Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Abrahamu—Mwanamume Jasiri

Abrahamu—Mwanamume Jasiri

Abrahamu​—Mwanamume Jasiri

Abrahamu anatazama familia yake na watumishi wake wanapojitayarisha kuondoka kwenda Kanaani. (Mwanzo 12:1-5) Anapotazama kikundi hicho kikubwa cha watu ambao wanamtegemea ili kupata riziki yao, Abrahamu anaelewa vizuri jukumu lake kuwaelekea. Atawaandaliaje mahitaji yao watakapokuwa katika nchi ya kigeni? Je, haingekuwa rahisi kufanya hivyo wakiwa huko Uru, eneo lenye ufanisi na sehemu kubwa za malisho, udongo wenye rutuba, na maji mengi? Itakuwaje akipatwa na ugonjwa au kufa katika nchi hiyo? Ni nani atakayeitunza familia yake? Ikiwa Abrahamu ana mahangaiko kama hayo, haachi yamzuie kutenda. Ameazimia kutenda, na kutii amri za Mungu—hata iweje—na hiyo ni ishara ya ujasiri wa kweli.

UJASIRI NI NINI? Ni sifa ya kuwa hodari, shujaa, na mwenye nguvu—kinyume cha kuwa mwenye wasiwasi au woga. Kuwa jasiri hakumaanishi kwamba hatuogopi kamwe. Badala yake, mtu mwenye ujasiri unaotoka kwa Mungu huchukua hatua licha ya kuwa na woga.

ABRAHAMU ALIONYESHAJE UJASIRI? Abrahamu hakuogopa kutenda tofauti na watu wengine. Abrahamu alilelewa katika eneo ambalo watu waliabudu miungu na sanamu nyingi. Hata hivyo, hakusita kutenda yale aliyojua kuwa sawa akiogopa jinsi ambavyo watu wangefikiri. Badala yake, kwa ujasiri Abrahamu aliamua kutenda tofauti kwa kuchagua kumwabudu Mungu mmoja tu—“Mungu Aliye Juu Zaidi,” Yehova.—Mwanzo 14:21, 22.

Abrahamu alitanguliza ibada yake kwa Mungu wa kweli, bali si vitu vya kimwili. Alikuwa tayari kuacha maisha yake ya starehe jijini Uru na kwenda nyikani, akiamini kabisa kwamba Yehova angemwandalia mahitaji yake. Kwa kweli, miaka ilipoendelea kusonga, huenda Abrahamu alifikiria starehe fulani alizofurahia jijini Uru. Lakini Abrahamu alikuwa na hakika kwamba Yehova angemwandalia mahitaji yake pamoja na ya familia yake. Kwa kushikamana na Yehova ambaye alimwona kuwa Mtu aliye muhimu zaidi maishani mwake, Abrahamu alipata ujasiri wa kutii amri Zake.

TUNAJIFUNZA NINI? Tunaweza kumwiga Abrahamu kwa kusitawisha ujasiri wa kumtii Yehova, hata ikiwa wengine hawafanyi hivyo. Kwa mfano, Biblia inafundisha kwamba huenda wale wanaotetea imani yao katika Yehova Mungu wakapingwa, labda na marafiki au watu wa ukoo wasio na nia mbaya. (Yohana 15:20) Hata hivyo, ikiwa tunaamini yale tunayojifunza kumhusu Yehova, tunatetea imani yetu kwa heshima.—1 Petro 3:15.

Pia, tunaweza kuamini ahadi ya Mungu kwamba atatimiza mahitaji ya wale wanaomwamini. Imani hiyo inatupa ujasiri wa kuzingatia mambo ya kiroho maishani mwetu badala ya kufuatilia vitu vya kimwili. (Mathayo 6:33) Ona jinsi ambavyo familia moja imefanya hivyo.

Ingawa Doug na Becky wana wavulana wawili wadogo, walitaka kuhamia nchi ambayo ina uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa habari njema za Biblia. Baada ya kufanya utafiti kwa makini na kusali kwa bidii, waliamua kusonga mbele na mipango yao. “Ilihitaji ujasiri kuwatayarisha watoto wetu ili kuhama, bila kujua jinsi hali zitakavyokuwa,” anasema Doug. “Lakini mapema tulipokuwa tukifanya uamuzi wetu, tulizungumzia mfano wa Abrahamu na Sara. Kufikiria jinsi walivyomwamini Yehova na jinsi alivyowategemeza sikuzote, kulitusaidia sana.”

Doug anasema hivi kuhusu maisha yao katika nchi ya kigeni: “Tumebarikiwa sana.” Anaendelea kusema: “Kwa sababu tumerahisisha maisha yetu, tunatumia muda mrefu pamoja—tukihubiri, kucheza na watoto wetu, na kuzungumza pamoja tukiwa familia. Tunahisi tuna uhuru usioweza kuelezeka.”

Bila shaka, si kila mtu anayeweza kufanya mabadiliko makubwa kama hayo. Hata hivyo, sote tunaweza kuiga mfano wa Abrahamu kwa kutanguliza ibada yetu kwa Mungu, tukiamini kwamba atatutegemeza. Tunapofanya hivyo, tunatii himizo la Biblia la ‘kuwa hodari na kusema: “Yehova ni msaidizi wangu; sitaogopa.”’—Waebrania 13:5, 6.

[Blabu katika ukurasa wa 7]

Mtu mwenye ujasiri unaotoka kwa Mungu huchukua hatua licha ya kuwa na woga

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8]

Mwanamke Mcha Mungu na Mke Bora

Sara alikuwa ameolewa na mwanamume mwenye imani isiyo na kifani. Lakini mwanamke huyu mcha Mungu pia aliweka mfano bora. Hata Biblia inamtaja kwa jina mara tatu kuwa mwanamke ambaye mfano wake unapaswa kuigwa na wanawake wanaomcha Mungu. (Isaya 51:1, 2; Waebrania 11:11; 1 Petro 3:3-6) Ingawa Biblia haisemi mengi kumhusu mwanamke huyu wa kipekee, bado tunaweza kuona kwamba Sara alikuwa na sifa nzuri.

Kwa mfano, fikiria jinsi Sara alivyoitikia wakati Abrahamu alipomweleza kuhusu agizo la Mungu la kuondoka Uru. Je, alishangaa walikuwa wakienda wapi na kwa sababu gani? Je, alihangaikia mahitaji yao ya kimwili? Je, alihuzunika kujua kwamba atawaacha marafiki na watu wa familia yao, bila kujua wakati ambapo atawaona tena—ikiwa atawahi kuwaona? Bila shaka, Sara alifikiria mambo hayo. Hata hivyo, aliondoka bila kulazimishwa, akiamini kwamba Yehova angembariki kwa sababu ya utii wake.—Matendo 7:2, 3.

Mbali na kuwa mtumishi mtiifu wa Mungu, Sara alikuwa mke bora. Badala ya kushindana na mume wake kuhusu kuongoza mambo katika familia yao, Sara alisitawisha heshima ya kutoka moyoni kuelekea mume wake, akimuunga mkono kwa upendo alipoiongoza familia yao. Kwa kufanya hivyo, alijipamba, yaani, alijirembesha kwa kuwa na sifa nzuri.—1 Petro 3:1-6.

Je, sifa kama hizo zinaweza kuwanufaisha wake leo? “Mfano wa Sara umenifundisha kwamba ninapaswa kujihisi huru kuzungumza na kumweleza mume wangu maoni niliyo nayo,” anasema mwanamke aitwaye Jill, ambaye aliolewa miaka 30 iliyopita. “Wakati huohuo,” anaendelea kusema, “mume wangu ndiye aliye na jukumu la kufanya uamuzi wa mwisho kwa kuwa yeye ndiye kichwa cha familia. Baada ya mume wangu kuamua, nina daraka la kufanya yote niwezayo kuhakikisha kwamba uamuzi huo umefaulu.”

Labda jambo lenye kugusa moyo zaidi tunalojifunza kutoka kwa Sara ni hili: Ingawa alikuwa mrembo sana, Sara hakuruhusu urembo wake umchochee kuwa na kiburi. (Mwanzo 12:10-13) Badala yake, alimuunga mkono Abrahamu kwa unyenyekevu katika panda-shuka za maisha yao pamoja. Hapana shaka kwamba Abrahamu na Sara walikuwa waaminifu, wanyenyekevu, na wenye upendo—mume na mke ambao maisha yao yaliwaletea baraka kwelikweli.