Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maono Kuhusu Makao ya Roho

Maono Kuhusu Makao ya Roho

Maono Kuhusu Makao ya Roho

HATA utazame anga muda mrefu kiasi gani, hutamwona kiumbe yeyote wa roho. Sikiliza, na hutamsikia hata mmoja. Hata hivyo, huenda ikawa unaamini kuwa viumbe hao wapo. Viumbe wa roho wana nguvu na akili nyingi sana, na wana majina ya kibinafsi na sifa mbalimbali. Baadhi yao wangependa kutusaidia na wengine kutuumiza. Wote wanatukazia fikira.

Mungu wa kweli mwenyewe ni Roho. (Yohana 4:24) Ana jina la kipekee linalomtofautisha na miungu mingine mingi ya uwongo. Jina lake ni Yehova. (Zaburi 83:18) Mtunga-zaburi aliandika: “Yehova ni mkuu na wa kusifiwa sana. Ni mwenye kuogopesha kuliko miungu mingine yote. Kwa maana miungu yote ya vikundi vya watu ni miungu isiyo na thamani; lakini Yehova, amezifanya mbingu. Utukufu na fahari ziko mbele zake; nguvu na uzuri zipo katika patakatifu pake.”—Zaburi 96:4-6.

Maono Kumhusu Mungu wa Kweli

Biblia inatuambia hivi: “Hakuna mwanadamu ambaye amemwona Mungu wakati wowote.” (Yohana 1:18) Hatuna uwezo wa kufahamu jinsi anavyoonekana na jinsi utukufu wake ulivyo, sawa na vile mtu aliyezaliwa kipofu asivyoweza kufahamu rangi tofauti-tofauti. Hata hivyo, kama vile ambavyo mwalimu mzuri huwaeleza wanafunzi mambo magumu kwa kutumia maneno wanayoweza kuelewa, ndivyo ambavyo Mungu kupitia Neno lake, Biblia, hutueleza mambo tusiyoweza kuona kwa kutumia mambo tunayoweza kuona. Kupitia maono aliyowapa watumishi wake waaminifu wa zamani, Yehova hutusaidia kupiga picha akilini ya jinsi mbingu zilivyo na kuelewa uhusiano wetu pamoja na wale wanaokaa huko.

Kwa mfano, katika mojawapo ya maono aliyoonyeshwa nabii Ezekieli, utukufu wa Yehova ulihusianishwa na moto, mwangaza, jiwe la yakuti, na upinde. Katika maono mengine, mtume Yohana anamwona Yehova kwenye kiti cha enzi na kusema kuwa “kuonekana kwake ni kama jiwe la yaspi na jiwe jekundu la thamani,” akiongezea kwamba “upinde wa mvua ambao kuonekana kwake ni kama zumaridi unakizunguka kile kiti cha ufalme.” Maelezo hayo yanaonyesha kuwa mwonekano wa Yehova ni wa kipekee, wenye kuvutia sana, na mwangavu.—Ufunuo 4:2, 3; Ezekieli 1:26-28.

Nabii Danieli pia alipata maono kumhusu Yehova. Aliona malaika “elfu kumi mara elfu kumi walioendelea kusimama mbele za [Yehova].” (Danieli 7:10) Lazima alishangaa sana! Kumwona malaika mmoja tu, hata katika maono, ni jambo lenye kustaajabisha sana, hivyo, jaribu kuwazia kuona makumi ya maelfu ya malaika wakamilifu!

Malaika wanatajwa mara 400 hivi katika Biblia, na wanatia ndani maserafi na makerubi. Neno la Kigiriki na la Kiebrania linalotafsiriwa “malaika” katika Biblia linamaanisha “mjumbe.” Kwa hiyo, malaika wanaweza kuwasiliana kati yao, na zamani waliwasiliana na wanadamu. Malaika si wanadamu ambao wakati fulani waliishi duniani. Yehova aliwaumba viumbe hao wa roho muda mrefu kabla ya kumuumba mwanadamu.—Ayubu 38:4-7.

Katika maono ya Danieli, makumi ya maelfu ya malaika walikuwa wamekusanyika kushuhudia tukio fulani la kipekee. Kisha Danieli akaona “mtu fulani kama mwana wa binadamu” akikaribia kiti cha enzi cha Yehova kwa ajili ya “kupewa utawala na heshima na ufalme, ili vikundi vyote vya watu, vya mataifa na lugha vimtumikie yeye.” (Danieli 7:13, 14) “Mwana wa binadamu” ambaye ni Yesu Kristo aliyefufuliwa ana jukumu muhimu mbinguni, naye amepewa utawala wa dunia yote. Hivi karibuni, utawala wake utachukua mahali pa serikali za kibinadamu na kuondoa magonjwa, huzuni, uonevu, umaskini, na hata kifo.—Danieli 2:44.

Bila shaka, malaika wengi waaminifu, wanaopenda kuwasaidia wanadamu, walishangilia sana Yesu alipotawazwa kuwa mfalme. Lakini, inasikitisha kwamba si viumbe wote wa roho walioshangilia.

Maadui wa Mungu na Mwanadamu

Mwanzoni mwa historia ya mwanadamu, mmoja wa malaika alichochewa na tamaa ya kutaka kuabudiwa na akamwasi Yehova, na hivyo akajifanya mwenyewe kuwa Shetani, jina linalomaanisha “Mpinzani.” Shetani ndiye kiumbe mwovu zaidi ulimwenguni naye anampinga vikali Yehova, Mungu ambaye ana upendo mwingi sana. Malaika wengine walijiunga na Shetani katika uasi wake na Biblia inawaita mashetani. Kama Shetani, mashetani wamekuwa maadui wakatili wa wanadamu. Uvutano wao umechangia pakubwa kuwepo kwa ukosefu wa haki, magonjwa, umaskini, na vita vingi duniani.

Ingawa siku hizi, dini nyingi hazizungumzi sana kumhusu Shetani, kitabu cha Biblia cha Ayubu kinaeleza kwa undani kuhusu tabia na nia ya malaika huyu mwasi. Kinasema: “Na ikaja siku ambapo wana wa Mungu wa kweli waliingia na kusimama mbele za Yehova, na hata Shetani akaingia katikati yao.” Katika mazungumzo yaliyofuata, Shetani alidai kwa dharau kwamba Ayubu alimtumikia Mungu tu kwa sababu ya mambo ambayo Mungu alimfanyia. Ili kuthibitisha dai lake, Shetani alimletea Ayubu mateso mengi na kuua mifugo wake na watoto wake wote kumi. Kisha, akamshambulia Ayubu kwa majipu mabaya kwenye mwili wake wote. Mashambulio yote ya Shetani hayakuthibitisha dai lake.—Ayubu 1:6-19; 2:7.

Kuna sababu nzuri ambazo zimemfanya Yehova amvumilie Shetani kwa muda mrefu, lakini hatafanya hivyo milele. Hivi karibuni, Ibilisi ataondolewa. Hatua za kwanza za kumwondoa Shetani tayari zimechukuliwa na zinaelezwa katika kitabu cha Ufunuo, ambacho kinafunua tukio lingine muhimu katika makao ya roho ambalo hatungeweza kuliona kamwe. Tunasoma: “Vita vikatokea ghafula mbinguni: Mikaeli [Yesu Kristo aliyefufuliwa] na malaika zake wakapigana na yule joka mkubwa [Shetani], naye joka mkubwa na malaika zake wakapigana lakini hakushinda, wala mahali hapakupatikana mbinguni kwa ajili yao tena. Kwa hiyo yule joka mkubwa akatupwa chini, yule nyoka wa zamani, yeye anayeitwa Ibilisi na Shetani, anayeipotosha dunia nzima inayokaliwa; akatupwa chini duniani, na malaika zake wakatupwa chini pamoja naye.”—Ufunuo 12:7-9.

Ona kwamba Shetani ‘anaipotosha dunia nzima inayokaliwa.’ Anawapotosha watu wamwache Yehova na Neno lake, kwa kuendeleza mafundisho ya kidini ya uwongo. Fundisho moja la uwongo ni kwamba kila mtu huenda katika makao ya roho baada ya kufa. Kuna maoni tofauti-tofauti kuhusu fundisho hilo. Kwa mfano, barani Afrika na Asia, watu wengi wanaamini kwamba watu wanapokufa wanaenda katika makao ya roho ambako mababu zao wanaishi. Mafundisho kuhusu toharani na moto wa mateso pia yanategemea wazo la kwamba mtu huendelea kuishi baada ya kufa.

Je, Watu Wanaenda Mbinguni Baada ya Kufa?

Namna gani kuhusu imani ya mamilioni ya watu ulimwenguni kwamba watu wote wema wanaenda mbinguni? Ni kweli kwamba watu fulani wema wanaenda mbinguni, lakini hesabu yao ni ndogo ikilinganishwa na mabilioni ya watu ambao wamekufa. Biblia inaonyesha kuwa watu 144,000 “wamenunuliwa kutoka duniani” na watatumika wakiwa “makuhani” na “wafalme juu ya dunia.” (Ufunuo 5:9, 10; 14:1, 3) Wao pamoja na Mwana wa binadamu, Yesu Kristo, watafanyiza serikali ya mbinguni, yaani, Ufalme wa Mungu. Serikali hiyo itamwondoa Shetani na mashetani wake na kuifanya dunia kuwa paradiso. Watu wengi waliokufa watafufuliwa wakiwa na tazamio la kuishi milele katika Paradiso hiyo ya kidunia.—Luka 23:43.

Hivyo basi, wale wanaokaa katika makao ya roho ni wengi sana. Aliye mkuu zaidi kati yao ni Yehova Mungu, Muumba wa vitu vyote vilivyo hai. Makumi ya maelfu ya malaika wanamtumikia kwa uaminifu. Malaika wengine waliongozwa na Shetani kumwasi Yehova, wanajitahidi kuwapotosha wanadamu. Kwa kuongozea, hesabu ndogo ya wanadamu “wamenunuliwa,” au kuchaguliwa, kutoka duniani ili kushughulikia majukumu ya pekee huko mbinguni. Tukiwa na hayo akilini, acheni sasa tuone ni nani tunayeweza kuwasiliana naye katika makao ya roho, na jinsi tunavyopaswa kufanya hivyo.