Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

MZAZI asiyekuwa na mwenzi huko Urusi aliimarishaje uhusiano wake na watoto wake na kuacha uraibu wa dawa za kulevya? Mwanamume asiyekuwa na makao huko Kyoto, Japani, alipata wapi nguvu za kushinda udhaifu wake uliofanya awe maskini? Ni nini kilichomsaidia mchungaji mmoja kutoka Australia aache ulevi? Fikiria mambo ambayo watu hao wanasema.

“Nilijifunza kuwa nina wajibu wa kujitegemeza.”—NELLY BAYMATOVA

UMRI: 45

NCHI: URUSI

HISTORIA: MRAIBU WA DAWA ZA KULEVYA

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nililelewa Vladikavkaz, mji mkuu wa Jamhuri ya Ossetia Kaskazini (ambayo sasa inaitwa Alania). Familia yetu ilikuwa yenye utajiri. Lakini sikuwa na furaha maishani ingawa tulikuwa na mali nyingi. Nilipofikia umri wa miaka 34, tayari nilikuwa nimeolewa mara mbili lakini ndoa zangu hazikufaulu. Nilikuwa mraibu wa dawa za kulevya kwa miaka kumi, na nikatibiwa mara mbili katika hospitali. Ingawa nilikuwa na watoto wawili, sikuhisi upendo wowote kuwaelekea; wala sikuwa na uhusiano wa kawaida na rafiki zangu wala na watu wa familia yangu.

Mama yangu alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, na mara kwa mara nilimsikia akimlilia Yehova na kumwomba anisaidie. Nilijiwazia: ‘Mama yangu ni mpumbavu jinsi gani! Yehova anaweza kunisaidia kwa njia gani?’ Nilijaribu kuacha kutumia dawa za kulevya, lakini sikuwa na nguvu za kuacha uraibu huo bila msaada. Wakati fulani, nilikaa siku mbili bila kutumia dawa hizo. Kisha nikaamua kuwa ninahitaji kutoka katika nyumba na hivyo nikaruka kupitia dirishani. Jambo la kusikitisha ni kwamba, nilikuwa kwenye ghorofa ya pili. Nilivunjika mkono na mguu, na mgongo wangu ukaumia pia. Nililazimika kukaa kitandani kwa zaidi ya mwezi mmoja.

Nilipokuwa nikiuguza majeraha yangu, mama yangu alinitunza na hakunishutumu. Alijua kwamba nilikuwa na tatizo la kudhibiti hisia zangu na pia tatizo la akili. Hata hivyo, aliniwekea nakala za gazeti la Amkeni! * kando ya kitanda changu. Nilisoma gazeti moja baada ya lingine na nikapata kuwa yalikuwa yenye kupendeza na kuelimisha. Kisha nikaamua kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Jambo moja ambalo nilijifunza katika Biblia ni kuwajibika. Badala ya kutarajia mama yangu anitegemeze, nilijifunza kuwa nina wajibu wa kujitegemeza na hata kuwategemeza watoto wangu kifedha. Baada ya kuwa huru na kufanya kile ninachotaka kwa muda mrefu, haikuwa rahisi kufanya kazi kwa ukawaida.

Pia, kanuni iliyo katika Kumbukumbu la Torati 6:5-7, inayowashauri wazazi wawafundishe watoto wao kumhusu Mungu, ilinisaidia sana. Nilitambua kuwa nitatoa hesabu mbele za Mungu kuhusu jinsi ninavyowalea watoto wangu wawili. Jambo hilo lilinichochea nitumie wakati mwingi pamoja nao na kusitawisha upendo kuwaelekea.

Nilithamini kwa moyo wote kuwa Mungu aliniruhusu nijifunze kweli kumhusu. Hivyo, nikajiweka wakfu kwake na kubatizwa na kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Kwa sababu nilijifunza jinsi ya kudhibiti hasira yangu, uhusiano wangu pamoja na mama yangu uliimarika. Uhusiano wangu pamoja na watoto wangu umeboreka pia.

Kwa kuwa sasa ninachukia vitu vinavyomchukiza Mungu, matatizo mengi yaliyosababishwa na maisha yangu ya hapo awali yametoweka. Sasa ninapata furaha nyingi kwa kuwasaidia wengine wajifunze ukweli kumhusu Yehova Mungu.

“Ninahisi kama maisha yangu yaliokolewa kihalisi.”—MINORU TAKEDA

UMRI: 54

NCHI: JAPANI

HISTORIA: ALIISHI MITAANI

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nililelewa na baba na nyanya katika mji wa Yamaguchi. Sikumjua mama yangu. Nyanya yangu alikufa nikiwa na umri wa miaka 19, na nikaendelea kuishi na baba yangu. Nilifanya kazi ya upishi, na baba yangu alifanya kazi hiyohiyo. Ratiba yetu ya kazi ilitofautiana, hivyo hatukuonana sana. Nikaanza kuwa na tabia ya kufanya kazi kwa saa nyingi na kunywa pombe na rafiki zangu.

Muda si muda nilianza kuchoshwa na kazi yangu. Nilibishana na mwajiri wangu na nikaanza kunywa kileo kupita kiasi. Mwishowe, nilipokaribia umri wa miaka 30, niliamua kuondoka nyumbani na kusafiri huku na huku. Pesa zangu zilipoisha, nilianza kufanya kazi katika mkahawa wa kuchezea kamari. Nilikutana na msichana mmoja na tukaoana. Lakini tukatengana baada ya miaka miwili na nusu tu.

Nilishuka moyo sana, nikawa geugeu, na mwenye madeni mengi. Niliwatoroka watu walionidai pesa na kurudi nyumbani kuishi na baba yangu, lakini nilimdanganya na tukakosana. Niliiba kiasi fulani cha pesa zake na kwenda kucheza kamari kwa muda. Hatimaye, nikawa maskini hohehahe na kuishi kwenye kituo cha garimoshi kwa muda. Nilihamia Hakata, kisha Himeji, na mwishowe jiji la Kyoto. Niliishi mitaani kwa miaka kadhaa.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Mnamo 1999, nilikuwa katika bustani fulani karibu na Mto Kamogawa huko Kyoto wakati wanawake wawili waliponikaribia. Mmoja wao aliniuliza, “Je, ungependa kujifunza Biblia?” Nilikubali mwaliko huo. Wakristo wakomavu wa kutaniko la Mashahidi wa Yehova la eneo hilo walijifunza Biblia nami na kunisaidia kutambua umuhimu wa kutumia kanuni zake. Walinishauri nitafute kazi na mahali pa kuishi. Ili niwapendeze nilienda kwenye mahojiano kadhaa ya kazi, lakini sikufanya hivyo kwa bidii. Hata hivyo, baadaye nilianza kusali ili nipate msaada, nikatafuta kazi kwa bidii, na mwishowe nikapata kazi.

Sala pia ilinisaidia wakati jaribu gumu lilipozuka. Wale watu waliokuwa wakinidai pesa walinitafuta hadi wakanipata na kutaka pesa zao. Jambo hilo lilinifadhaisha sana. Katika usomaji wangu wa Biblia wa kila siku, nilipata maneno ya Isaya 41:10. Katika mstari huo, Mungu anawaahidi hivi watumishi wake waaminifu: ‘Nitawasaidia kwelikweli.’ Ahadi hiyo ilinitia nguvu na kunipa ujasiri. Nilifanya kazi kwa bidii na mwishowe nikafaulu kulipa madeni yangu. Katika mwaka wa 2000, nilibatizwa na kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Nilichojifunza katika Biblia kilinichochea nirekebishe uhusiano wangu pamoja na baba yangu, naye akanisamehe makosa yangu ya hapo awali. Alifurahi sana kwa sababu nilikuwa nimejifunza kuishi kupatana na kanuni za Biblia. Ninahisi kama maisha yangu yaliokolewa kihalisi kwa sababu nilianza kuishi kupatana na kanuni za Biblia.

Kwa kuongezea, sasa ninaweza kufanya kazi na kujitegemeza. (Waefeso 4:28; 2 Wathesalonike 3:12) Pia, nimepata marafiki wa kweli katika kutaniko la Kikristo. (Marko 10:29, 30) Ninashukuru kwa moyo wote kwa yote ambayo Yehova amenifundisha.

“Haikuwa rahisi kwangu kufanya mabadiliko.”—DAVID HUDSON

UMRI: 72

NCHI: AUSTRALIA

HISTORIA: MLEVI

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Mimi ni mtoto wa 11 wa wazazi wangu, Willie na Lucy. Familia yetu iliishi katika kijiji cha Wenyeji wa Asili wa Australia kinachoitwa Aurukun, katika eneo la mbali upande wa kaskazini mwa Queensland. Kijiji cha Aurukun kiko karibu na bahari kando ya Mto Archer ambao ni maridadi sana. Wazazi wetu walitufundisha kuwinda na kuvua samaki ili kupata chakula. Wakati huo, sisi Wenyeji wa Asili wa Australia tulikuwa chini ya amri ya serikali iliyotukataza tusitumie pesa, na tulikuwa na sehemu maalum ya kuishi.

Wazazi wangu walijitahidi sana kunifunza sifa nzuri na wakatufunza sisi watoto kuwaheshimu watu walio wakubwa kwa umri na kuwagawia wengine katika jamii kile kidogo tulichokuwa nacho. Hivyo, tuliwaona watu wote wakubwa kwa umri kuwa baba na mama na mashangazi na wajomba.

Baba yangu alikufa nikiwa na umri wa miaka saba, kwa hiyo tukahamia misheni ya Wenyeji wa Asili wa Australia ya Mapoon, iliyo umbali wa kilomita 150 kusini ya Aurukun. Nilipokuwa na umri wa miaka 12, nilianza kujifunza kutumia farasi ili kuchunga mifugo. Nilipokaribia umri wa miaka 50 nilikuwa nimefanya kazi katika mashamba mengi ya kufuga ng’ombe nikiwa mchungaji. Maisha yalikuwa magumu. Nilikunywa pombe kupita kiasi mara kwa mara. Na jambo hilo lilinifanya niwe na maumivu mengi ya kichwa na matatizo mengi maishani.

Wakati fulani nilipokuwa nimelewa chakari, nilitoka nje ya hoteli na kuingia barabarani, na nikagongwa na gari lililokuwa likienda kwa kasi sana. Aksidenti hiyo ilinifanya nikae katika kituo cha kutibu viungo kwa miaka miwili. Huo ndio uliokuwa mwisho wa kazi yangu ya uchungaji.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Nilipokuwa katika kituo hicho cha kuwatibu walevi, mwanamke mmoja rafiki yangu aliniletea magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! ili niyasome. Sikuwa na elimu ya kutosha, hivyo sikuweza kusoma vizuri. Siku moja iliyokuwa na joto sana, mwanamume mwenye umri wa miaka 83 alinitembelea. Nilimkaribisha anywe maji baridi. Alinipa vitabu vinavyotegemea Biblia na akaniuliza kama ningependa arudi ili anieleze habari zilizomo ndani ya vitabu hivyo. Mwishowe, tulianza kujifunza Biblia kwa ukawaida. Nikatambua kwamba nilihitaji kubadili utu na maisha yangu kama ningetaka kumpendeza Mungu.

Haikuwa rahisi kufanya mabadiliko hayo. Lakini, kwa sababu ya mambo ambayo mama yangu alinifundisha, nilimheshimu huyu mzee aliyejifunza Biblia nami na ujuzi wa kiroho alionipa. Hata hivyo, nilisitasita kujiweka wakfu kwa Mungu. Nilihisi kuwa nilihitaji kujua kila kitu kilichoandikwa ndani ya Biblia.

Hatimaye, mfanyakazi mwenzangu alinisaidia kubadili mawazo yangu kuhusu jambo hilo. Alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, na akaniomba nisome maneno yenye kutia moyo ya Wakolosai 1:9, 10. Andiko hilo linasema kuwa tunahitaji kuendelea “kuongezeka katika ujuzi sahihi wa Mungu.” Huyo mfanyakazi mwenzangu alinisadia kuelewa kuwa nitajifunza mambo mapya kila siku, hivyo sikupaswa kuruhusu elimu kidogo ya kiroho niliyokuwa nayo inizuie nisijiweke wakfu kwa Yehova.

Nilivutiwa sana na Mashahidi wa Yehova nilipoanza kushirikiana nao. Nilijionea watu wa jamii mbalimbali wakimwabudu Mungu kwa umoja. Umoja huo ulinisadikisha kwamba nilikuwa nimeipata dini ya kweli, hivyo katika mwaka wa 1985, nilibatizwa na kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Nimeboresha ustadi wangu wa kusoma, na sasa ninatumia saa nyingi kila juma kuwafundisha watu kusoma na kuandika, na kuwasaidia kujifunza Biblia. Kwa kuongezea, yule mwanamke aliyeniletea magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, alijifunza na Mashahidi, akabatizwa, na sasa ni mke wangu mpendwa. Mimi na mke wangu tunapata furaha nyingi kwa kuwasaidia watu wengine wa jamii ya Wenyeji wa Asili wa Australia wajifunze kumhusu Yehova Mungu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Lililochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Blabu katika ukurasa wa 21]

Mimi na mke wangu tunapata furaha nyingi kwa kuwasaidia watu wengine wa jamii ya Wenyeji wa Asili wa Australia wajifunze kumhusu Mungu