sababu ya umaskini, ukosefu wa haki, ubinafsi, na ukosefu wa fadhili, kwa kuwa upendo kwa Mungu na jirani umepoa. (Mathayo 24:12; 2 Timotheo 3:1-5) Wengi wanahisi kuwa wamebaguliwa kwa sababu ya jamii, kabila, au umri wao. Zaidi ya hayo, wanaumia kwa sababu ya ukosefu wa chakula, magonjwa, vita, na kifo. Kama Yeremia, waamini wengi wanyofu wanajiuliza kama kuna “zeri katika Gileadi” ambayo wanaweza kutumia ili kufunga majeraha ya kihisia na ya kiroho ya wale wanaoteseka.

Habari Njema Inayoponya

Katika siku za Yesu, watu wanyenyekevu walijiuliza vivyo hivyo. Lakini walipata jibu. Akiwa katika sinagogi huko Nazareti mwanzoni mwa mwaka wa 30 W.K., Yesu alisoma kitabu cha kukunjwa cha Isaya kinachosema: “Yehova amenitia mafuta niwatangazie wapole habari njema. Amenituma kufunga majeraha ya waliovunjika moyo.” (Isaya 61:1) Kisha, Yesu akasema maneno hayo yanamhusu yeye mwenyewe, na akajitambulisha kuwa Masihi aliyetumwa kuwatangazia watu ujumbe wa faraja.—Luka 4:16-21.

Katika huduma yake yote, Yesu alihubiri kwa bidii habari njema ya Ufalme wa Mungu. (Mathayo 4:17) Katika Mahubiri ya Mlimani, aliwaahidi walioteseka kwamba hali zao zingebadilika: “Wenye furaha ni ninyi mnaolia sasa, kwa sababu mtacheka.” (Luka 6:21) Kwa kutangaza kuja kwa Ufalme wa Mungu—ujumbe wa tumaini—Yesu ‘alifunga majeraha ya waliovunjika moyo.’

Katika siku zetu, sisi pia tunafarijiwa na “habari njema ya ufalme.” (Mathayo 6:10; 9:35) Kwa mfano, fikiria kisa cha Roger na Liliane. Mnamo Januari (Mwezi wa 1) 1961, walijifunza kwa mara ya kwanza kuhusu ahadi ya Mungu ya uzima wa milele, na jambo hilo lilikuwa kama mafuta yanayotuliza. Liliane anakumbuka: “Nilicheza-cheza jikoni nilipofikiria yale ambayo nilikuwa nikijifunza. Nilifurahi sana.” Roger, ambaye kwa wakati huo alikuwa amepooza kwa miaka kumi katika sehemu fulani ya mwili wake, anaongeza: “Nilipata shangwe kubwa sana maishani kwa sababu ya tumaini hilo zuri, yaani, tumaini la ufufuo na mwisho wa uchungu na maumivu.”—Ufunuo 21:4.

Katika mwaka wa 1970, Roger na Liliane walifiwa na mwana wao mwenye miaka 11. Lakini hawakukata tamaa. Walihisi kwamba Yehova “anawaponya wenye mioyo iliyovunjika, naye anafunga sehemu zao zenye maumivu.” (Zaburi 147:3) Tumaini lao liliwafariji sana. Sasa, kwa miaka karibu 50, habari njema ya Ufalme wa Mungu unaokuja imewaletea amani na uradhi.

Uponyaji wa Wakati Ujao

Hivyo, je, kuna “zeri katika Gileadi” leo? Ndiyo, leo bado kuna zeri ya kiroho. Habari njema ya Ufalme inaweza kuwapa watu tumaini na faraja ambazo zinaweza kuponya mioyo iliyovunjika. Je, ungependa kupata uponyaji kama huo? Kile tu unachohitaji kufanya ni kufungua moyo wako ili ukubali ujumbe wenye faraja kutoka katika Neno la Mungu na kuufuata maishani mwako. Tayari mamilioni ya watu wamefanya hivyo.

Uponyaji unaoletwa na mafuta ya zeri unaonyesha kwamba kuna kitulizo kikubwa ambacho bado kitakuja. Karibuni sana, Yehova Mungu ‘ataponya mataifa’ ili watu wapate uzima wa milele. Wakati huo, “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’” Ndiyo, bado kuna “zeri katika Gileadi”!—Ufunuo 22:2; Isaya 33:24.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Nguvu za kuponya za habari njema ya Ufalme wa Mungu zinaendelea kutuliza uchungu wa watu waliovunjika moyo leo