Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

7 Je, Mungu Atasikiliza na Kujibu Sala Zetu?

7 Je, Mungu Atasikiliza na Kujibu Sala Zetu?

Sala

7 Je, Mungu Atasikiliza na Kujibu Sala Zetu?

SWALI hilo linafanya watu wasisimuke na kuwa na hamu ya kupata jibu. Biblia inaonyesha kwamba Yehova husikiliza sala leo. Iwe atasikiliza sala za mtu au hatazisikiliza, hilo hasa litategemea mtu mwenyewe.

Yesu aliwalaumu viongozi wa kidini wa nyakati zake ambao walisali kwa unafiki, wakihangaikia tu kuonekana kuwa waadilifu. Alisema kuwa watu hao wangepata “thawabu yao kwa ukamili,” akimaanisha kwamba wangepata tu kile walichotaka sana, yaani, kuonekana na watu, bali si kile walichohitaji, yaani, kusikilizwa na Mungu. (Mathayo 6:5) Vivyo hivyo leo, wengi husali kulingana na mapenzi yao bali si ya Mungu. Kwa kuwa wanapuuza kanuni za Biblia ambazo tumezungumzia, Mungu hasikilizi sala zao.

Namna gani wewe? Je, Mungu atasikiliza na kujibu sala zako? Jibu halitegemei wewe ni wa jamii, taifa, au cheo gani katika jamii. Biblia inatuhakikishia hivi: “Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.” (Matendo 10:34, 35) Je, wewe unafanya hivyo? Ikiwa unamwogopa Mungu, inamaanisha kwamba unamheshimu sana, na hutaki kumchukiza. Unapotenda uadilifu, unajitahidi kufanya yale ambayo Mungu anasema ni sawa badala ya kufanya mapenzi yako au ya wanadamu wenzako. Je, kweli unataka Mungu asikilize sala zako? Biblia inaonyesha jinsi unavyoweza kusali ili Mungu asikilize sala zako. a

Bila shaka, wengi wanataka Mungu ajibu sala zao kwa kufanya muujiza. Lakini hata katika nyakati za Biblia, si mara nyingi Mungu alijibu sala kwa kufanya miujiza. Baada ya muujiza mmoja kufanywa, miaka mingi ilipita kabla ya mwingine kufanywa. Zaidi ya hilo, Biblia inaonyesha kwamba kipindi cha kufanya miujiza kiliisha baada ya siku za mitume. (1 Wakorintho 13:8-10) Je, hilo linamaanisha kwamba leo Mungu hajibu sala? Hapana! Ona baadhi ya sala ambazo anajibu.

Mungu anatupa hekima. Yehova ndiye Chanzo pekee cha hekima yote ya kweli. Yeye huitoa kwa ukarimu, akiwapa wale wanaotaka mwongozo wake na wanaojitahidi kuishi kulingana na mwongozo huo.—Yakobo 1:5.

Mungu hutupa roho yake takatifu na faida zote zinazotokana nayo. Roho takatifu ni nguvu ya utendaji ya Mungu. Hakuna nguvu inayozidi hiyo. Inaweza kutusaidia kuvumilia majaribu. Inaweza kutupa amani tunapokabili hali ngumu. Inaweza kutusaidia kusitawisha sifa nyingine nzuri na zinazopendeza. (Wagalatia 5:22, 23) Yesu aliwahakikishia wafuasi wake kwamba Mungu hutoa zawadi hiyo kwa ukarimu.—Luka 11:13.

Mungu huwapa ujuzi wale wanaomtafuta kwa bidii. (Matendo 17:26, 27) Ulimwenguni pote, kuna watu ambao wanatafuta kweli kwa unyofu. Wanataka kujua kumhusu Mungu—jina lake ni nani, kusudi lake la kuumba dunia na wanadamu, na jinsi wanavyoweza kumkaribia. (Yakobo 4:8) Mara nyingi, Mashahidi wa Yehova wanakutana na watu kama hao, nao hufurahi kujibu maswali hayo kwa kutumia Biblia.

Je, hiyo ndiyo sababu ulichukua gazeti hili? Je, unamtafuta Mungu? Labda hii ndiyo njia anayotumia kujibu sala yako.

[Maelezo ya Chini]

a Kwa habari zaidi kuhusu jinsi ya kusali na kusikilizwa na Mungu, ona sura ya 17 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.