Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Uishi Kupatana na Viwango vya Biblia?

Kwa Nini Uishi Kupatana na Viwango vya Biblia?

Kwa Nini Uishi Kupatana na Viwango vya Biblia?

JE, MAMBO ambayo Biblia inasema kuhusu ngono yamepitwa na wakati na yanatunyima uhuru kupita kiasi? Hapana. Badala yake, mambo ambayo Biblia inasema kuhusu ngono yanaweza kutusaidia kuepuka mambo yafuatayo:

Magonjwa yanayopitishwa kingono

Kupata mimba nje ya ndoa

Matokeo yenye uchungu yanayosababishwa na kuvunjika kwa ndoa

Kusumbuliwa na dhamiri

Kutojiheshimu kwa sababu unahisi kwamba umetumiwa vibaya na wengine

Muumba wetu, Yehova Mungu, * anataka tufurahie na tufaidike na zawadi anazotupa. Mungu ndiye “anayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe.” (Isaya 48:17) Mtu anayeishi kupatana na miongozo ya Biblia kuhusu ngono anapata faida zifuatazo:

Kukubaliwa na Mungu

Kuwa na amani ya akili

Kuwa na uhusiano wenye nguvu katika familia yake

Kujulikana kuwa mtu mwenye tabia nzuri

Kujiheshimu

Hata hivyo, namna gani ikiwa kwa sasa huishi kupatana na viwango vya Biblia kuhusu maadili? Je, inawezekana ubadili maisha yako? Je, Mungu ataendelea kukumbuka mambo uliyofanya zamani?

Fikiria hili: Watu fulani waliokuwa katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza, zamani walikuwa waasherati, wazinzi, na hata wengine walifanya ngono na watu wa jinsia moja. Waliamua kubadili maisha yao na wakafaidika sana. (1 Wakorintho 6:9-11) Leo, maelfu ya watu ulimwenguni pote wamefanya uamuzi kama huo. Wameacha maisha yaliyopotoka kiadili na wamefaidika kwa sababu ya kuishi kulingana na viwango vya Biblia. Kwa mfano, fikiria kisa cha Sarah, aliyetajwa kwenye makala ya kwanza.

“Mara Moja, Nikapata Kitulizo”

Sarah aligundua kwamba alipoishi bila kufuata viwango vyovyote hakupata uhuru na uradhi ambao alitamani. “Nilihisi kwamba dhamiri yangu ilikuwa imekufa ganzi,” anasema. “Niliaibika na kuwa na wasiwasi kwamba ningepata mimba au kuambukizwa ugonjwa mbaya. Sikuwahi kusahau kamwe kwamba kuna Mungu na nilijua kuwa maisha yangu yalimfanya ahisi uchungu moyoni. Nilijiona kuwa mchafu na jambo hilo liliniumiza sana kihisia.”

Mwishowe, Sarah alipata nguvu za kubadili maisha yake. Alitafuta msaada kutoka kwa wazazi wake ambao ni Mashahidi wa Yehova. Pia, aliomba msaada kutoka kwa wazee Wakristo wa kutaniko la kwao. “Nilishangazwa sana na jinsi wazazi wangu na wazee wa kutaniko walivyonitendea kwa fadhili na kwa upendo,” anasema Sarah. “Mara moja, nikapata kitulizo.”

Sasa Sarah analea watoto wake wawili. Anasema hivi: “Mimi huwaeleza watoto wangu waziwazi kuhusu maamuzi niliyofanya. Ninataka waelewe jinsi kupuuza viwango vya Mungu kulivyoniathiri. Lengo langu ni kuwasaidia waone kwamba tunafaidika kimwili, kiakili, na kihisia tunapoishi kulingana na viwango vya Mungu kuhusu ngono. Nina hakika kwamba Mungu anatuwekea viwango vya maadili kwa sababu hataki tuumie.”

Wewe pia unaweza kufaidika kwa kufuata mwongozo wenye upendo wa Mungu. Biblia inatoa ahadi hii: “Maagizo kutoka kwa Yehova ni manyoofu, huufanya moyo ushangilie; amri ya Yehova ni safi, huyafanya macho yang’ae. . . . Katika kuyashika kuna thawabu kubwa.”—Zaburi 19:8, 11. *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu kama inavyofunuliwa katika Biblia.

^ fu. 20 Ili ujifunze mengi zaidi kuhusu mashauri ya Biblia yenye faida, wasialiana na Mashahidi wa Yehova walio katika eneo lenu. Au unaweza kuandika barua ukitumia anwani inayofaa kwenye ukurasa wa 4 au utembelee Tovuti yetu ya www.watchtower.org.

[Blabu katika ukurasa wa 8]

Mara nyingi watu wanaopuuza viwango vya Biblia huumiza wengine kihisia

[Blabu katika ukurasa wa 9]

Watu wanaoishi kupatana na viwango vya Biblia wanakuwa na dhamiri safi na wanakuwa na uhusiano wenye nguvu katika familia zao