Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ufalme wa Mungu Ni Nini?

Ufalme wa Mungu Ni Nini?

Ufalme wa Mungu Ni Nini?

“Hii habari njema ya ufalme . . .”—MATHAYO 24:14.

KATIKA Mahubiri yake ya Mlimani yanayojulikana sana, Yesu alifundisha sala ya kielelezo, ambayo inatia ndani ombi hili linalotolewa kwa Mungu: “Ufalme wako na uje.” Watu wengi wameikariri sala hiyo na wameirudia-rudia mara nyingi. Kitabu kimoja cha marejeo kinasema kuwa “hiyo ndiyo sala kuu inayotumiwa na Wakristo wote katika ibada yao ya kawaida.” Hata hivyo, wengi wanaorudia-rudia maneno ya sala hiyo hawajui Ufalme ni nini wala hawajui utafanya nini utakapokuja.—Mathayo 6:9, 10.

Hilo si jambo linaloshangaza. Kwa kuwa viongozi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo husema mambo yenye kupingana, kuchanganya, na magumu kueleweka wanapoufafanua Ufalme. Mwandishi mmoja anasema kwamba Ufalme wa Mungu ni “kitu kisicho cha kawaida, . . . uhusiano wa ndani kati yetu na Mungu aliye hai . . . , mambo tunayojionea kumhusu Mungu ambayo katika hayo wanaume na wanawake wanapata ukombozi.” Mwingine anaelezea injili kuhusu Ufalme kuwa “miongozo kuhusu kanisa.” Na kitabu kimoja cha Kanisa Katoliki (Catechism of the Catholic Church) kinasema: “Ufalme wa Mungu [ni] uadilifu na amani na shangwe katika Roho Mtakatifu.”

Utapata ufafanuzi ulio wazi zaidi katika ukurasa wa 2 wa gazeti hili. Ufafanuzi huo unasema: “Hivi karibuni Ufalme wa Mungu, ambao ni serikali halisi iliyo mbinguni, utakomesha uovu wote na kuigeuza dunia kuwa paradiso.” Acheni tuone jinsi Biblia inavyounga mkono maoni hayo.

Watakaoitawala Dunia Yote Wakati Ujao

Ufalme ni serikali inayoongozwa na mfalme. Mfalme wa Ufalme wa Mungu ni Yesu Kristo aliyefufuliwa. Kuwekwa kwake kuwa mfalme mbinguni kulifafanuliwa katika maono aliyopewa nabii Danieli, ambaye aliandika: “Nikaendelea kuona katika maono ya usiku, na, tazama! mtu fulani kama mwana wa binadamu [Yesu] alikuwa anakuja na mawingu ya mbingu; naye akaja kwa Mzee wa Siku, [Yehova Mungu] nao wakamleta karibu mbele zake Yule. Naye akapewa utawala na heshima na ufalme, ili vikundi vyote vya watu, vya mataifa na lugha vimtumikie yeye. Utawala wake ni utawala unaodumu mpaka wakati usio na kipimo ambao hautapitilia mbali, na ufalme wake ni ufalme ambao hautaharibiwa.”—Danieli 7:13, 14.

Kitabu cha Danieli pia kinaonyesha kwamba Mungu atauimarisha kabisa Ufalme huo ambao utazikomesha falme zote za kibinadamu, nao hautapinduliwa kamwe. Sura ya 2 inafafanua kuhusu ndoto iliyoongozwa na roho ambayo mfalme wa Babiloni aliota. Katika ndoto hiyo, aliona sanamu kubwa iliyowakilisha mfuatano wa serikali kuu za ulimwengu. Nabii Danieli aliifasiri ndoto hiyo. Nabii huyo aliandika, “Katika siku za mwisho . . . Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaharibiwa kamwe. Na ufalme huo hautapewa watu wengine wowote. Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote, nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.”—Danieli 2:28, 44.

Mfalme wa Ufalme wa Mungu hatatawala peke yake. Wakati wa huduma yake hapa duniani, Yesu aliwahakikishia mitume wake waaminifu kwamba wao, pamoja na watu wengine, wangefufuliwa na kuketi katika viti vya ufalme mbinguni. (Luka 22:28-30) Yesu hakumaanisha viti halisi vya ufalme, kwa kuwa kama alivyoonyesha, Ufalme huo ungekuwa mbinguni. Biblia inaeleza kuwa hao watawala wenzake wanatoka katika “kila kabila na lugha na watu na taifa.” Wangekuwa ‘ufalme na makuhani kwa Mungu wetu, nao wangetawala wakiwa wafalme juu ya dunia.’—Ufunuo 5:9, 10.

Kwa Nini Habari Kuhusu Ufalme Huo Ni Njema?

Ona kwamba Kristo Yesu amepewa utawala juu ya “vikundi vyote vya watu, vya mataifa na lugha” na wale watakaoshirikiana naye “watatawala wakiwa wafalme juu ya dunia.” Ni nani watakaokuwa raia wa Ufalme huo? Wale wanaokubali habari njema inayohubiriwa leo. Raia hao wanatia ndani wale watakaofufuliwa hapa duniani wakiwa na tumaini la kuishi milele.

Biblia inaeleza waziwazi baraka ambazo watu watazifurahia chini ya Ufalme huo. Ona baadhi ya baraka hizo:

“Anakomesha vita mpaka kwenye mwisho wa dunia. Upinde anauvunja na kuukata mkuki vipande-vipande; magari ya kukokotwa anayateketeza motoni.”Zaburi 46:9.

“Hakika wao watajenga nyumba na kukaa ndani yake; na hakika wao watapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake. Hawatajenga na mtu mwingine akae ndani yake; hawatapanda na mtu mwingine ale.”Isaya 65:21, 22.

[Mungu] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”Ufunuo 21:3, 4.

“Wakati huo macho ya vipofu yatafunguliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Wakati huo kilema atapanda juu kama vile paa anavyofanya, na ulimi wa bubu utapaaza sauti kwa furaha.”Isaya 35:5, 6.

“Saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti [ya Yesu] na kutoka, wale waliotenda mambo mema kwenye ufufuo wa uzima.”Yohana 5:28, 29.

“Wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”Zaburi 37:11.

Bila shaka, hiyo ni habari njema! Zaidi ya hayo, unabii mbalimbali wa Biblia uliotimizwa unaonyesha kuwa wakati umekaribia kwa Ufalme kuanza kuitawala dunia yote kwa uadilifu.