Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Majina yaliyo katika mihuri ya kale ya udongo yanafanana jinsi gani na majina yanayopatikana katika Biblia?

Nyakati za zamani, wale walioshughulikia nyaraka rasmi walizikunja na kuzifunga kwa kamba, kisha wakaweka donge la udongo mbichi kwenye fundo walilofunga na kupiga mhuri juu yake. Walitumia mhuri kuweka sahihi, kuthibitisha, na kufanya nyaraka ziwe halali.

Baadaye, mihuri iliwekwa katika pete na zilionwa kuwa vitu vyenye thamani. (Mwanzo 38:18; Esta 8:8; Yeremia 32:44) Mara nyingi, mhuri ulikuwa na jina la mwenye pete, cheo chake, na jina la baba yake.

Watafiti wamepata mamia ya vifaa vyenye alama za mihuri ya kale vinavyoitwa bullae. Baadhi ya alama hizo zinatia ndani majina ya watu wanaotajwa katika Biblia. Kwa mfano, wataalamu wa vitu vya kale wamepata alama zinazoaminika kuwa zilitokana na mihuri ya kibinafsi ya wafalme wawili wa Yudea. Mhuri mmoja uliotumiwa ulikuwa na maneno haya: “Ni mali ya Ahazi [mwana wa] Yehotam [Yothamu], Mfalme wa Yuda.” Na mwingine ulisema hivi: “Ni mali ya Hezekia [mwana wa] Ahazi, Mfalme wa Yuda.” (2 Wafalme 16:1, 20) Ahazi na Hezekia walitawala katika karne ya nane K.W.K.

Wasomi wamechunguza bullae nyingine kadhaa ambazo zimepingwa mihuri inayoaminika kuwa ilimilikiwa na watu fulani wanaotajwa katika Biblia. Baadhi ya watu hao ni wale wanaotajwa katika maandishi ya Yeremia, kama vile Baruku (mwandishi wa Yeremia), Gemaria (“mwana wa Shafani”), Yerahmeeli (“mwana wa mfalme”), Yukali (“mwana wa Shelemia”), na Seraya (ndugu ya Baruku).—Yeremia 32:12; 36:4, 10, 26; 38:1; 51:59.

Nyakati tofauti za siku zinaelezwa jinsi gani katika Biblia?

Maandiko ya Kiebrania yanatumia maneno kama vile “asubuhi,” “katikati ya mchana,” na “jioni.” (Mwanzo 24:11; Kumbukumbu la Torati 28:29; 1 Wafalme 18:26) Waebrania waligawanya usiku katika makesha matatu yenye urefu wa saa nne hivi lakini baadaye walifuata mfumo wa Wagiriki na Waroma waliogawanya usiku katika vipindi vinne. Ni wazi kwamba Yesu alirejelea njia hiyo ya Wagiriki na Waroma ya kugawanya saa za usiku aliposema hivi: “Endeleeni kukesha, kwa maana hamjui bwana wa nyumba anakuja wakati gani, kama ni wakati wa jioni au katikati ya usiku au anapowika jogoo au asubuhi na mapema.” (Marko 13:35) Kipindi cha kesha la “jioni-jioni” kilianza jua lilipotua hadi saa tatu usiku. Kipindi kilichofuata kiliendelea hadi katikati ya usiku na kipindi cha tatu, yaani, “anapowika jogoo,” kiliendelea hadi saa tisa usiku. Kipindi cha mwisho, yaani, kesha la kuamkia asubuhi, kiliendelea hadi jua lilipochomoza. Yesu alitembea juu ya maji ya Bahari ya Galilaya wakati wa “kipindi cha kesha la nne la usiku.”​—Mathayo 14:⁠23-​26.

Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, ­kipindi cha mchana kiligawanywa katika sehemu 12, hivyo, neno “saa” lilirejelea se­hemu moja ya sehemu hizo 12. Kipindi cha mchana kilihesabiwa kuanzia jua lilipochomoza hadi lilipotua. (Yohana 11:9) Kuchomoza na kutua kwa jua huko Israeli kulitofautiana kulingana na majira, hivyo, watu walikadiria tu wakati ambapo tukio lilitokea, kama “karibu saa sita.”​​—⁠Matendo 10:9.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Mihuri ya udongo yenye jina la Hezekia na Ahazi (mbele) na yaelekea jina la Baruku (nyuma)

[Hisani]

Back: Courtesy of Israel Museum, Jerusalem

Front: www.BibleLandPictures.com/​Alamy

[Picha katika ukurasa wa 15]

Saa ya kivuli, wakati wa utawala wa Roma (27 K.W.K.—476 W.K.)

[Hisani]

© Gerard Degeorge/​The Bridgeman Art Library International