Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Abrahamu Alikuwa Nani?

Abrahamu Alikuwa Nani?

Abrahamu Alikuwa Nani?

NI WATU wachache ambao wamekuwa na uvutano mkubwa juu ya dini za ulimwengu kama Abrahamu. * Anaheshimiwa sana na Wayahudi, Waislamu, na Wakristo na ametajwa kuwa “mtu muhimu zaidi katika Maandiko” na kwamba “aliweka mfano mzuri sana wa imani yenye nguvu.” Biblia inamwita “baba ya wale wote walio na imani.”—Waroma 4:11.

Kwa nini Abrahamu anaheshimiwa sana hivyo? Sababu moja ni kwamba Abrahamu ndiye mtu pekee ambaye Biblia inamtaja moja kwa moja kuwa rafiki ya Mungu.—Isaya 41:8; Yakobo 2:23.

Hata hivyo, katika mambo mengine, Abrahamu alikuwa mtu wa kawaida kama sisi tu. Alipambana na mengi ya matatizo ambayo tunakabili leo na akayashinda. Je, ungependa kujua jinsi alivyofanya hivyo? Fikiria yale ambayo Biblia inasema kumhusu mwanamume huyu wa kipekee.

Malezi Yake

Abrahamu alizaliwa mwaka wa 2018 K.W.K. na alilelewa jijini Uru. (Mwanzo 11:27-31) Jiji la Uru lilikuwa kubwa na lenye ufanisi na ibada ya sanamu ilikuwa imeenea sana humo. Huenda Tera, baba ya Abrahamu, alikuwa miongoni mwa wale walioabudu sanamu mbalimbali. (Yoshua 24:2) Hata hivyo, Abrahamu aliamua kumwabudu Yehova * pekee badala ya kuabudu sanamu zisizo na uhai.

Ni nini kilichomsukuma Abrahamu kufanya uamuzi huo? Abrahamu alizaliwa miaka 150 kabla ya kifo cha Shemu, mwana wa Noa. Ikiwa alishirikiana na mwanamume huyo mzee, huenda ushirika huo ulikuwa na matokeo gani juu yake? Inawezekana Abrahamu alijifunza moja kwa moja kutoka kwa Shemu jinsi yeye na familia yake walivyookoka Gharika iliyoikumba dunia yote. Pia, huenda alijifunza umuhimu wa kumwabudu Yehova, Mungu aliyemwokoa Shemu na familia yake wakati wa Gharika hiyo.

Iwe alijifunza kutoka kwa Shemu au kupitia njia nyingine, Abrahamu aliitikia vizuri mambo aliyojifunza kumhusu Mungu wa kweli. Wakati Yehova, “mchunguzaji wa mioyo,” alipomchunguza Abrahamu, aliona sifa fulani nzuri ndani yake, hivyo akamsaidia kusitawisha sifa hizo.—Methali 17:3; 2 Mambo ya Nyakati 16:9.

Maisha Yake

Ingawa mara nyingi alikabili changamoto mbalimbali, Abrahamu aliishi maisha yenye furaha, yenye kuridhisha, na yenye kusudi. Fikiria mambo machache yaliyompata.

Abrahamu alipokuwa akiishi Uru, Mungu alimwagiza aondoke katika eneo hilo na kwenda katika nchi ambayo Yeye angemwonyesha. Ingawa Abrahamu na Sara hawakujua mambo yote yaliyohusika—kule ambako wangeenda au kwa nini Mungu alikuwa akiwaagiza waondoke—bado walitii. Hatimaye Abrahamu na Sara walienda kuishi kwenye mahema katika nchi ya Kanaani na wakawa wakaaji wa muda kwa maisha yao yote.—Matendo 7:2, 3; Waebrania 11:8, 9, 13.

Ingawa Abrahamu na Sara hawakuwa na mtoto, Yehova aliahidi kufanyiza taifa kubwa kutoka kwa Abrahamu. Yehova aliongeza kusema kwamba familia zote za dunia zingejibariki kupitia Abrahamu. (Mwanzo 11:30; 12:1-3) Baadaye, Yehova alimhakikishia Abrahamu tena kuwa angetimiza ahadi hiyo. Alimwambia kwamba uzao wake ungeongezeka na kuwa kama nyota za angani.—Mwanzo 15:5, 6.

Abrahamu alipokuwa na umri wa miaka 99 na Sara miaka 90 hivi, Yehova aliwaahidi kwamba wangepata mwana. Kwa maoni ya mwanadamu, hilo lilikuwa jambo lisilowezekana, lakini punde si punde Abrahamu na Sara wakajifunza kwamba hakuna jambo ambalo ni “kubwa mno isivyo kawaida kwa Yehova.” (Mwanzo 18:14) Mwaka mmoja baadaye, akiwa na umri wa miaka 100, Abrahamu alipata mwana aliyemwita Isaka. (Mwanzo 17:21; 21:1-5) Mungu alitaja kihususa kwamba kupitia Isaka, wanadamu wangepata baraka nyingi.

Miaka kadhaa baadaye, Yehova alimwambia Abrahamu afanye jambo lisilo la kawaida kabisa: Alimwambia amdhabihu mwana wake mpendwa, Isaka, ijapokuwa Isaka hakuwa na mke wala watoto. * Ingawa huenda wazo la kumpoteza mwana wake lilimuumiza sana, Abrahamu aliamua kutii na kumdhabihu Isaka. Abrahamu aliamini kabisa kwamba Mungu alikuwa na uwezo wa kumfufua Isaka, ikihitajika, ili atimize ahadi Zake. (Waebrania 11:19) Wakati Abrahamu alipokuwa tu karibu kumdhabihu mwana wake, Mungu aliingilia kati na kumwokoa Isaka. Alimpongeza Abrahamu kwa utii wake usio na kifani. Kisha, akarudia tena ahadi zake kwa Abrahamu.—Mwanzo 22:1-18.

Baada ya kuishi miaka 175, Abrahamu alilala katika kifo. ‘Alikufa katika umri mwema wa uzee,’ inasema Biblia, na kuongeza kwamba ‘alikuwa mzee na mwenye kutosheka.’ (Mwanzo 25:7, 8) Hivyo, Abrahamu aliona utimizo wa ahadi nyingine iliyotolewa na Mungu, yaani, angefurahia maisha marefu kabla ya kufa kwa amani.—Mwanzo 15:15.

Mfano Mzuri wa Abrahamu

Abrahamu si mtu tu wa dini au wa kihistoria aliyeishi zamani za kale. Hata leo, mfano wake bado unakumbukwa, na ni muhimu sana kwetu. (Waebrania 11:8-10, 17-19) Acheni tufikirie nne kati ya sifa nyingi nzuri ambazo Abrahamu alionyesha. Tutaanza na sifa ambayo labda ndiyo inayojulikana zaidi—imani.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Mwanzoni, Abrahamu aliitwa Abramu naye mke wake aliitwa Sarai. Baadaye, Mungu alibadili jina la Abramu kuwa Abrahamu, linalomaanisha “Baba ya Umati” na pia akabadili jina la Sarai kuwa Sara, linalomaanisha “Binti ya Mfalme.” (Mwanzo 17:5, 15) Ili kurahisisha mambo katika mfululizo huu, tutatumia majina Abrahamu na Sara.

^ fu. 6 Katika Biblia, jina la kibinafsi la Mungu ni Yehova.

[Sanduku katika ukurasa wa 4]

Mtu Muhimu Sana Katika Historia ya Biblia

Katika sura za kwanza kumi za kitabu cha Biblia cha Mwanzo, kuna masimulizi kuhusu maisha ya wanaume kadhaa wenye imani, kutia ndani Abeli, Enoko, na Noa. Hata hivyo, sehemu kubwa ya sura 15 zinazofuata, inazungumzia maisha ya mwanamume mmoja—Abrahamu.

Isitoshe, Biblia inapozungumzia Abrahamu, inataja kwa mara ya kwanza baadhi ya mafundisho muhimu zaidi. Kwa mfano, katika masimulizi kuhusu maisha yake tunapata . . .

maelezo ya kwanza yanayomrejelea Mungu kuwa Ngao ya, au Mlinzi wa, watumishi wake.—Mwanzo 15:1; ona Kumbukumbu la Torati 33:29; Zaburi 115:9; Methali 30:5.

maneno kuwa na imani katika Mungu yametajwa kwa mara ya kwanza.—Mwanzo 15:6.

neno nabii limetumiwa kwa mara ya kwanza.—Mwanzo 20:7.

▪ upendo wa mzazi unatajwa kwa mara ya kwanza.—Mwanzo 22:2.