Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Habari Njema Kwa Maskini

Habari Njema Kwa Maskini

Habari Njema Kwa Maskini

NENO LA MUNGU linatuhakikishia: “Maskini hawatasahauliwa sikuzote.” (Zaburi 9:18) Biblia pia inasema hivi kumhusu Muumba wetu: “Unaufumbua mkono wako na kutosheleza tamaa ya kila kitu kilicho hai.” (Zaburi 145:16) Tumaini hilo linalopatikana katika Neno la Mungu si ndoto tu. Mungu Mweza Yote anaweza kuandaa chochote kinachohitajiwa ili kumaliza umaskini. Maskini wanahitaji nini?

Mtaalamu fulani wa uchumi wa nchi za Afrika alisema kwamba nchi maskini zinahitaji “dikteta mwenye fadhili.” Alimaanisha kwamba ili kumaliza umaskini, kunahitajika mtawala mwenye mamlaka ya kuchukua hatua za kuumaliza, na mwenye fadhili zinazomsukuma kufanya hivyo. Tunaweza pia kuongezea kwamba mtu anayeweza kuwaondolea watu wote umaskini anapaswa kuwa mtawala wa dunia yote, kwa sababu mara nyingi umaskini wa kupindukia hutokana na kutokuwepo kwa usawa kati ya mataifa. Zaidi ya hayo, mtawala huyo anapaswa kuwa na uwezo wa kukabiliana na chanzo cha umaskini, yaani, mwelekeo wa mwanadamu wa kuwa na ubinafsi. Mtawala kama huyo anaweza kupatikana wapi?

Mungu alimtuma Yesu akiwa na habari njema kwa maskini. Yesu aliposimama kusoma kuhusu mgawo, au kazi, aliyopewa na Mungu, alisema: “Roho ya Yehova iko juu yangu, kwa sababu alinitia mafuta kuwatangazia maskini habari njema.”—Luka 4:16-18.

Habari Njema Ni Nini?

Mungu amemweka Yesu kuwa Mfalme. Hizo kwa kweli ni habari njema. Yeye ndiye Mtawala anayefaa kabisa kumaliza umaskini kwa sababu (1) atatawala wanadamu wote na ana mamlaka ya kuchukua hatua zinazohitajika ili kuumaliza; (2) anawatendea maskini kwa huruma na anawafundisha wafuasi wake kuwajali; na (3) anaweza kuondoa chanzo cha umaskini ambacho ni mwelekeo tuliorithi wa kuwa na ubinafsi. Acheni tuchunguze sehemu hizo tatu za habari njema.

1. Mamlaka ya Yesu juu ya mataifa yote Neno la Mungu linasema hivi kumhusu Yesu: “Akapewa utawala . . . ili vikundi vyote vya watu, vya mataifa na lugha vimtumikie yeye.” (Danieli 7:14) Hebu fikiria faida za kuwa na serikali moja tu duniani kote? Serikali kama hiyo inaweza kumaliza ugomvi na hali ya kung’ang’ania maliasili za dunia. Raia wote watafaidika. Yesu mwenyewe alituhakikishia kwamba atakuwa Mtawala wa ulimwengu wote, mwenye mamlaka ya kuchukua hatua. Alitangaza hivi: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.”—Mathayo 28:18.

2. Yesu anawahurumia maskini Wakati wa huduma yake yote duniani, Yesu aliwatendea maskini kwa huruma. Kwa mfano, mwanamke fulani aliyekuwa ametumia mali zake zote kulipia matibabu yake aligusa vazi la Yesu, akitazamia kuponywa. Alikuwa na mtiririko wa damu kwa miaka 12 na bila shaka alikuwa na upungufu mkubwa wa damu mwilini. Kulingana na Sheria, angemtia unajisi mtu yeyote aliyemgusa. Lakini Yesu alimwonyesha huruma. Alimwambia: “Binti yangu, imani yako imekuponya. Nenda kwa amani, na uwe na afya njema kutokana na ugonjwa wako wenye kuhuzunisha.”—Marko 5:25-34.

Mafundisho ya Yesu yana uwezo wa kubadili mioyo ya watu ili watende kwa huruma pia. Kwa mfano, fikiria vile Yesu alivyomjibu mtu fulani aliyetaka kujua jinsi ya kumpendeza Mungu. Mtu huyo alijua kuwa Mungu anataka sisi tuwapende jirani zetu, lakini akamuuliza Yesu: “Ni nani kwa kweli aliye jirani yangu?”

Katika jibu lake, Yesu alitoa mfano wa mtu aliyekuwa anasafiri kutoka Yerusalemu kwenda Yeriko ambaye alinyang’anywa vitu na kuachwa akiwa “karibu kufa.” Kuhani aliyekuwa akishuka kwenye barabara hiyo, alipita upande ule mwingine. Mlawi naye akafanya vivyo hivyo. “Lakini Msamaria fulani aliyekuwa akisafiri katika barabara ile alikuja, akamkuta na, alipomwona, akamsikitikia.” Alisafisha majeraha ya mtu huyo, akampeleka kwenye nyumba ya wageni, na kumlipa mtu aliyekuwa akitunza nyumba hiyo ili amtunze. “Ni nani . . . alijifanya kuwa jirani kwa mtu aliyeanguka katikati ya wanyang’anyi?” Yesu akamuuliza. Naye akajibu, “Ni yule aliyemtendea kwa rehema.” Ndipo Yesu akamwambia: “Uwe ukifanya vivyo hivyo.”—Luka 10:25-37.

Watu wanaokuwa Mashahidi wa Yehova wanajifunza mambo hayo ambayo Yesu alifundisha na kubadili mtazamo wao kuelekea kuwasaidia wenye uhitaji. Kwa mfano, mwandishi fulani kutoka Latvia aliandika kwenye kitabu chake, Women in Soviet Prisons, kuhusu ugonjwa uliompata alipokuwa akifanya kazi kwenye kambi ya gereza huko Potma katikati ya miaka ya 1960. “Wakati wote nilipokuwa mgonjwa [Mashahidi] walinitunza vizuri sana. Nilifurahia sana utunzaji wao.” Aliongeza kusema: “Mashahidi wa Yehova wanaona kuwa ni jukumu lao kumsaidia yeyote, hata awe wa dini au taifa gani.”

Wakati matatizo ya kiuchumi yalipofanya Mashahidi wa Yehova fulani wapoteze kazi au mapato yao huko Ancón, Ekuado, Mashahidi wenzao waliamua kufanya jambo fulani ili kuwachangia pesa. Walipika chakula na kuwauzia wavuvi wanaorudi ufuoni baada ya kuvua samaki usiku (picha upande wa kulia). Wote walishirikiana, kutia ndani watoto. Walianza kupika saa saba usiku kila siku ili chakula kiwe tayari wakati wavuvi waliporudi saa kumi usiku. Pesa walizopata ziligawanywa kulingana na mahitaji ya kila mmoja.

Visa kama hivyo vinaonyesha kwamba mfano na mafundisho ya Yesu yana uwezo wa kubadili mtazamo wa watu ili kuwasaidia walio na uhitaji.

3. Uwezo wa Yesu wa kubadili mwelekeo wenye dhambi tuliorithi Mwelekeo wa mwanadamu wa kutenda kwa ubinafsi ni jambo ambalo sote tunajua na tunakubali lipo. Biblia inauita mwelekeo huo dhambi. Hata mtume Paulo aliandika: “Basi, mimi naona sheria hii katika hali yangu: kwamba ninapotaka kufanya yaliyo sawa, yaliyo mabaya yapo pamoja nami.” Kisha akaongeza: “Ni nani atakayeniokoa kutoka katika mwili unaopatwa na kifo hiki? Shukrani kwa Mungu kupitia Yesu Kristo.” (Waroma 7:21-25) Hapa Paulo alirejelea jinsi ambavyo Mungu kupitia Yesu, angewakomboa waabudu wa kweli kutoka katika mielekeo yenye dhambi waliyorithi, kama vile ubinafsi, ambao ndio chanzo kikuu cha umaskini. Angefanya hivyo jinsi gani?

Muda fulani baada ya Yesu kubatizwa, Yohana Mbatizaji alimtambulisha akisema: “Ona, Mwana-Kondoo wa Mungu ambaye huondolea mbali dhambi ya ulimwengu!” (Yohana 1:29) Hivi karibuni, dunia itajaa watu waliokombolewa kutoka katika dhambi tuliyorithi, kutia ndani mwelekeo wetu wa kuwa na ubinafsi. (Isaya 11:9) Yesu atakuwa ameondoa chanzo cha umaskini.

Tunafurahi kama nini tunapotafakari kuhusu wakati ambapo kila mtu atatimiziwa mahitaji yake! Neno la Mungu linasema: “Wataketi, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake, wala hakutakuwa na mtu yeyote anayewatetemesha.” (Mika 4:4) Maneno hayo ni kama shairi linaloelezea wakati ambapo watu wote watakuwa na kazi yenye kuridhisha, usalama, na nafasi tele za kufurahia ulimwengu usio na umaskini. Mambo hayo yatamletea Yehova sifa.