Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kweli Watu wa Nyakati za Biblia Waliishi Kwa Muda Mrefu Sana?

Je, Kweli Watu wa Nyakati za Biblia Waliishi Kwa Muda Mrefu Sana?

Je, Kweli Watu wa Nyakati za Biblia Waliishi Kwa Muda Mrefu Sana?

JEANNE LOUISE CALMENT alikufa Agosti 4, 1997 (4/8/1997), katika mji wao, kusini-mashariki mwa Ufaransa. Alikuwa na umri wa miaka 122!

Leo, maendeleo katika sayansi, matibabu, na katika taaluma nyingine yanawasaidia watu leo kuishi miaka mingi. Hata hivyo, si watu wengi wanaoishi kwa miaka mia moja au zaidi. Labda hiyo ndio sababu nyakati nyingine umri wao mkubwa hutangazwa katika vyombo vya habari kama ilivyotokea katika kisa cha Bibi Calment.

Biblia inasema kwamba nyakati za kale watu waliishi miaka mingi sana, katika visa fulani karibu miaka elfu moja. Je, jambo hilo ni la kweli au linaaminika? Je, kweli watu wa nyakati za Biblia waliishi muda mrefu hivyo? Je, jambo hilo lina umaana wowote kwetu leo?

Watu Walioishi Muda Mrefu

Kitabu cha Mwanzo kinazungumza kuhusu wanaume saba walioishi zaidi ya miaka 900, wote wakiwa wamezaliwa kabla ya Gharika ya siku za Noa. Watu hao ni Adamu, Sethi, Enoshi, Kenani, Yaredi, Methusela, na Noa. (Mwanzo 5:5-27; 9:29) Huenda watu wengi wasiwafahamu wengi wa wanaume hao, lakini wote walikuwa miongoni mwa vizazi kumi vya kwanza katika historia ya mwanadamu. Methusela anajulikana kwa kuishi miaka mingi zaidi, yaani, miaka 969!

Biblia inataja watu wengine 25 ambao waliishi miaka mingi zaidi ya ile ambayo watu wanaishi leo. Baadhi yao waliishi miaka 300, 400, hata miaka 700 au zaidi. (Mwanzo 5:28-31; 11:10-25) Hata hivyo, kwa watu wengi masimulizi ya Biblia kuhusu watu walioishi miaka mingi hivyo ni hadithi tu zisizo za kweli. Je, ndivyo ilivyo?

Je, Ni Habari za Kweli au ni Hadithi za Uwongo?

Kulingana na ripoti iliyochapishwa na Taasisi ya Uchunguzi wa Idadi ya Watu ya Max Planck nchini Ujerumani, wataalamu walikadiria umri wa Bibi Calment, aliyetajwa mwanzoni, baada ya kukusanya “taarifa sahili na zinazoweza kuthibitishwa” ambazo Calment mwenyewe alitoa. Taarifa hizo zilihusu wakati matukio fulani yaliyomhusu yeye mwenyewe au watu wake wa ukoo, yalipotokea. Kisha, yale aliyosema yakalinganishwa na rekodi za umma, rekodi za mthibitishaji wa hati, rekodi za kanisa, na pia makala za magazeti ya habari na sensa za watu. Jambo la kufurahisha ni kwamba, hata ingawa haikuwa rahisi kuthibitisha kila jambo, uthibitisho wa moja kwa moja na usio wa moja kwa moja ulifanya iwezekane kuthibitisha muda ambao Calment aliishi.

Namna gani masimulizi ya Biblia? Je, yamethibitika kuwa ya kweli? Bila shaka! Ingawa si habari zote ambazo zimethibitishwa na vyanzo visivyo vya kidini, uthibitisho uliopo unaonyesha tena na tena kwamba yale yanayoelezwa katika Biblia ni ya kweli kihistoria, kisayansi, na yanalingana na mfuatano wa matukio. * Hilo halipaswi kutushangaza, kwa kuwa Biblia yenyewe inasema hivi: “Mungu anatambulikana kuwa msema kweli, na binadamu yeyote kuwa mwongo.” (Waroma 3:4, Verbum Bible) Kwa kuwa Biblia ni kitabu ‘kilichoongozwa na roho ya Mungu,’ hakina hadithi zozote za uwongo.—2 Timotheo 3:16.

Musa ambaye aliongozwa na Yehova Mungu kuandika vitabu vitano vya kwanza vya Biblia, anatajwa miongoni mwa watu wenye kuheshimiwa na wenye uvutano mkubwa zaidi katika historia. Wayahudi wanamwona kuwa mwalimu mkuu zaidi kati ya walimu wao wote. Waislamu wanamwona kuwa mmoja wa manabii wao wakuu zaidi. Na kwa Wakristo, Musa ni mtangulizi wa Yesu Kristo. Je, ni jambo linalopatana na akili kuamua kwamba maandishi ya mtu muhimu kama huyo katika historia si ya kuaminika?

Je, Wakati Ulipimwa kwa Njia Tofauti?

Wengine wamedai kwamba wakati ulipimwa kwa njia tofauti nyakati hizo na kwamba ule uliokuwa ukiitwa mwaka kwa kweli ulikuwa mwezi mmoja. Hata hivyo, uchunguzi wa masimulizi ya kitabu cha Mwanzo, unaonyesha waziwazi kwamba watu wa nyakati zile walipima wakati kama tu tunavyofanya leo. Fikiria mifano miwili. Katika simulizi la Gharika, tunasoma kwamba Gharika hiyo ilianza wakati Noa alipokuwa na miaka 600, katika “mwezi wa pili, siku ya kumi na saba ya mwezi.” Kisha linaendelea kusema kwamba maji yaliifunika dunia kwa siku 150 na kwamba “katika mwezi wa saba, siku ya kumi na saba ya mwezi, safina i[li]tua kwenye milima ya Ararati.” (Mwanzo 7:11, 24; 8:4) Kwa hiyo, kipindi hicho cha miezi mitano—kuanzia siku ya 17 ya mwezi wa pili mpaka siku ya 17 ya mwezi wa saba mwaka huo—ni siku 150. Bila shaka, dai la kwamba mwaka mmoja ulikuwa ni mwezi mmoja kwa kweli halina msingi.

Fikiria mfano wa pili. Kulingana na Mwanzo 5:15-18, Mahalaleli alimzaa mwana wake akiwa na umri wa miaka 65, na akaendelea kuishi kwa miaka 830, na kufa akiwa na umri wa miaka 895. Pia Enoko mjukuu wake alimzaa mwana akiwa na umri wa miaka 65. (Mwanzo 5:21) Ikiwa kwa kweli mwaka ulikuwa sawa na mwezi mmoja, basi wanaume hao wawili walizaa wakiwa na miaka mitano tu. Je, hilo linalopatana na akili?

Elimu ya vitu vya kale pia inatusaidia kuelewa vizuri jambo hilo, kwani inakubaliana na Biblia kwamba kuna watu walioishi miaka mingi. Kuhusu mzee wa ukoo Abrahamu, Biblia inasema kwamba alitoka katika jiji la Uru, na baadaye akaishi katika jiji la Harani na kisha katika eneo la Kanaani. Pia inasema kuwa alipigana na Kedorlaoma mfalme wa Elamu na kumshinda. (Mwanzo 11:31; 12:5; 14:13-17) Uvumbuzi unathibitisha kwamba kulikuwa na watu kama hao na maeneo kama hayo. Elimu ya vitu vya kale pia imetusaidia kuelewa jiografia ya maeneo hayo na utamaduni wa watu wanaotajwa kuhusiana na Abrahamu. Kwa kuwa yale ambayo Biblia inasema kumhusu Abrahamu ni sahihi, kwa nini kuwe na shaka kuhusu umri wake wa miaka 175?—Mwanzo 25:7.

Hivyo, hakuna sababu ya kutilia shaka yale ambayo Biblia inasema kuhusu muda mrefu isivyo kawaida ambao watu fulani katika nyakati za kale waliishi. Lakini huenda ukajiuliza, ‘Iwe watu hao waliishi miaka mingi au hawakuishi, hilo lina umuhimu gani kwangu?’

Unaweza Kuishi Muda Mrefu Zaidi Kuliko Unavyofikiri!

Miaka mingi ambayo watu wa kabla ya Gharika waliishi inathibitisha kwamba mwili wa mwanadamu una uwezo wa ajabu wa kuishi muda marefu sana. Teknolojia ya kisasa imewawezesha wanasayansi kuchunguza vizuri mwili wa mwanadamu na jinsi ulivyobuniwa kwa njia ya ajabu, kutia ndani uwezo wake wa ajabu wa kujifanyiza upya na kujiponya wenyewe. Wamefikia uamuzi gani? Mwili wa mwanadamu unaweza kuishi milele. Profesa wa Kitiba Tom Kirkwood, anasema, “[Kuzeeka] ni moja kati ya mambo magumu yasiyoweza kufafanuliwa katika sayansi ya kitiba.”

Hata hivyo, Yehova Mungu haoni uzee kuwa jambo gumu au tatizo ambalo haliwezi kusuluhishwa. Alimuumba mtu wa kwanza, Adamu, akiwa mkamilifu na alikusudia kwamba wanadamu waishi milele. Jambo la kusikitisha ni kwamba Adamu aliamua kumpa Mungu kisogo. Matokeo yake ni kwamba Adamu alianguka katika dhambi na kupoteza ukamilifu. Huu ndio ufafanuzi ambao wanasayansi wamekuwa wakiutafuta: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” (Waroma 5:12) Tunakuwa wagonjwa, tunazeeka, na kisha tunakufa kwa sababu ya dhambi na kutokamilika.

Hata hivyo, kusudi la Muumba wetu mwenye upendo halijabadilika. Ili athibitishe jambo hilo, aliandaa fidia au dhabihu ya ukombozi ya Mwana wake, Yesu Kristo, ambayo inafanya iwezekane kwa wanadamu kuwa wakamilifu na waishi milele. Biblia inasema hivi: “Kama vile katika Adamu wote wanakufa, vivyo hivyo pia katika Kristo wote watafanywa kuwa hai.” (1 Wakorintho 15:22) Watu walioishi kabla ya Gharika walikuwa karibu zaidi na ukamilifu kuliko sisi, na ndio sababu waliishi miaka mingi zaidi kuliko tunavyoishi sasa. Hata hivyo, leo tuko karibu na wakati ambapo ahadi za Mungu zitatimia. Hivi karibuni hali ya kutokamilika na dhambi zote zitaondolewa, na watu hawatadhoofika wala kufa.—Isaya 33:24; Tito 1:2.

Unaweza kupata baraka hizo jinsi gani? Usifikiri kwamba ahadi ya Mungu ni ndoto tu. Yesu alisema: “Yule ambaye husikia neno langu na kumwamini yule aliyenituma ana uzima wa milele.” (Yohana 5:24) Hivyo, jifunze Biblia na kuishi kupatana na yale unayojifunza. Ikifanya hivyo, utakuwa ukifuata mfano wa wale ambao mtume Paulo alisema kuwa ‘wanajiwekea wenyewe kwa usalama hazina ya msingi mzuri kwa ajili ya wakati ujao, ili waushike imara uzima ulio wa kweli.’ (1 Timotheo 6:19) Unaweza kuwa na hakika kwamba Mungu aliyewawezesha watu wanaotajwa katika Biblia waishi miaka mingi, anaweza kukufanya wewe uishi milele!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Kwa habari zaidi, ona kitabu Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Grafu katika ukurasa wa 12]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

1000*

969* METHUSELA

950* NOA

930* ADAMU

900*

800*

700*

600*

500*

400*

300*

200*

100* MWANADAMU WA SIKU HIZI

*UMRI