Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Abrahamu—Mwanamume Mwenye Imani

Abrahamu—Mwanamume Mwenye Imani

Abrahamu​—Mwanamume Mwenye Imani

Abrahamu anasimama nje katika usiku mtulivu. Anapotazama anga jangavu, lenye nyota, hana budi kufikiria ahadi ya Mungu kwamba uzao wake ungeongezeka na kuwa kama nyota hizo. (Mwanzo 15:5) Abrahamu anaona nyota hizo kuwa kikumbusho kinachoonekana cha ahadi ya Yehova. Pia, anaziona kuwa uhakikisho. Ikiwa Yehova ana uwezo wa kuumba ulimwengu huu mkubwa sana na vyote vilivyomo, je, anaweza kushindwa kufanya Abrahamu na Sara wapate mtoto? Abrahamu alikuwa na imani kwelikweli.

IMANI NI NINI? Neno “imani,” kama linavyotumiwa katika Biblia, linamaanisha kusadiki jambo kabisa ingawa halionekani. Usadikisho huo unategemea uthibitisho ulio hakika. Mtu mwenye imani hukazia fikira kutimizwa kwa ahadi za Yehova, akiwa na uhakika kwamba ahadi hizo ni kana kwamba tayari zimetimia.

ABRAHAMU ALIONYESHAJE IMANI? Abrahamu alionyesha kwamba aliamini ahadi za Mungu. Kwa imani, Abrahamu aliondoka katika nchi alimozaliwa, akiwa na uhakika kwamba Yehova angetimiza ahadi Yake ya kumwonyesha nchi nyingine. Kwa imani, Abrahamu alitangatanga katika nchi ya Kanaani, akiwa na uhakika kwamba hatimaye uzao wake ungemiliki nchi hiyo. Na kwa imani, Abrahamu alimtii Mungu na kujaribu kumdhabihu Isaka, akiwa na uhakika kuwa, ikihitajika, Yehova angemfufua Isaka.—Waebrania 11:8, 9, 17-19.

Abrahamu alizingatia wakati ujao bali si wakati uliopita. Ingawa huenda Abrahamu na Sara walifurahia maisha yenye starehe jijini Uru tofauti na ilivyokuwa nchini Kanaani, “hawakuendelea kufikiria nchi waliyoacha.” (Waebrania 11:15, Today’s English Version) Badala yake, walizingatia jinsi ambavyo Mungu angewabariki na pia kubariki uzao wao wakati ujao.—Waebrania 11:16.

Je, imani ya Abrahamu ilikuwa na msingi imara? Bila shaka. Yehova alitimiza kila mojawapo ya ahadi zake. Hatimaye, uzao wa Abrahamu uliongezeka na kuwa taifa lililoitwa Israeli. Baadaye, Waisraeli walikuja kuishi katika nchi ya Kanaani, ile nchi ambayo Yehova alikuwa amemwahidi Abrahamu.—Yoshua 11:23.

TUNAJIFUNZA NINI? Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatimiza ahadi zake. Ingawa kwa maoni ya binadamu huenda baadhi ya ahadi hizo zikaonekana kuwa haziwezi kutimia, tunaamini kuwa “kwa Mungu mambo yote yanawezekana.”—Mathayo 19:26.

Pia, mfano wa Abrahamu unatufundisha kuzingatia baraka tutakazofurahia wakati ujao, bali si jinsi mambo yalivyokuwa wakati uliopita. Hivyo ndivyo mwanamume anayeitwa Jason anavyofanya. Jason ana ugonjwa wenye kudhoofisha ambao umemlemaza kabisa. “Ninakubali kwamba kuna nyakati ambapo ninajikuta nikifikiria wakati uliopita,” anasema Jason. Kisha, anaongeza kusema: “Ninatamani zaidi mambo madogo-madogo kama vile kumkumbatia mke wangu Amanda.”

Hata hivyo, Jason ana imani thabiti kwamba Yehova atatimiza ahadi zake, kutia ndani ahadi ya kwamba hivi karibuni dunia yetu itakuwa paradiso na kwamba wanadamu waaminifu watafurahia uzima wa milele wakiwa na afya kamili. * (Zaburi 37:10, 11, 29; Isaya 35:5, 6; Ufunuo 21:3, 4) “Mimi hujikumbusha kwamba wakati ujao tutafurahia hali nzuri kabisa,” anasema Jason na kueleza: “Hivi karibuni, mambo kama vile mfadhaiko, wasiwasi, huzuni, kuhisi kuwa na hatia yatatoweka milele.” Bila shaka, huo ni mfano mzuri sana wa imani, sawa na ile ya Abrahamu!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Ili kujifunza mengi zaidi kuhusu paradiso itakayokuwa duniani, ona sura ya  3, 7, na 8 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.