Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Habari Njema Ni Nini?

Habari Njema Ni Nini?

Habari Njema Ni Nini?

“Hii habari njema . . .”—MATHAYO 24:14.

WAKRISTO wanapaswa kuhubiri “habari njema ya ufalme” kwa kuwaeleza wengine kuuhusu, wakifafanua kwamba Ufalme huo ni serikali ya wakati ujao itakayoitawala dunia kwa uadilifu. Hata hivyo, maneno “habari njema” yametumiwa kwa njia nyinginezo katika Biblia. Kwa mfano, tunasoma kuhusu “habari njema za wokovu” (Zaburi 96:2); “habari njema ya Mungu” (Waroma 15:16); na “habari njema juu ya Yesu Kristo.”—Marko 1:1.

Kwa ufupi, habari njema inatia ndani kweli zote zilizofundishwa na Yesu na kuandikwa na wanafunzi wake. Kabla hajapanda mbinguni, Yesu aliwaambia hivi wafuasi wake: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.” (Mathayo 28:19, 20) Hivyo, kazi ya Wakristo wa kweli si kuwaeleza tu wengine kuhusu Ufalme; wanapaswa pia kujitahidi kufanya wanafunzi.

Je, makanisa yanatii agizo hilo? Watu wengi hawafahamu Ufalme ni nini, hivyo hawawezi kuwafundisha wengine kwa usahihi kuuhusu. Badala yake, wanahubiri mambo yanayokusudiwa kuwafurahisha watu, kama vile msamaha wa dhambi na kumwamini Yesu. Pia, wanajitahidi kupata waumini kwa kujaribu kuboresha maisha ya watu au kwa kujenga hospitali, shule, na kuwajengea maskini nyumba. Ingawa shughuli hizo zinaweza kuongeza idadi ya waumini wa kanisa, hazitokezi Wakristo wa kweli wanaojitahidi kwa unyofu kuishi kulingana na mambo ambayo Yesu alifundisha.

Mwanatheolojia mmoja aliandika hivi: “Ni wasomi au viongozi wachache miongoni mwa Wakristo wanaopinga kwamba tunapaswa kuwafanya watu kuwa wanafunzi wa Yesu na kuwafundisha kufanya mambo yote ambayo Yesu alisema. . . . Maagizo ya Yesu kuhusu jambo hilo ni wazi kabisa. Lakini hatufanyi wala hatujaribu hata kidogo kufanya yale aliyotuagiza tufanye. Na inaonekana hata hatujui jinsi ya kuyafanya.”

Vivyo hivyo, uchunguzi uliohusisha Wakatoliki nchini Marekani ulionyesha kwamba asilimia 95 ya watu walikubali kwamba kuhubiri habari njema ni takwa la imani yao. Hata hivyo, wote walihisi kuwa njia bora ya kuhubiri habari njema si kuwaeleza wengine kuihusu, bali ni kuishi kwa njia itakayokuwa mfano kwa wengine. Mmoja wa wale waliohojiwa alisema: “Kuhubiri hakumaanishi kuzungumza tu na watu. Tunapaswa kuishi kulingana na Habari Njema.” Gazeti lililofanya uchunguzi huo (U.S. Catholic), lilisema kwamba wengi husita kuwaeleza wengine kuhusu imani yao kwa sababu ya “sifa mbaya ya kanisa inayotokana na visa vya hivi karibuni vya unyanyasaji wa kingono na mafundisho ya kanisa yenye utata.”

Kwingineko, askofu wa Kanisa la Methodisti alisikitika kwamba kanisa lake limegawanyika na kuchanganyikiwa na linakosa ujasiri wa kutimiza utume wake, na kuwa waumini wake wengi wanaishi tu kama watu wa ulimwengu. Akionekana kuwa amekata tamaa, aliuliza: “Ni nani walio na jukumu la kuhubiri habari njema ya Ufalme?”

Askofu huyo hakujibu swali lake. Lakini kuna jibu. Utalipata katika makala inayofuata.

[Blabu katika ukurasa wa 6]

Habari njema inahusu Ufalme wa Mungu na ukombozi unaopatikana kwa kumwamini Yesu Kristo