Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Walimkataa Masihi?

Kwa Nini Walimkataa Masihi?

Kwa Nini Walimkataa Masihi?

YESU alipokuwa duniani, watu walivutiwa sana na mambo aliyofundisha na kushangazwa na miujiza aliyofanya. Kwa sababu hiyo, wengi “walimwamini” na kumkubali kuwa ndiye Masihi aliyetabiriwa, au Kristo. Waliuliza: “Kristo atakapofika, je, atafanya ishara zaidi ya zile ambazo mtu huyu amefanya?”—Yohana 7:31.

Ingawa kulikuwa na uthibitisho mwingi ulioonyesha kwamba Yesu ndiye Masihi, wengi wa wale waliomwona na kumsikia hawakumwamini. Kwa kusikitisha, hata wale ambao mwanzoni walimwamini walimwacha baadaye. Kwa nini watu wengi walimkataa Yesu kuwa ndiye Masihi ingawa kulikuwa na uthibitisho mwingi? Acheni tuchunguze sababu, na kadiri tunavyoendelea kufanya hivyo, jiulize, ‘Je, ninaweza kufanya kosa hilohilo leo?

Matazamio Ambayo Hayakutimizwa

Yesu alipozaliwa, Wayahudi wengi walikuwa wakitazamia kutokea kwa Masihi. Wakati alipopelekwa hekaluni akiwa mtoto mchanga, alikutana na wale “waliokuwa wakiungojea ukombozi wa Yerusalemu” kupitia Masihi aliyeahidiwa. (Luka 2:38) Baadaye, wengi walioshuhudia mambo ambayo Yohana Mbatizaji alifanya walijiuliza: “Je, labda yeye ndiye Kristo?” (Luka 3:15) Hata hivyo, Wayahudi wa karne ya kwanza walitazamia Masihi afanye nini?

Wayahudi wengi siku hizo waliamini kwamba Masihi angekuja na kuwakomboa kutoka katika ukandamizaji wa Waroma na kuurudisha ufalme wa Israeli hapa duniani. Kabla ya Yesu kuanza huduma yake, viongozi wengi wenye ushawishi walitokea na kuchochea upinzani mkubwa juu ya mamlaka ya kisiasa iliyokuwa ikitawala. Yaelekea mambo ambayo viongozi hao walifanya yaliongoza matazamio ya watu kuelekea Masihi.

Kinyume cha hilo, Yesu alikuwa tofauti kabisa na jinsi walivyotazamia. Hakuunga mkono matendo ya jeuri, bali aliwafundisha wasikilizaji wake wawapende adui zao na wajitiishe kwa wenye mamlaka. (Mathayo 5:41-44) Alikataa jitihada za watu za kumfanya mfalme. Badala yake, alifundisha kwamba ufalme wake ungekuwa “si sehemu ya ulimwengu huu.” (Yohana 6:15; 18:36) Hata hivyo, maoni yaliyokuwapo kumhusu Masihi yalikuwa na uvutano mkubwa juu ya watu.

Yohana Mbatizaji aliona na kusikia kuhusu miujiza iliyothibitisha kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu. Hata hivyo, Yohana alipotiwa gerezani, aliwatuma wanafunzi wake wakamuulize Yesu: “Je, wewe ndiye Yule Anayekuja, au tumtarajie mwingine?” (Mathayo 11:3) Huenda Yohana alijiuliza ikiwa kwa kweli Yesu ndiye Mkombozi, ambaye angetimiza matazamio ya Wayahudi.

Ilikuwa vigumu kwa mitume wa Yesu kuamini kwamba atauawa na kisha kufufuliwa. Pindi moja Yesu alipoeleza kwamba itakuwa ni lazima Masihi ateseke na kisha kufa, Petro “a[li]mchukua kando na kuanza kumkemea.” (Marko 8:31, 32) Bado Petro hakuelewa jinsi kifo cha Yesu kilivyohusiana na daraka lake akiwa Masihi.

Alipoingia Yerusalemu muda mfupi kabla ya Pasaka ya mwaka wa 33 W.K., Yesu alikaribishwa na umati wenye shangwe uliokuwa ukimsifu kuwa ni Mfalme. (Yohana 12:12, 13) Jinsi mambo yalivyobadilika haraka! Katika muda wa juma moja, Yesu alikamatwa na kuuawa. Baada ya kifo cha Yesu, wanafunzi wake wawili waliomboleza: “Sisi tulikuwa tukitumaini kwamba mtu huyu ndiye angekomboa Israeli.” (Luka 24:21) Hata Yesu aliyefufuliwa alipowatokea wanafunzi wake, bado walikuwa wanawaza kwamba Masihi angeanzisha ufalme wa kidunia. Walimuuliza: “Bwana, je, unarudishia Israeli ufalme wakati huu?” Kwa wazi, matazamio yenye makosa kuhusu Masihi yalikuwa yametia mizizi katika mioyo na akili za wasikilizaji wa Yesu.—Matendo 1:6.

Baada ya Yesu kupaa mbinguni na roho takatifu kumwagwa, wanafunzi wake walikuja kuelewa vizuri kwamba Masihi angetawala akiwa Mfalme mbinguni. (Matendo 2:1-4, 32-36) Mtume Petro na Yohana walihubiri kwa ujasiri kuhusu kufufuliwa kwa Yesu na kwa kufanya miujiza, wakathibitisha kuwa waliungwa mkono na Mungu. (Matendo 3:1-9, 13-15) Maelfu ya watu huko Yerusalemu waliitikia na kuwa waamini. Hata hivyo, Wayahudi wenye mamlaka hawakufurahia jambo hilo. Kama walivyompinga Yesu, sasa walianza kuwapinga wanafunzi na mitume wake. Kwa nini viongozi wa dini ya Kiyahudi walimkataa Yesu?

Akataliwa na Viongozi wa Kidini

Kufikia wakati Yesu alipokuja duniani, kufikiri na kutenda kwa wafuasi wa dini ya Kiyahudi kulikuwa tofauti sana na yale ambayo Maandiko yaliyoongozwa na roho ya Mungu yanafundisha. Viongozi wa kidini wa wakati huo—Masadukayo, Mafarisayo, na waandishi—walikuwa wakishikilia mapokeo ya wanadamu, wakiyatanguliza badala ya kutanguliza Neno la Mungu. Mara kwa mara, walimshutumu Yesu kwa kuvunja Sheria kwa sababu alifanya miujiza na kuponya siku ya Sabato. Kwa kuonyesha waziwazi kwamba mafundisho yao hayakuwa ya kimaandiko, Yesu alipinga mamlaka na madai yao kwamba walikuwa na msimamo mzuri mbele za Mungu. Tofauti nao, Yesu alizaliwa katika familia maskini na hakuwa na elimu ya kidini kama wao. Si ajabu kwamba ilikuwa vigumu sana kwa viongozi hao wenye kiburi kumtambua Yesu kuwa ndiye Masihi! Makabiliano hayo yaliwakasirisha sana hivi kwamba ‘walifanya shauri juu ya Yesu ili wapate kumwangamiza.’—Mathayo 12:1-8, 14; 15:1-9.

Viongozi hao wa kidini wangeweza kueleza jinsi gani uwezo wa Yesu wa kufanya miujiza? Hawakupinga kwamba miujiza hiyo ilifanyika. Badala yake, kwa kukufuru walijaribu kuwafanya watu wasimwamini Yesu wakidai kwamba anapata nguvu kutoka kwa Shetani na kusema hivi: “Mtu huyu hatoi roho waovu ila kwa nguvu za Beelzebuli, mtawala wa roho waovu.”—Mathayo 12:24.

Kulikuwa na sababu nyingine iliyowafanya wasimtambue Yesu kuwa Masihi. Baada ya Yesu kumfufua Lazaro, viongozi wa madhehebu mbalimbali walishauriana na kusema: “Tufanye nini, kwa sababu mtu huyu anafanya ishara nyingi? Tukimwacha hivyo, hao wote watamwamini, na Waroma watakuja na kuondolea mbali mahali petu na taifa letu pia.” Kwa kuwa waliogopa kupoteza mamlaka na vyeo vyao, viongozi hao walipanga njama ya kumuua Yesu na Lazaro!—Yohana 11:45-53; 12:9-11.

Wabaguliwa na Kuteswa na Jamii

Mtazamo wa viongozi wa dini ya Kiyahudi ulifanya watu wamchukie mtu yeyote aliyekubali kuwa Yesu ni Masihi. Kwa kujivunia vyeo vyao, walimdharau mtu yeyote aliyemwamini Yesu, wakisema: “Je, kuna hata mmoja wa watawala au wa Mafarisayo ambaye amemwamini?” (Yohana 7:13, 48) Baadhi ya viongozi wa Kiyahudi, kama vile Nikodemo na Yosefu wa Arimathea, walikuwa wanafunzi wa Yesu, lakini kwa sababu ya hofu walificha jambo hilo. (Yohana 3:1, 2; 12:42; 19:38, 39) Viongozi wa kidini walikuwa wameazimia kwamba “ikiwa yeyote angemkiri [Yesu] kuwa ndiye Kristo, angefukuzwa katika sinagogi.” (Yohana 9:22) Mtu kama huyo, angeepukwa na kudhihakiwa na jamii.

Upinzani kuelekea mitume na wanafunzi wa Yesu mwishowe ulichochea mateso makali. Kwa sababu ya kuhubiri kwao kwa ujasiri, mitume waliteswa na Sanhedrini, mahakama kuu ya Wayahudi. (Matendo 5:40) Wapinzani walitunga mashtaka ya uwongo dhidi ya mwanafunzi Stefano. Alihukumiwa na Sanhedrini na kupigwa mawe hadi kufa. Kisha, “mateso makubwa yakatokea juu ya kutaniko lililokuwa katika Yerusalemu; wote isipokuwa mitume walitawanywa kotekote katika maeneo ya Yudea na Samaria.” (Matendo 6:8-14; 7:54–8:1) Sauli ambaye baadaye alikuja kuwa mtume Paulo, alishiriki katika kampeni hiyo ya kulitesa kutaniko ambayo iliungwa mkono na kuhani mkuu na “kusanyiko lote la wanaume wazee.”—Matendo 9:1, 2; 22:4, 5.

Hata katika hali ngumu kama hizo, Ukristo ulikua haraka baada ya kifo cha Yesu. Ingawa maelfu ya watu walikuja kuwa waamini, Wakristo waliendelea kuwa jamii ya watu wachache huko Palestina katika karne ya kwanza. Ikiwa mtu angejitambulisha waziwazi kuwa mfuasi wa Kristo, angetengwa na wengine na hata kutendwa vibaya.

Jifunze Kutoka kwa Wale Waliomkataa Yesu

Kama tulivyoona, maoni yasiyofaa, uvutano wa kijamii, na mateso yaliwazuia wengi katika karne ya kwanza wasimwamini Yesu. Leo, maoni yenye makosa kuhusu Yesu na mafundisho yake yanaweza kuwa na matokeo hayohayo. Kwa mfano, wengi wamefundishwa kwamba Ufalme wa Mungu upo moyoni mwao au utakuja kupitia jitihada za wanadamu. Wengine wameshawishiwa kutegemea sayansi au teknolojia ili itatue matatizo ya wanadamu na hivyo kusiwe na umuhimu wa kumwamini Masihi. Wachambuzi wengi wa siku hizi wanadai kwamba matukio katika huduma ya Yesu yaliyorekodiwa kwenye Biblia si ya kweli kihistoria, kwa hiyo, wanadhoofisha imani ya watu katika Yesu akiwa Masihi.

Maoni na mawazo kama hayo yanafanya wengi ama wachanganyikiwe kuhusu jukumu la Masihi au wasione umuhimu wa kuchunguza jambo hilo. Hata hivyo, kwa wale wanaotaka kuchunguza habari kumhusu Masihi, leo kuna uthibitisho mwingi unaoonyesha kuwa Yesu ndiye Masihi kuliko ilivyokuwa katika karne ya kwanza. Tuna Maandiko ya Kiebrania yenye unabii mwingi kuhusu yale ambayo Masihi angefanya na rekodi katika zile Injili nne kuhusu yale ambayo Yesu alifanya katika kutimiza unabii huo. *

Kwa kweli tuna uthibitisho wa kutosha unaoweza kutusaidia kufanya uamuzi unaofaa kuhusu jambo hilo. Na tunapaswa kuufanya haraka. Kwa nini? Kwa sababu Biblia inafunua kwamba akiwa Mfalme wa Kimasihi katika Ufalme wa Mungu, hivi karibuni Yesu atachukua hatua ya kuwaondoa wale wote wanaoiharibu dunia na kuleta utawala mwadilifu ambao utawawezesha raia watiifu kuishi milele duniani katika mazingira ya kiparadiso. (Danieli 2:44; Ufunuo 11:15, 18; 21:3-5) Unaweza kufurahia tazamio hilo zuri ukijitahidi kujifunza na kumwamini Yesu sasa. Zingatia maneno haya ya Yesu mwenyewe: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.”—Yohana 3:16.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 22 Ona chati “Unabii Kumhusu Masihi” katika ukurasa wa 200 wa kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Blabu katika ukurasa wa 20]

Je, ungemtambua Masihi ikiwa ungeishi katika siku za Yesu?

[Picha katika ukurasa wa 21]

Usiruhusu maoni uliyo nayo yakuzuie usijifunze ukweli kumhusu Yesu