Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ufalme Ambao Utabadili Dunia Nzima

Ufalme Ambao Utabadili Dunia Nzima

Wafundishe Watoto Wako

Ufalme Ambao Utabadili Dunia Nzima

JE, UNAJUA ni Ufalme gani tunaozungumzia?— a Ni ule ambao Yesu alitufundisha tuombe uje. Alitufundisha tumwombe Mungu hivi: “Ufalme wako na uje.” (Mathayo 6:9, 10) Kwa karibu miaka 2,000, wafuasi wa Yesu wamekuwa wakimwomba Mungu kwamba Ufalme Wake uje. Je, umewahi kuomba ufalme huo uje?—

Ili kuelewa ufalme ni nini, unahitaji kujua mfalme ni nani. Mfalme ni mtu anayetawala. Na nchi anayotawala inaitwa miliki yake. Miliki ya Ufalme wa Mungu inatia ndani dunia nzima. Ufalme wa Mungu utakapokuja, kila mtu duniani atafurahia baraka ambazo utawala huo utawaletea wanadamu.

Ufalme wa Mungu ni serikali ya mbinguni. Katika andiko la Isaya 9:6, Biblia inamtaja Mtawala wa serikali hiyo. Ona vile linavyosema kumhusu: “Kuna mtoto ambaye amezaliwa kwetu, . . . na utawala wa ukuu utakuwa juu ya bega lake. Naye ataitwa jina . . . Mkuu wa Amani [au mwana-mfalme wa amani].”

Je, unajua mkuu, au mwana-mfalme, ni nani?— Ndiyo, ni mtoto wa kiume wa mfalme. Ni nani Mfalme mkuu zaidi mbinguni?— Jibu lako ni sahihi ukisema ni Yehova. Biblia inasema yeye ndiye ‘Aliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.’ (Zaburi 83:18) Katika Biblia, mara nyingi Yesu anaitwa “Mwana wa Mungu.” Sababu moja ya kuitwa hivyo ni kwamba Yehova ndiye aliyempa uhai. Yehova ndiye hasa Baba ya Yesu.—Luka 1:34, 35; Yohana 1:34, 49; 3:17; 11:27; 20:31; Matendo 9:20.

Ufalme wa Mungu, ambao Yesu alitufundisha tuombe uje, ni serikali ya kipekee sana. Ni “utawala wa ukuu” kwa sababu Yehova anamfanya Mwana wake Yesu kuwa Mtawala, au Mfalme, wa Ufalme huo. Lakini je, unajua kwamba watu wengine watachaguliwa kutawala wakiwa wafalme pamoja na Yesu katika Ufalme wa Baba yake?— Hebu tuzungumze kuhusu watu hao.

Muda mfupi kabla ya kufa, Yesu aliwaambia mitume wake waaminifu kwamba alikuwa anaenda katika “nyumba” ya Baba yake huko mbinguni. “Ninaenda kuwatayarishia ninyi mahali,” akasema, “ili mahali nilipo mimi, ninyi pia muwe hapo.” (Yohana 14:1-3) Je, unajua mitume na watu wengine ambao wamechaguliwa watafanya nini mbinguni pamoja na Yesu?— “Watatawala wakiwa wafalme pamoja naye.” Biblia hata inatuambia ni watu wangapi watakaotawala pamoja na Yesu. Watakuwa 144,000.—Ufunuo 14:1, 3; 20:6.

Unafikiri hali zitakuwa namna gani duniani wakati Mkuu wa Amani na wale 144,000 aliowachagua watakapotawala?— Hali zitakuwa nzuri wee! Hakutakuwa na vita. Kutakuwa na amani kati ya wanyama wenyewe na pia kati ya wanyama na wanadamu. Hakuna mtu atakayekuwa mgonjwa wala kufa. Macho ya wasioweza kuona yataona, masikio ya wasioweza kusikia yatasikia, mtu aliye kilema ataruka kama paa. Dunia itatokeza chakula kizuri kwa ajili ya kila mtu. Na watu wote watapendana kama vile Yesu alivyowafundisha wanafunzi wake wafanye. (Yohana 13:34, 35) Hebu tusome mistari iliyoorodheshwa hapa kutoka katika kitabu cha Isaya na tuone mambo mazuri ambayo yatatokea.—Isaya 2:4; 11:6-11; 25:8; 33:24; 35:5, 6; 65:21-24.

Tangu Yesu alipowafundisha watu waombe “ufalme wako na uje,” mamilioni ya watu wamejifunza kuhusu Ufalme huo. Ujuzi huo umebadili maisha yao. Hivi karibuni wakati Ufalme huo utakapokuja na kuondoa serikali zote duniani, kila mtu anayemtumikia Yehova Mungu na Mtawala wake aliyemchagua, Yesu Kristo, atakuwa na amani, afya nzuri, na furaha.—Yohana 17:3.

[Maelezo ya Chini]

a Kama unasoma sehemu hii pamoja na mtoto, unapoona kistari kama hiki (—), tua na umtie moyo mtoto atoe maoni yake.

MASWALI:

▪ Kwa nini Ufalme wa Mungu pia unaitwa “utawala wa ukuu”?

▪ Ni nani watakaotawala pamoja na Yesu katika Ufalme wa Baba yake?

▪ Hali zitakuwa namna gani duniani chini ya utawala wa Yesu?