Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Shetani Alitumia Nyoka Kuzungumza na Hawa?

Kwa Nini Shetani Alitumia Nyoka Kuzungumza na Hawa?

Wasomaji Wetu Wanauliza . . .

Kwa Nini Shetani Alitumia Nyoka Kuzungumza na Hawa?

▪ Huenda ukakubali kuwa kama ilivyozungumziwa kwenye ukurasa wa 7, Shetani ndiye aliyefanya nyoka azungumze na Hawa. Hivyo ndivyo Biblia inavyofundisha. Hata hivyo, huenda ukajiuliza, ‘Kwa nini kiumbe wa roho mwenye nguvu azungumze kupitia nyoka?’

Biblia inafafanua mbinu za Shetani kuwa “hila,” au “matendo ya ujanja,” na tukio hilo linasaidia kuthibitisha jambo hilo. (Waefeso 6:11) Mambo yaliyotukia katika Edeni si hadithi tu kuhusu mnyama fulani anayezungumza; bali ni mfano wenye kuogopesha wa kutumia mbinu ya ujanja ili kuwakengeusha watu watoke kwa Mungu. Jinsi gani?

Shetani alichagua kwa makini mtu ambaye angemdanganya. Hawa ndiye aliyekuwa kiumbe mchanga zaidi kati ya viumbe wenye akili katika ulimwengu wote. Shetani alitumia hali ya Hawa ya kutokuwa na uzoefu ili kumdanganya na kumshawishi. Kwa kutumia nyoka, kiumbe ambaye ni mwenye kujihadhari sana, Shetani alificha kwa ujanja nia yake ya ushupavu na ya kujitakia makuu. (Mwanzo 3:1) Ona pia aliyotimiza kwa kumfanya nyoka aonekane kama anazungumza.

Kwanza, Shetani alinasa kabisa akili ya Hawa. Alijua kuwa nyoka hawazungumzi; mume wake alikuwa amewapa wanyama wote majina, kutia ndani nyoka, yaelekea baada ya kuwachunguza kwa makini. (Mwanzo 2:19) Yaelekea pia Hawa alikuwa amemchunguza kiumbe huyu mwenye kujihadhari. Kwa hiyo, mbinu ya Shetani ilimchochea Hawa awe mwenye udadisi; ikamfanya akazie fikira kitu kimoja tu katika shamba lote ambacho alikuwa amekatazwa. Pili, ikiwa nyoka alikuwa kwenye matawi ya mti uliokatazwa, Hawa alifikiria nini? Je, huenda alifikiri kwamba kiumbe huyo wa hali ya chini asiyeweza kuzungumza alikuwa amekula matunda hayo, kisha akawa na uwezo wa kuzungumza? Ikiwa matunda hayo yalimfanya nyoka azungumze, je, yangekuwa na matokeo gani juu yake? Hatuwezi kujua kwa uhakika Hawa alifikiria nini au kama nyoka alikuwa amekula matunda hayo, lakini tunajua kuwa nyoka alipomwambia Hawa kwamba matunda hayo yangemfanya awe “kama Mungu,” Hawa alikuwa tayari kuamini uwongo huo.

Maneno aliyochagua Shetani yanafunua mengi pia. Alimfanya Hawa awe na shaka, akimwonyesha kwamba Mungu alikuwa akimnyima kitu kizuri na kumwekea vizuizi bila sababu. Mbinu hiyo ya Shetani ingefaulu tu kama Hawa angependezwa na faida za kibinafsi zaidi ya alivyompenda Mungu ambaye alikuwa amempa kila kitu alichokuwa nacho. (Mwanzo 3:4, 5) Inasikitisha kuwa mbinu ya Shetani ilifaulu; Adamu na Hawa hawakuwa wamesitawisha mioyoni mwao aina ya upendo na uthamini ambao walipaswa kuwa nao kumwelekea Yehova. Je, leo Shetani hachochei watu kuwa na mtazamo kama huo wa kupendezwa na faida za kibinafsi tu na kutochukua mambo kwa uzito?

Namna gani nia ya Shetani? Alitaka nini? Huko Edeni, alijaribu kuficha yeye ni nani na ana nia gani. Lakini baada ya muda alijifunua. Alipomjaribu Yesu, alijua waziwazi kuwa hangeweza kuficha yeye ni nani. Kwa hiyo alimwambia Yesu moja kwa moja hivi: ‘Anguka chini na kunifanyia tendo la ibada.’ (Mathayo 4:9) Bila shaka, kwa muda mrefu Shetani amechochewa na wivu kuhusu ibada inayotolewa kwa Yehova Mungu. Atafanya yote awezayo kuwazuia watu wasimwabudu Mungu au wamwabudu kwa njia asiyokubali. Anapenda kutushawishi tusiendelee kuwa waaminifu kwa Mungu.

Kwa wazi, Biblia inamfunua Shetani kuwa kiumbe anayetumia mbinu mbaya ili atimize malengo yake. Inafurahisha kujua kuwa si lazima tudanganywe kama Hawa alivyodanganywa, “kwa maana sisi hatukosi kuzijua mbinu zake.”—2 Wakorintho 2:11.