Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unabii wa 4. Watu Hawatakuwa na Upendo wa Asili

Unabii wa 4. Watu Hawatakuwa na Upendo wa Asili

Unabii wa 4. Watu Hawatakuwa na Upendo wa Asili

“Watu watakuwa . . . wasiowapenda wa kwao.”—2 TIMOTHEO 3:1-3, Union Version.

● Chris anafanya kazi na kikundi cha kuwasaidia watu wanaokabili jeuri nyumbani, huko Wales Kaskazini. “Ninakumbuka mwanamke mmoja ambaye alikuwa amepigwa vibaya sana hivi kwamba nisingeweza kumtambua ingawa nilikuwa nimemwona hapo awali,” anasema Chris. “Wanawake wengine huathiriwa sana kihisia kiasi kwamba hawawezi kuinua macho yao kukutazama.”

MAMBO YA HAKIKA YANAONYESHA NINI? Katika nchi moja barani Afrika, inakadiriwa kwamba mwanamke 1 kati ya kila wanawake 3 alilalwa kinguvu akiwa mtoto. Uchunguzi uliofanywa katika nchi hiyo ulionyesha kwamba zaidi ya asilimia 33 ya wanaume wanaona kwamba ni sawa kuwapiga wake zao. Hata hivyo, si wanawake tu wanaokabili jeuri nyumbani. Kwa mfano, nchini Kanada, karibu wanaume 3 kati ya kila wanaume 10 wamepigwa au kutendewa vibaya na wanawake wanaoishi nao.

NI KIPINGAMIZI GANI KINACHOTOLEWA MARA NYINGI? Jeuri inayotokea nyumbani si jambo jipya, imekuwako sikuzote. Lakini wakati huu inatangazwa zaidi kuliko hapo zamani.

JE, KIPINGAMIZI HICHO KINA MSINGI? Katika miaka ya hivi karibuni, jeuri inayotokea nyumbani imetangazwa sana. Lakini je, jambo hilo limefanya visa vya jeuri inayotokea nyumbani vipungue? Hapana. Watu wasio na upendo wa asili wanazidi kuongezeka.

UNA MAONI GANI? Je, andiko la 2 Timotheo 3:1-3 linatimia? Je, watu wengi wanakosa upendo kwa familia zao, sifa ambayo kiasili wanapaswa kuwa nayo?

Unabii wa tano unaotimia sasa unahusu dunia, makao yetu. Ona yale ambayo Biblia inasema kuhusu jambo hilo.

[Blabu katika ukurasa wa 7]

“Jeuri inayotokea nyumbani ni mojawapo ya mambo yanaripotiwa mara chache sana katika jamii. Mwanamke atashambuliwa mara 35 hivi na mwanamume anayeishi naye kabla ya kuripoti jambo hilo kwa polisi.”​—MSEMAJI WA KITUO CHA KUWASAIDIA WATU WANAOTENDEWA JEURI NYUMBANI NCHINI WALES.