Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kweli Mungu Anakujali?

Je, Kweli Mungu Anakujali?

Je, Kweli Mungu Anakujali?

JE, UNAHISI kwamba unapendwa? Au nyakati nyingine unahisi kuwa hakuna mtu anayekujali? Katika ulimwengu huu wenye ubinafsi na shughuli nyingi, inaweza kuwa rahisi kufikiri kwamba huna thamani na kwamba hakuna mtu anayekujali. Kulingana na ufafanuzi wa Biblia kuhusu nyakati zetu, watu wengi leo wanajipenda sana hivi kwamba mtazamo wa kutowajali wengine umeenea sana.—2 Timotheo 3:1, 2.

Licha ya umri, utamaduni, lugha, au jamii, wanadamu wote wanahitaji kupenda na kupendwa. Kulingana na ripoti fulani, mfumo wetu wa neva umebuniwa hasa ili uhisi upendo na wororo. Yehova Mungu, ambaye alituumba, anajua vizuri kuliko mtu mwingine yeyote uhitaji wetu wa kupendwa na kuthaminiwa. Ungejihisi jinsi gani kama angekuhakikishia kuwa una thamani kwake? Bila shaka, hilo lingekuwa hakikisho bora sana ambalo unaweza kupata. Je, kweli tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova anapendezwa na wanadamu wasio wakamilifu? Je, anatujali sisi tukiwa mtu mmojammoja? Ikiwa ndivyo, ni nini kinachofanya apendezwe na mtu?

Yehova Anajali

Miaka 3,000 hivi iliyopita, mtunga-zaburi mwenye kumhofu Mungu alistaajabu sana alipoona fahari kuu ya mbingu wakati wa usiku. Hakuwa na shaka katika akili yake kuhusu ukuu wa Yeye aliyeziumba nyota zisizo na hesabu. Alipotafakari ukuu wa Yehova na uduni wa mwanadamu, mtunga-zaburi alieleza kuwa alishangazwa na jinsi Yehova anavyowapenda na kuwajali watu: “Ninapoziona mbingu zako, kazi za vidole vyako, mwezi na nyota ambazo umetayarisha, mwanadamu anayeweza kufa ni nini hivi kwamba umweke akilini, na mwana wa mtu wa udongo hivi kwamba umtunze?” (Zaburi 8:3, 4) Ni rahisi kusema kwamba Aliye Mkuu Zaidi yuko mbali sana au ana shughuli nyingi sana hivi kwamba hawezi kumfikiria mwanadamu ambaye si mkamilifu. Hata hivyo, mtunga-zaburi alijua kwamba ingawa sisi ni viumbe duni na uhai wetu ni mfupi, sisi tuna thamani kwa Mungu.

Mtunga-zaburi mwingine alituhakikishia hivi: “Yehova anawafurahia wale wanaomwogopa, wale wanaozingojea fadhili zake zenye upendo.” (Zaburi 147:11) Wazo linalotajwa katika zaburi hizo mbili linagusa moyo sana. Hata ingawa Yehova ni mkuu sana, hatosheki tu na kujua kwamba wanadamu wapo. Badala yake, ‘anawajali’ na ‘kuwafurahia.’

Uhakika huo unakaziwa zaidi na unabii wa Biblia ambao unafafanua mambo ambayo yanatukia wakati wetu. Kupitia nabii Hagai, Yehova alionyesha kuwa habari njema za Ufalme wa Mungu zingehubiriwa ulimwenguni pote. Kukiwa na matokeo gani? Ona mojawapo ya matokeo hayo: “Vitu vyenye kutamanika vya mataifa yote vitaingia; nami nitaijaza nyumba hii utukufu.”—Hagai 2:7.

Ni vitu gani hivyo “vyenye kutamanika” ambavyo vinakusanywa kutoka katika mataifa yote? Vitu hivyo haviwezi kuwa utajiri. (Hagai 2:8) Kinachofanya moyo wa Yehova ushangilie si fedha wala dhahabu. Yeye anapendezwa na watu ambao ingawa si wakamilifu, wanamwabudu kwa sababu ya upendo. (Methali 27:11) Hao ndio “vitu vyenye kutamanika” vinavyomletea utukufu, na anathamini ujitoaji wao wa nafsi yote na utumishi wenye bidii. Je, wewe ni mmoja wao?

Huenda ikaonekana kuwa vigumu kuamini kwamba Muumba Mkuu wa ulimwengu wote anaweza kuwapenda viumbe wasio wakamilifu. Hata hivyo, ukweli huo unapaswa kutuchochea kukubali mwaliko wenye upendo wa kumkaribia.—Isaya 55:6; Yakobo 4:8.

“Wewe Ni Mtu Mwenye Kutamanika Sana”

Katika umri wake wa uzee, nabii Danieli alishuhudia jambo fulani lisilo la kawaida jioni moja. Alipokuwa akisali, ghafla alitembelewa na mgeni wa heshima. Jina lake ni Gabrieli. Danieli alikuwa amewahi kukutana naye wakati mwingine na alimtambua kuwa ni malaika wa Yehova. Gabrieli alimweleza kwa nini alimtembelea ghafla: “Ee Danieli, sasa nimekuja kukufanya upate ufahamu kwa kuelewa . . . kwa maana wewe ni mtu mwenye kutamanika sana.”—Danieli 9:21-23.

Katika pindi nyingine, mmoja wa malaika wa Yehova alimwambia Danieli hivi: “Ee Danieli, wewe mtu mwenye kutamanika sana.” Kisha, ili kumuimarisha Danieli, malaika huyo akasema: “Usiogope, Ee mtu mwenye kutamanika sana. Na uwe na amani.” (Danieli 10:11, 19) Danieli anatajwa mara tatu kuwa mtu “mwenye kutamanika sana.” Pia, maneno hayo yanaweza kumaanisha mtu “anayependwa sana,” “anayeheshimiwa sana,” hata “kipenzi.”

Bila shaka, Danieli tayari alihisi yuko karibu na Yehova Mungu wake na kwa kweli aliona kwamba alipendezwa na utumishi aliojitolea kufanya. Lakini ujumbe huo wa Mungu uliotolewa na malaika lazima uwe ulimwimarisha sana. Haishangazi kwamba, Danieli alisema hivi: “Umenitia nguvu.”—Danieli 10:19.

Simulizi hilo lenye kutia moyo kuhusu hisia nyororo za Yehova kuelekea nabii wake mwaminifu limeandikwa katika Neno la Mungu kwa faida yetu. (Waroma 15:4) Kutafakari kuhusu mfano wa Danieli kunatusaidia kuelewa ni nini kinachomfanya mtu apendwe na Baba yetu wa mbinguni.

Jifunze Neno la Mungu kwa Ukawaida

Danieli alikuwa mwanafunzi mwenye bidii wa Maandiko. Tunajua hilo kwa sababu yeye mwenyewe aliandika hivi: “Nilitambua kwa vitabu hesabu ya miaka . . . ya kutimiza ukiwa wa Yerusalemu.” (Danieli 9:2) Yaelekea vitabu alivyokuwa navyo wakati huo vilitia ndani maandishi yaliyoongozwa na roho ambayo yaliandikwa na Musa, Daudi, Sulemani, Isaya, Yeremia, Ezekieli, na manabii wengine. Tunaweza kuwazia Danieli akiwa amezungukwa na vitabu kadhaa vya kukunjwa, akivisoma kwa makini, na kulinganisha unabii mbalimbali uliohusu kurudishwa kwa ibada safi huko Yerusalemu. Yaelekea wakati huo Danieli alikuwa katika chumba chake cha darini, akitafakari maana ya maandiko hayo kwa makini bila kukengeushwa. Kwa kuwa alijifunza akiwa na kusudi maalumu, Danieli alikuwa na imani thabiti na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova.

Pia, kujifunza Neno la Mungu kulimsaidia Danieli aboreshe utu wake na maisha yake kwa ujumla. Bila shaka, miongozo ya Kimaandiko aliyopata akiwa bado kijana mdogo ilimsaidia aazimie kushika maagizo ya Sheria ya Mungu kuhusu vyakula yaliyofuatwa wakati huo. (Danieli 1:8) Baadaye, alitoa ujumbe wa Mungu kwa wafalme wa Babiloni bila woga. (Methali 29:25; Danieli 4:19-25; 5:22-28) Bidii, unyofu, na uaminifu wake ulijulikana sana. (Danieli 6:4) Zaidi ya yote, badala ya kulegeza msimamo wake ili aokoe maisha yake, Danieli alimtegemea Yehova kabisa. (Methali 3:5, 6; Danieli 6:23) Si ajabu kwamba alikuwa “mwenye kutamanika sana” mbele za Mungu!

Kwa kadiri fulani, leo ni rahisi zaidi kujifunza Biblia kuliko ilivyokuwa siku za Danieli. Badala ya vitabu vikubwa vya kukunjwa, sasa kuna vitabu ambavyo ni rahisi kubeba. Sasa tuna Biblia nzima, inayotia ndani maandishi yanayoonyesha jinsi unabii wa Danieli ulivyotimizwa. Tuna vitabu na vifaa vingi vya kutusaidia kujifunza Biblia na kufanya utafiti. * Je, unavitumia vizuri? Je, una ratiba ya kujifunza Biblia na kutafakari? Matokeo ya kufanya hivyo yatakuwa kama ilivyokuwa katika kisa cha Danieli. Utaweza kujenga imani yenye nguvu na kuimarisha uhusiano wako pamoja na Yehova. Neno la Mungu litakuwa mwongozo wenye kutegemeka katika maisha yako, likikupa uhakikisho wa kwamba anakujali.

Dumu Katika Sala

Danieli alikuwa mtu wa sala. Alisali kwa Mungu kuhusu mambo hususa. Akiwa kijana alikabili tisho la kuuawa ikiwa angeshindwa kutafsiri ndoto ya Mfalme Nebukadneza wa Babiloni. Bila kusita, Danieli alimsihi Yehova amsaidie na kumlinda. (Danieli 2:17, 18) Miaka kadhaa baadaye, akitambua udhaifu wake wa kibinadamu, nabii huyo mwaminifu alitubu dhambi zake na za watu wake na akamwomba Yehova msamaha. (Danieli 9:3-6, 20) Alipokosa kuelewa mambo ambayo alipewa kupitia mwongozo wa roho, Danieli alimwomba Mungu amsaidie. Katika kisa kimoja, malaika aliyemtembelea Danieli ili kumfafanulia mambo zaidi, alimwambia hivi: “Maneno yako yamesikiwa.”—Danieli 10:12.

Hata hivyo, kando na kumsihi Mungu, Danieli mwaminifu alifanya mengi zaidi. Andiko la Danieli 6:10 linasema: ‘Alikuwa akisali mara tatu kwa siku na kutoa sifa mbele za Mungu wake, kama vile alivyokuwa akifanya.’ Danieli alikuwa na sababu nyingi za kumshukuru na kumsifu Yehova. Na alifanya hivyo kwa ukawaida. Ndiyo, sala ilikuwa sehemu muhimu sana ya ibada yake hivi kwamba hakuacha kusali hata uhai wake ulipokuwa hatarini. Bila shaka, Yehova alimpenda kwa sababu ya ushikamanifu wake.

Pendeleo la sala ni zawadi nzuri kama nini! Usiruhusu siku ipite bila kuzungumza na Baba yako wa mbinguni. Kumbuka kumshukuru na kumsifu kwa mema yote anayokutendea. Mweleze mahangaiko yako kwa uhuru. Fikiria jinsi ambavyo sala au maombi yako yamejibiwa na umshukuru. Usisali haraka-haraka. Tunapomweleza Yehova yaliyo moyoni mwetu katika sala, tunahisi upendo wake kwa njia isiyo ya kawaida. Ndiyo maana tunahimizwa hivi: “Dumuni katika sala”!—Waroma 12:12.

Litukuze Jina la Mungu

Hakuna urafiki unaoweza kudumu ikiwa mtu mmoja ana ubinafsi. Hivyo ndivyo ilivyo kuhusu urafiki wetu pamoja na Yehova. Danieli alijua jambo hilo. Ona jinsi alivyohangaikia kulitukuza jina la Yehova.

Mungu alipojibu sala yake kwa kumfunulia ndoto ya Nebukadneza na maana yake, Danieli alisema hivi: “Jina la Mungu na libarikiwe kutoka wakati usio na kipimo mpaka wakati usio na kipimo, maana hekima na nguvu ni zake.” Baadaye alipokuwa akimjulisha Nebukadneza ndoto na maana yake, Danieli alimtukuza Yehova tena na tena, akikazia kwamba Yehova ndiye “Mfunuaji wa siri.” Vivyo hivyo, alipokuwa akimwomba Yehova awasamehe na kuwakomboa, Danieli alisali: “Ee Mungu wangu, . . . jina lako mwenyewe limeitwa juu ya jiji lako na juu ya watu wako.”—Danieli 2:20, 28; 9:19.

Tuna nafasi nyingi za kumwiga Danieli katika jambo hilo. Tunaposali tunaweza kuonyesha hangaiko letu la kutaka ‘jina la Mungu litakaswe.’ (Mathayo 6:9, 10) Hatutaki mwenendo wetu ufanye jina la Yehova lishutumiwe. Badala yake, acheni tuendelee kumtukuza Yehova kwa kuwaeleza wengine mambo ambayo tumejifunza kuhusu habari njema za Ufalme wa wake.

Bila shaka, katika ulimwengu wa leo, watu wengi hawawapendi wala kuwajali wanadamu wenzao. Hata hivyo, tunaweza kupata faraja kwa kujua kwamba Yehova kweli anawajali waabudu wake wakiwa mtu mmojammoja. Kama mtunga-zaburi anavyosema: “Yehova anawafurahia watu wake. Anawarembesha wapole kwa wokovu.”—Zaburi 149:4.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 18 Mashahidi wa Yehova wanaandaa vitabu na vifaa vingi unavyoweza kutumia kujifunza na kufanya utafiti, na hivyo kufanya usomaji na funzo lako la Biblia liwe na manufaa. Ikiwa ungependa kupata vifaa hivyo, tafadhali wasiliana na Shahidi wa Yehova yeyote.

[Blabu katika ukurasa wa 21]

Mungu alionyesha upendo wake kwa Danieli kwa kumtuma malaika Gabrieli ili amtie nguvu

[Blabu katika ukurasa wa 23]

Bidii ya Danieli ya kujifunza na kusali iliboresha utu wake na kufanya apendwe na Mungu