Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Aliwatetea Watu wa Mungu

Aliwatetea Watu wa Mungu

Igeni Imani Yao

Aliwatetea Watu wa Mungu

ESTA alijaribu kutuliza moyo wake alipokaribia ua wa jumba la mfalme huko Shushani. Haikuwa rahisi kufanya hivyo. Jumba hilo lilikuwa na michongo yenye rangi mbalimbali ya ng’ombe dume wenye mabawa, wapiga-mishale, na michongo ya simba ambayo ilikuwa kwenye kuta za matofali yenye kung’aa, nguzo ndefu zilizorembeshwa, na sanamu zenye kuvutia. Pia, lilikuwa kubwa sana na lilikuwa limejengwa karibu na Milima ya Zagros iliyofunikwa kwa theluji kwenye eneo lililoinuka karibu na maji safi ya mto Choaspes. Mambo hayo yote yalikusudiwa kumkumbusha kila mgeni mamlaka kuu ya mtu ambaye Esta alikuwa ameenda kumwona, na ambaye alijiita “mfalme mkuu.” Mfalme huyo alikuwa mume wake.

Mume mwenye mamlaka kwelikweli! Bila shaka, Ahasuero alikuwa tofauti kabisa na mume ambaye msichana mwaminifu wa Kiyahudi angetazamia kupata! * Hangelinganishwa kamwe na Abrahamu, mwanamume ambaye kwa unyenyekevu alikubali mwongozo wa Mungu na kumsikiliza Sara, mke wake. (Mwanzo 21:12) Mfalme huyo hakujua mengi au jambo lolote kumhusu Yehova, Mungu wa Esta, wala Sheria Zake. Hata hivyo, Ahasuero alijua sheria za Waajemi kutia ndani sheria iliyokataza jambo ambalo Esta alikuwa karibu kufanya. Jambo gani hilo? Sheria hiyo ilisema kuwa mtu yeyote ambaye angeenda mbele ya mfalme wa Waajemi bila kuitwa na mfalme, angepaswa kuuawa. Esta hakuwa ameitwa, lakini alikuwa anaenda mbele ya mfalme. Alipokuwa akikaribia ua wa ndani mahali ambapo mfalme angemwona akiwa kwenye kiti chake, huenda Esta alihisi kana kwamba anaenda kuuawa.—Esta 4:11; 5:1.

Kwa nini Esta alihatarisha uhai wake hivyo? Na tunaweza kujifunza nini kutokana na imani ya mwanamke huyo wa pekee? Kwanza acheni tuchunguze jinsi Esta alivyokuja kuwa malkia huko Uajemi.

“Alikuwa Mrembo”

Esta alikuwa yatima. Hatujui mengi kuhusu wazazi wake waliompa jina Hadasa, neno la Kiebrania linalomaanisha “mhadasi,” mmea wenye kupendeza unaochanua maua meupe. Wazazi wa Esta walipokufa, mmoja wa watu wake wa ukoo, mwanamume mwenye huruma anayeitwa Mordekai, alimsikitikia mtoto huyo. Mordekai alikuwa binamu ya Esta, lakini alikuwa na umri mkubwa zaidi. Alimchukua Esta na kumlea kama binti yake.—Esta 2:5-7, 15.

Mordekai na Esta walikuwa Wayahudi waliohamishwa na waliishi katika mji mkuu wa Waajemi, ambako huenda walidhihakiwa kwa sababu ya dini yao na Sheria ambazo walijitahidi kufuata. Lakini ni wazi kwamba Esta alisitawisha uhusiano wa karibu na binamu yake alipokuwa akimfundisha kuhusu Yehova, Mungu mwenye rehema ambaye aliwaokoa watu wake hapo zamani kutoka katika matatizo mengi—na ambaye angewaokoa tena. (Mambo ya Walawi 26:44, 45) Kwa kweli, uhusiano wa karibu na wenye upendo uliimarika kati ya Esta na Mordekai.

Inaonekana kwamba Mordekai alifanya kazi akiwa ofisa katika makao ya mfalme huko Shushani na alikuwa akiketi kwa ukawaida katika lango la makao hayo pamoja na watumishi wengine wa mfalme. (Esta 2:19, 21; 3:3) Hatujui mambo ambayo Esta alifanya alipokuwa kijana, lakini inaonekana kwamba alimsaidia binamu yake mkubwa na akasaidia kutunza nyumba yake, ambayo huenda ilikuwa katika sehemu ya mji iliyotengewa watu maskini ng’ambo ya mto kutoka kwa makao ya mfalme. Labda alifurahia kwenda sokoni huko Shushani, ambako mafundi wa dhahabu na wa fedha, na wafanyabiashara wengine waliuza bidhaa zao. Esta hangewazia kwamba baadaye angepata kwa wingi vitu hivyo vya bei ghali; hakujua kamwe mambo ambayo yangetukia baadaye.

Malkia Aondolewa

Wakati fulani, watu katika jiji la Shushani walikuwa wakieneza porojo kuhusu matatizo yaliyokuwa katika nyumba ya mfalme. Katika sherehe fulani kubwa, ambapo Ahasuero alikuwa akiwatumbuiza wakuu wake kwa chakula cha bei ghali na mvinyo, aliamua kumwita malkia wake mrembo, Vashti, ambaye alikuwa akisherehekea na wanawake katika chumba tofauti. Lakini Vashti alikataa kuja. Akiwa ameaibika na kukasirika, mfalme aliwauliza washauri wake jinsi ya kumwadhibu Vashti. Matokeo yalikuwa nini? Aliondolewa kuwa malkia. Kisha, watumishi wa mfalme wakaanza kuzunguka kotekote nchini wakitafuta wasichana warembo walio mabikira. Mfalme angechagua mmoja kati yao awe malkia.—Esta 1:1–2:4.

Tunaweza kuwazia Mordekai akimtazama Esta mara kwa mara kwa wasiwasi na wakati huohuo akijivunia kwamba binamu yake mdogo alikuwa amekomaa na kuwa msichana mrembo sana. Tunasoma hivi: “Mwanamke [huyo] kijana alikuwa mrembo na mwenye umbo linalopendeza.” (Esta 2:7) Urembo wa nje ni wenye kuvutia, lakini mwanamke mrembo anahitaji pia kuwa na sifa ya hekima na unyenyekevu. Bila sifa hizo, urembo unaweza kumfanya awe na majivuno, kiburi, na kusitawisha moyoni tabia nyingine zisizofaa. (Methali 11:22) Je, umewahi kujionea ukweli wa jambo hilo? Katika kisa cha Esta, je, urembo wake ungemsaidia au ungemfanya awe na sifa mbaya? Baada ya muda, jambo hilo lingethibitika.

Watumishi wa mfalme walimwona Esta na kumchukua kutoka kwa Mordekai, kisha wakampeleka kwa jumba la kifahari la mfalme lililokuwa ng’ambo ya mto. (Esta 2:8) Kwa kweli, haikuwa rahisi kwa Esta na binamu yake kuachana, kwa sababu walikuwa kama baba na binti yake. Mordekai hakutaka Esta aolewe na mtu asiyeamini Mungu, hata awe mfalme, lakini hangeweza kuzuia jambo hilo. Kabla hajachukuliwa, lazima Esta awe alisikiliza kwa makini mashauri ya Mordekai. Alipokuwa akipelekwa kwenye makao ya mfalme huko Shushani, Esta alikuwa na maswali mengi akilini. Angeishi maisha ya aina gani?

Alipata Kibali “Machoni pa Kila Mtu Aliyemwona”

Maisha ya Esta yalibadilika na kuwa tofauti kabisa. Alikuwa kati ya “wanawake wengi vijana” waliokuwa wamekusanywa kutoka maeneo mbalimbali ya Milki ya Uajemi. Lazima tamaduni, lugha, na mitazamo yao ilitofautiana kabisa. Chini ya usimamizi wa ofisa anayeitwa Hegai, wanawake hao vijana wangerembeshwa sana katika programu ya mwaka mmoja iliyotia ndani kukandwa kwa mafuta yenye marashi. (Esta 2:8, 12) Huenda hali hiyo ilifanya wasichana hao wafikirie sana urembo wao, wawe na kiburi, na kushindana. Esta aliathiriwa jinsi gani?

Bila shaka, Mordekai alijali sana hali ya Esta. Tunasoma kwamba siku baada ya siku, alienda karibu wa nyumba ya wanawake ili apate kujua hali ya Esta. (Esta 2:11) Habari chache alizopata, labda kutoka kwa wafanyakazi walioshirikiana naye, lazima zilimfurahisha sana. Kwa nini?

Hegai alivutiwa sana na mwenendo wa Esta hivi kwamba alimtendea kwa fadhili sana na kumpa vijakazi saba na mahali bora zaidi katika nyumba ya wanawake. Simulizi hilo hata linasema hivi: “Wakati huo wote Esta alikuwa akizidi kupata kibali machoni pa kila mtu aliyemwona.” (Esta 2:9, 15) Je, urembo peke yake ndio uliofanya kila mtu avutiwe sana naye? Hapana, Esta alikuwa na sifa nyingine nzuri.

Kwa mfano, tunasoma: “Esta hakuwa amesema kuhusu watu wake wala kuhusu jamaa zake, kwa maana Mordekai alikuwa amemwamuru kwamba asiseme.” (Esta 2:10) Mordekai alikuwa amemwagiza msichana huyo asifunue kwamba yeye ni Myahudi; bila shaka Mordekai alijua kuwa mamlaka ya Waajemi iliwabagua watu wake. Lilikuwa jambo lenye kupendeza kama nini kwa Mordekai kujua kwamba ingawa Esta hukuwa karibu naye, bado aliendelea kuwa mwenye hekima na mtiifu!

Leo, vijana wanaweza pia kuwaletea wazazi na walezi wao furaha. Wanapokuwa mbali na wazazi wao—hata wanapozungukwa na watu wasio na busara, wenye maadili mapotovu, au wajeuri—wanaweza kukataa kushawishiwa kufanya mambo mabaya, na badala yake kufuata kanuni wanazojua zinafaa. Wanapofanya hivyo, kama Esta, wanafanya Baba yao wa mbinguni afurahi.—Methali 27:11.

Wakati ulipofika wa Esta kupelekwa kwa mfalme, alipewa nafasi ya kuchagua vitu ambavyo alifikiri angehitaji, labda vitu ambavyo angetumia kujirembesha zaidi. Hata hivyo, kwa kufuata shauri la Hegai, Esta alikuwa na kiasi na hakuomba kitu chochote zaidi ya vitu alivyopewa. (Esta 2:15) Yaelekea alijua kuwa urembo pekee haungeweza kufurahisha moyo wa mfalme; kiasi na unyenyekevu zilikuwa sifa muhimu mbele ya mfalme. Je, ni kweli?

Simulizi linajibu hivi: “Mfalme akampenda Esta kuliko wale wanawake wengine wote, hata akapata kibali na fadhili zenye upendo kuliko wale mabikira wengine wote. Ndipo mfalme akamvika taji la kifalme juu ya kichwa chake na kumfanya kuwa malkia badala ya Vashti.” (Esta 2:17) Haikuwa rahisi kwa msichana huyo mnyenyekevu Myahudi kubadili maisha yake—sasa alikuwa malkia mpya, mke wa mfalme mwenye nguvu zaidi duniani wakati huo! Je, cheo hicho kipya kingemfanya awe na kiburi?

Bila shaka, hapana! Esta aliendelea kumheshimu Mordekai, baba yake mlezi. Hakufunua kwamba yeye ni Myahudi. Zaidi ya hayo, Mordekai alipomweleza kuhusu njama ya kumuua Ahasuero, kwa utii Esta alimweleza mfalme, na watu waliopanga njama hiyo wakauawa. (Esta 2:20-23) Bado alionyesha imani yake kwa Mungu kwa kuwa mnyenyekevu na mtiifu. Leo, utii hauonekani kuwa sifa nzuri, badala yake uvunjaji wa sheria na uasi ndiyo mambo ya kawaida. Lakini watu walio na imani ya kweli wanathamini utii kama vile Esta.

Imani ya Esta Yajaribiwa

Mwanamume aliyeitwa Hamani alipewa cheo cha juu katika utawala wa Ahasuero. Mfalme alimchagua Hamani kuwa waziri mkuu, hivyo akawa mshauri wake mkuu na mtu wa pili kwa cheo katika milki yake. Hata mfalme aliagiza kwamba kila mtu amwinamie anapomwona. (Esta 3:1-4) Sheria hiyo ilitokeza tatizo kubwa kwa Mordekai. Alijua kwamba alipaswa kumtii mfalme, lakini hangefanya hivyo ikiwa jambo hilo lingemvunjia Mungu heshima. Ona kwamba Hamani alikuwa “Mwagagi.” Hilo linamaanisha kwamba alikuwa mzao wa Agagi, mfalme wa Waamaleki ambaye aliuawa na Samweli, nabii wa Mungu. (1 Samweli 15:33) Waamaleki walikuwa waovu sana na hivyo wakawa maadui wa Yehova na Waisraeli. Taifa la Waamaleki lilihukumiwa na Mungu. * (Kumbukumbu la Torati 25:19) Myahudi mwaminifu angewezaje kumwinamia Mwamaleki mwenye mamlaka? Mordekai hangefanya hivyo. Alisimama imara. Leo pia, wanaume na wanawake wenye imani wamehatarisha maisha yao kwa kutii kanuni hii: “Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”—Matendo 5:29.

Jambo hilo lilimkasirisha sana Hamani. Lakini hangetosheka kwa kumwangamiza Mordekai peke yake. Alitaka kuwaangamiza watu wote wa Mordekai! Hamani alizungumza na mfalme na kufanya Wayahudi waonekane kuwa watu wabaya. Bila kuwataja Wayahudi moja kwa moja, alisema wao si watu wa maana na kwamba “wa[me]tawanyika na kujitenga kati ya vikundi vya watu.” Hata alisema kwamba hawakuheshimu sheria za mfalme; hivyo, walikuwa waasi hatari. Kisha, akajitolea kuchanga kiasi kikubwa cha pesa kwa hazina ya mfalme ili kulipia kazi ya kuwaua Wayahudi wote katika milki hiyo. * Basi Ahasuero akampa Hamani pete yake ya kifalme ya mhuri ili atie mhuri amri yoyote aliyotaka itekelezwe.—Esta 3:5-10.

Muda mfupi baadaye, wajumbe walizunguka kwa farasi kila mahali katika milki hiyo kubwa wakitoa hukumu ya kifo kwa Wayahudi. Wazia jinsi tangazo hilo lilivyowaathiri mabaki ya Wayahudi waliokuwa mbali jijini Yerusalemu. Mabaki hao waliokuwa wamerudi kutoka uhamishoni Babiloni, walikuwa wakijitahidi kujenga upya jiji hilo ambalo halikuwa na kuta za kuwalinda. Huenda Mordekai aliposikia kuhusu habari hizo mbaya aliwafikiria Wayahudi hao waliokuwa Yerusalemu, rafiki zake, na watu wake wa ukoo waliokuwa Shushani. Akiwa amefadhaika alirarua mavazi yake, akavaa magunia, akajipaka majivu kwenye kichwa chake, na kulia kwa sauti ya juu katikati ya jiji. Hata hivyo, Hamani aliendelea kunywa pamoja na mfalme, bila kujali huzuni ambayo alikuwa amewasababishia Wayahudi na rafiki zao jijini Shushani.—Esta 3:12–4:1.

Mordekai alijua kwamba alipaswa kuchukua hatua fulani. Angefanya nini? Esta alisikia kuhusu mfadhaiko wake na akaagiza apelekewe mavazi, lakini Mordekai akakataa kufarijiwa. Labda alikuwa akijiuliza kwa nini Yehova, Mungu wake, aliruhusu Esta achukuliwe kutoka kwake na kuwa malkia wa mtawala mpagani. Sasa inaonekana alikuwa ameanza kuelewa sababu. Hivyo, Mordekai akatuma ujumbe kwa malkia, akimwomba Esta aingilie kati kwa kuzungumza na mfalme ili kuwatetea “watu wake mwenyewe.”—Esta 4:4-8.

Bila shaka, Esta aliingiwa na wasiwasi alipopata ujumbe huo. Lilikuwa jaribu kubwa sana la imani yake. Aliogopa na jambo hilo lilionekana wazi katika jibu lake kwa Mordekai. Esta alimkumbusha sheria ya mfalme. Ikiwa angeenda mbele ya mfalme bila kuitwa, angeuawa. Lakini mtu hangeuawa ikiwa mfalme angemnyooshea fimbo yake ya enzi ya dhahabu. Je, Esta alikuwa na sababu yoyote ya kutazamia kwamba hangeuawa, hasa akikumbuka kilichompata Vashti alipokataa kwenda mbele ya mfalme alipoagizwa kufanya hivyo? Alimwambia Mordekai kwamba mfalme hakuwa amemwita kwenda mbele yake kwa siku 30! Kwa sababu hakuwa ameitwa kwa siku nyingi, Esta hakujua ikiwa alikuwa amepoteza kibali cha mfalme ambaye hisia zake zilibadilika-badilika. *Esta 4:9-11.

Mordekai alimjibu Esta kwa uhakika ili kuimarisha imani yake. Alimhakikishia kwamba ikiwa hangechukua hatua, wokovu wa Wayahudi ungetoka katika chanzo kingine. Lakini angewezaje kutazamia kuepuka kifo wakati ambapo Wayahudi wangeanza kuuawa? Mordekai alionyesha imani yake yenye nguvu kwa Yehova, ambaye hangeacha kamwe watu wake waangamizwe na ahadi zake zikose kutimizwa. (Yoshua 23:14) Kisha, Mordekai akamuuliza Esta: “Ni nani anayejua ikiwa si kwa ajili ya wakati kama huu kwamba umefikia heshima ya kifalme?” (Esta 4:12-14) Mordekai alimtegemea kabisa Yehova, Mungu wake. Je, sisi tunafanya hivyo?—Methali 3:5, 6.

Imani Yenye Nguvu Yafanya Asiogope Kifo

Sasa Esta alipaswa kufanya uamuzi. Alimwomba Mordekai awaambie Wayahudi wenzake waungane naye katika kufunga kwa siku tatu, na akamalizia ujumbe wake kwa maneno ambayo kwa muda mrefu yameonyesha imani na ujasiri: “Nikiangamia, na niangamie.” (Esta 4:15-17) Bila shaka, alisali kwa bidii sana katika siku hizo tatu kuliko wakati mwingine wowote maishani mwake. Mwishowe, wakati ukafika. Esta alijipamba na kuvalia mavazi bora ya kifalme ili avutie mbele ya mfalme. Kisha, akaingia mbele yake.

Kama ilivyoelezwa mwanzoni mwa makala hii, Esta aliingia katika ua wa mfalme. Tunaweza tu kuwazia jinsi alivyohangaika akilini na moyoni na jinsi alivyosali kwa bidii. Aliingia ndani ya ua, mahali ambapo angeweza kumwona Ahasuero akiwa ameketi kwenye kiti chake cha ufalme. Labda aliutazama uso wa mfalme ili ajaribu kutambua hisia zake. Ikiwa Esta alihitaji kungoja kwa muda fulani, lazima alihisi kana kwamba amengoja kwa muda mrefu sana. Lakini muda huo ulipita na mume wake akamwona. Kwa kweli, alishangaa lakini akatulia. Kisha, akamnyooshea fimbo yake ya enzi ya dhahabu!—Esta 5:1, 2.

Esta alikuwa amefaulu kuzungumza na mfalme. Alikuwa ameamua kumtetea Mungu wake na watu wake, akiwawekea mfano mzuri watumishi wote waaminifu wa Mungu. Lakini huo ulikuwa tu mwanzo wa kazi yake. Angeweza kumshawishi mfalme jinsi gani aamini kwamba Hamani, mshauri wake aliyempenda, alikuwa amepanga njama mbaya? Angefanya nini ili asaidie kuwaokoa watu wake? Tutachunguza maswali hayo katika makala ya baadaye.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Watu wengi wanadhani kwamba Ahasuero alikuwa Shasta wa Kwanza, ambaye alitawala Milki ya Uajemi mwanzoni mwa karne ya tano K.W.K.

^ fu. 24 Yaelekea Hamani alikuwa mmoja wa wazao wa mwisho-mwisho wa Waamaleki, kwa sababu wale ‘waliobaki’ waliangamizwa katika siku za Mfalme Hezekia.—1 Mambo ya Nyakati 4:43.

^ fu. 25 Hamani alitoa mchango wa talanta 10,000 za fedha, kiasi ambacho leo ni sawa na mamilioni ya dola. Ikiwa Ahasuero alikuwa Shasta wa Kwanza, basi huenda pesa hizo zilimchochea akubali pendekezo la Hamani. Shasta alikuwa ametumia pesa nyingi sana alipopigana na Wagiriki katika vita vilivyosababisha uharibifu mkubwa. Labda alipigana vita hivyo kabla ya kumwoa Esta.

^ fu. 28 Shasta wa Kwanza alikuwa na hisia zilizobadilika-badilika na hasira yenye jeuri. Herodoto, mwanahistoria Mgiriki, aliandika mambo fulani ambayo Shasta alifanya wakati wa vita vyake na Wagiriki yanayoonyesha hisia za mfalme huyo. Mfalme aliagiza daraja la muda la meli zilizounganishwa lijengwe ili kuvuka mlango wa bahari wa Hellespont. Dhoruba ilipofagilia mbali daraja hilo, Shasta aliagiza mafundi wake wakatwe vichwa na watu wake “waadhibu” Hellespont kwa kupiga maji huku ujumbe wa matusi ukisomwa kwa sauti kubwa. Pindi hiyo, mwanamume fulani tajiri alipoomba mwana wake asiandikishwe jeshini, Shasta aliagiza kijana huyo akatwe vipande viwili na mwili wake uwekwe mahali palipo wazi ili kuwa onyo kwa wengine.

[Picha katika ukurasa wa 19]

Mordekai alikuwa na sababu nzuri ya kujivunia kuwa baba mlezi wa Esta

[Picha katika ukurasa wa 20]

Esta alijua kwamba sifa ya unyenyekevu na hekima ni muhimu zaidi kuliko urembo

[Picha katika ukurasa wa 22, 23]

Esta alihatarisha uhai wake ili awalinde watu wa Mungu