Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Igeni Imani Yao

Alitenda kwa Hekima, Ujasiri, na Bila Ubinafsi

Alitenda kwa Hekima, Ujasiri, na Bila Ubinafsi

ESTA alitembea polepole kuelekea kwenye kiti cha mfalme, huku moyo wake ukidunda kwa kasi. Wazia kimya kilichotanda katika jumba la mfalme wa Uajemi huko Shushani, kimya kikubwa hivi kwamba Esta angesikia nyayo za miguu yake na sauti ya mavazi yake alipokuwa akitembea. Hangeruhusu akengeushwe na makao ya kifahari ya mfalme, nguzo zilizopambwa, dari lenye michongo mingi lililotengenezwa kwa mierezi iliyoletwa kutoka nchi ya mbali ya Lebanoni. Alimwelekezea fikira mwanamume aliyeketi kwenye kiti cha ufalme, mwanamume ambaye angeamua ikiwa Esta angeendelea kuishi au la.

Mfalme alimtazama Esta kwa makini alipomkaribia, kisha akamnyooshea fimbo yake ya enzi ya dhahabu. Lilikuwa jambo rahisi, lakini liliokoa uhai wa Esta, kwa maana kwa kufanya hivyo mfalme alimsamehe Esta kosa ambalo alikuwa amefanya—kosa la kwenda mbele ya mfalme bila kualikwa. Alipokaribia kiti cha mfalme, Esta alinyoosha mkono wake na kugusa kwa shukrani ncha ya ile fimbo.—Esta 5:1, 2. *

Kila kitu kumhusu Mfalme Ahasuero kilionyesha kwamba alikuwa mfalme tajiri mwenye mamlaka kubwa. Inaaminiwa kwamba mavazi ya wafalme wa Uajemi wa nyakati hizo yalikuwa na thamani inayolingana na mamia ya mamilioni ya dola. Ingawa hivyo, Esta aliona uchangamfu fulani katika macho ya mume wake; mume wake alimpenda kwa njia fulani. Alisema: “Una nini, Ee Esta, malkia, na ombi lako ni nini? Hata nusu ya ufalme—na upewe wewe!”—Esta 5:3.

Tayari Esta alikuwa ameonyesha imani na ujasiri mwingi; alienda mbele ya mfalme ili kuwalinda watu wake kutokana na njama ya kuwaangamiza wote. Kufikia sasa, alikuwa amefaulu, lakini angekabili hali ngumu zaidi baadaye. Alipaswa kumsadikisha mtawala huyo mwenye kiburi kwamba mshauri wake aliyemwamini zaidi ni mtu mwovu ambaye alikuwa amemdanganya aagize watu wa Esta wauawe. Angemsadikishaje? Na tunaweza kujifunza nini kutokana na imani yake?

Alichagua kwa Hekima “Wakati wa Kusema”

Je, Esta angemfunulia mfalme tatizo lake mbele ya wafanyakazi wa makao ya mfalme? Kama angefanya hivyo angemfedhehesha mfalme na kumpa mshauri wake Hamani wakati wa kupinga au hata kupunguza uzito wa mashtaka yake. Kwa hiyo, Esta alifanya nini? Karne nyingi mapema, Mfalme Sulemani mwenye hekima aliongozwa na roho ya Mungu kuandika: “Kuna wakati uliowekwa wa kila kitu, . . . wakati wa kukaa kimya na wakati wa kusema.” (Mhubiri 3:1, 7) Tunaweza kumwazia Mordekai, baba mlezi wa Esta ambaye alikuwa mwanamume mwaminifu, akimfundisha mwanamke huyo mchanga kanuni hizo alipokuwa akikua chini ya utunzaji wake. Bila shaka, Esta alielewa umuhimu wa kuchagua kwa makini “wakati wa kusema.”

Esta alisema: “Mfalme akiona vema, mfalme na aje leo pamoja na Hamani kwenye karamu ambayo nimemwandalia.” (Esta 5:4) Mfalme alikubali na akaagiza Hamani aitwe. Je, unaona jinsi Esta alivyozungumza kwa hekima? Hakumvunjia heshima mume wake, badala yake aliandaa kikao kinachofaa zaidi ili kumfunulia mahangaiko yake.

Haikosi Esta alitayarisha karamu hiyo kwa makini, akihakikisha kwamba kila jambo lingempendeza mume wake. Karamu hiyo ilitia ndani divai nzuri ili wawe wenye furaha. (Zaburi 104:15) Ahasuero alifurahia karamu hiyo, na akachochewa kumuuliza Esta tena amweleze ombi lake. Je, huo ndio uliokuwa wakati wa kuzungumza?

Esta hakufikiri hivyo. Badala yake, alimkaribisha mfalme na Hamani kwenye karamu nyingine, siku iliyofuata. (Esta 5:7, 8) Kwa nini alikawia? Kumbuka, watu wote wa Esta walikabili kifo kutokana na agizo la mfalme. Kwa sababu ya hatari hiyo kubwa, Esta alipaswa kuhakikisha kwamba alizungumza wakati uliofaa. Kwa hiyo alingoja, akiandaa nafasi nyingine ya kumwonyesha mume wake jinsi alivyomheshimu sana na jinsi alivyotamani kumfurahisha.

Subira ni sifa yenye thamani ambayo watu wengi hawana. Ingawa jambo hilo lilimhangaisha na alitaka sana kusema yaliyokuwa moyoni mwake, Esta alisubiri wakati unaofaa. Mfano wake unaweza kutufunza mengi, kwa sababu inaelekea sote tumeona makosa fulani yanayohitaji kurekebishwa. Ikiwa tunataka kumsadikisha mtu mwenye mamlaka ashughulikie tatizo fulani, huenda tukahitaji kumwiga Esta na kuwa na subira. Andiko la Methali 25:15 linasema: “Kwa subira kiongozi hushawishiwa, na ulimi wa upole unaweza kuvunja mfupa.” Tukingoja kwa subira wakati unaofaa, kisha tuzungumze kwa upole, kama alivyofanya Esta, tunaweza hata kuvunja upinzani ulio mgumu kama mfupa. Je, Yehova, Mungu wa Esta alibariki subira na hekima yake?

Subira Yatokeza Haki

Subira ya Esta iliongoza kwenye matukio makubwa yaliyofuatana. Hamani aliondoka kwenye karamu ya kwanza akiwa mchangamfu sana, “akiwa na shangwe na furaha moyoni” kwa sababu ya kualikwa na mfalme na malkia wake. Hata hivyo, Hamani alipokuwa akipita kwenye lango la jumba la mfalme, alimwona Mordekai, Myahudi ambaye alikataa kumpa heshima ya kipekee. Mordekai hakufanya hivyo ili kumvunjia heshima, badala yake, alihangaikia dhamiri yake na uhusiano wake pamoja na Yehova Mungu. Ingawa hivyo, ‘upesi Hamani alijawa na ghadhabu.’—Esta 5:9.

Hamani alipowaambia rafiki zake na mke wake kuhusu tendo hilo la kumvunjia heshima, walimwambia atengeneze mti mkubwa, wenye urefu wa mita 22, kisha amwombe mfalme ruhusa ili amtundike Mordekai juu yake. Hamani alipendezwa na wazo hilo na mara moja akaanza kufanya hivyo.—Esta 5:12-14.

Wakati huohuo, mfalme hakuweza kulala. Biblia inasema: “Usingizi wa mfalme ulimtoka,” hivyo akaagiza asomewe kwa sauti rekodi rasmi za Taifa. Usomaji huo ulitia ndani ripoti kuhusu njama ya kumuua Ahasuero. Alikumbuka tukio hilo; watu waliotaka kumuua walikamatwa na kuuawa. Namna gani mwanamume aliyefunua njama hiyo—Mordekai? Kwa ghafula, mfalme aliuliza jinsi Mordekai alivyotuzwa. Alijibiwaje? Hakuwa ametuzwa kwa njia yoyote ile.—Esta 6:1-3.

Akiwa amekasirika, mfalme aliuliza ni maofisa gani wa jumba la mfalme waliokuwapo ili kumsaidia kurekebisha jambo hilo. Ofisa aliyekuwapo katika makao ya mfalme ni Hamani. Inaonekana alikuwa amefika mapema kwa sababu alitaka sana kupata kibali cha kumuua Mordekai. Lakini kabla ya kutoa ombi lake, mfalme alimuuliza Hamani jinsi ya kumheshimu kwa njia iliyo bora zaidi mwanamume ambaye alikuwa amepata kibali cha mfalme. Hamani alifikiri mfalme alikuwa akizungumza kumhusu. Hivyo akafikiria jambo ambalo lingemletea heshima kubwa: Mwanamume huyo avishwe mavazi ya kifalme, na apewe ofisa wa cheo cha juu aandamane naye kuzunguka Shushani akiwa amepanda juu ya farasi wa mfalme, na kumsifu kwa sauti ili watu wote wasikie. Wazia jinsi uso wa Hamani ulivyoonekana alipoambiwa kwamba mtu ambaye angeonyeshwa heshima hiyo ni Mordekai! Na mfalme alimpa nani kazi ya kumsifu Mordekai kwa nyimbo? Hamani!—Esta 6:4-10.

Bila kutaka, Hamani alifanya kazi hiyo yenye kumchukiza, kisha akaenda nyumbani haraka akiwa amevunjika moyo. Huenda alitazamia kuhurumiwa na rafiki zake na mke wake, lakini wakamwambia kwamba kulingana na jinsi hali zilivyoonekana, hiyo ni ishara kwamba angepatwa na mabaya; angeshindwa katika vita vyake dhidi ya Mordekai na Wayahudi.—Esta 6:12, 13.

Kwa sababu Esta alionyesha subira, akangoja siku moja zaidi kabla ya kutoa ombi lake kwa mfalme, hatua hiyo iliandaa nafasi kwa Hamani kujiletea fedheha kubwa badala ya heshima. Na je, si inawezekana kwamba Yehova Mungu ndiye aliyefanya mfalme akose usingizi? (Methali 21:1) Basi, haishangazi kwamba Neno la Mungu linatutia moyo tuonyeshe ‘mtazamo wa kungojea.’ (Mika 7:7) Tunapomngojea Mungu, huenda tukatambua kwamba njia yake ya kutatua matatizo ni bora zaidi kuliko njia zetu.

Alisema kwa Ujasiri

Esta hangethubutu kumfanya mfalme aendelee kusubiri; lazima angemweleza mambo yote kwenye karamu aliyoandaa siku ya pili. Jinsi gani? Mfalme alimpa nafasi ya kujieleza, akimuuliza tena kuhusu ombi lake. (Esta 7:2) ‘Wakati wa Esta wa kusema’ ulikuwa umefika.

Tunaweza kuwazia Esta akitoa sala fupi kwa Mungu kabla ya kusema maneno haya: “Ikiwa nimepata kibali machoni pako, Ee mfalme, na mfalme akiona vema, na nipewe nafsi yangu mwenyewe kuwa ombi langu na watu wangu kuwa haja yangu.” (Esta 7:3) Ona kwamba kwanza alimheshimu mfalme, akimhakikishia kuwa aliheshimu uamuzi wake kuhusu mambo aliyoona yanafaa. Esta alikuwa tofauti kama nini na Vashti ambaye alimfedhehesha mume wake kimakusudi! Vashti alikuwa mke wa mfalme kabla ya Esta. (Esta 1:10-12) Isitoshe, Esta hakumwonyesha mfalme kwamba alitenda kipumbavu kwa kumwamini Hamani. Badala yake, alimwomba mfalme amlinde kutokana na hatari iliyomkabili.

Bila shaka, ombi hilo lilimshangaza mfalme na kumgusa moyo. Ni nani ambaye angethubutu kumtisha malkia? Esta aliendelea kusema: “Tumeuzwa, mimi na watu wangu, tuangamizwe, tuuawe na kuharibiwa. Basi ikiwa tungaliuzwa tuwe watumwa na wajakazi, ningalinyamaza kimya. Lakini taabu hii haifai ikiwa inamletea mfalme hasara.” (Esta 7:4) Ona kwamba Esta alifunua tatizo waziwazi, lakini akaongezea kuwa angenyamaza kuhusu jambo hilo ikiwa hatari ilikuwa kuuzwa kama watumwa tu. Hata hivyo, mauaji hayo ya jamii nzima yangemletea mfalme hasara kubwa, kwa hiyo hata mfalme mwenyewe hangepaswa kunyamaza.

Mfano wa Esta unatufunza mengi kuhusu njia bora ya kutumia ushawishi. Ikiwa ungependa kufunua tatizo zito kwa mtu unayempenda au hata mtu mwenye mamlaka, kuwa na subira, heshima, na kusema mambo waziwazi kunaweza kukusaidia sana.—Methali 16:21, 23.

Ahasuero aliuliza: “Ni nani huyo, na yuko wapi mtu huyo ambaye amejipatia ujasiri wa kufanya hivyo?” Wazia Esta akinyoosha kidole chake na kutamka maneno haya: “Mtu huyo, mpinzani na adui, ni huyu Hamani mtu mbaya.” Mashtaka yalikuwa yametolewa. Hamani alijawa na hofu. Wazia jinsi uso wa mfalme huyo mwenye hasira ulivyobadilika na kuwa mwekundu alipotambua kwamba mshauri wake aliyemwamini alikuwa amemdanganya atie sahihi agizo ambalo lingemwangamiza mke wake mpendwa! Mfalme alitoka kwa hasira na kwenda kwenye bustani ili atulie.—Esta 7:5-7.

Hamani, aliyekuwa amefunuliwa jinsi alivyo—mtu mwenye hila na mwoga—aliinama miguuni pa malkia. Mfalme aliporudi chumbani na kumwona Hamani akimsihi Esta akiwa juu ya kitanda chake, mfalme akamshtaki Hamani kwa hasira kwamba alikuwa akijaribu kumlala malkia kinguvu katika nyumba ya mfalme. Maneno hayo yalimaanisha hukumu ya kifo kwa Hamani. Aliondolewa huku uso wake ukiwa umefunikwa. Kisha, mmoja wa maofisa wa mfalme akapaaza sauti na kumwambia mfalme kuhusu mti mkubwa ambao Hamani alikusudia kumtundika Mordekai. Mara moja, Ahasuero akaagiza kwamba Hamani atundikwe juu ya mti huo.—Esta 7:8-10.

Katika ulimwengu wa leo usio na haki, ni rahisi kuwazia kwamba haki haitawahi kutekelezwa. Je, umewahi kuhisi hivyo? Esta hakukata tamaa kamwe, hakuwa na shaka, wala kukosa imani. Wakati ulipofika, alisema kwa ujasiri kuhusu mambo yaliyofaa, na aliamini kwamba Yehova angefanya lolote lililohitajika. Acheni tufanye vivyo hivyo! Yehova hajabadilika tangu siku za Esta. Bado ana uwezo wa kuwanasa waovu na wenye hila katika mitego yao wenyewe, kama alivyomnasa Hamani.—Zaburi 7:11-16.

Alitenda Bila Ubinafsi kwa Ajili ya Yehova na Watu Wake

Mwishowe, mfalme alijua Mordekai alikuwa nani. Hakuwa tu mtu aliyemlinda kutokana na njama ya kumuua bali pia baba mlezi wa Esta. Ahasuero alimpa Mordekai cheo cha Hamani cha waziri mkuu. Kisha, akampa Esta nyumba ya Hamani kutia ndani utajiri wake mwingi, naye Esta akamweka Mordekai kuwa msimamizi wa nyumba hiyo.—Esta 8:1, 2.

Sasa kwa kuwa Esta na Mordekai walikuwa salama, je, malkia angetulia na kustarehe? Angefanya hivyo tu ikiwa angekuwa na ubinafsi. Wakati huo, agizo la Hamani la kuwaua Wayahudi wote bado lilikuwa likisambazwa kotekote katika milki hiyo. Hamani alikuwa amepiga kura, au Puri—labda njia fulani ya kuwasiliana na pepo—ili kuamua wakati uliofaa wa kutekeleza mashambulizi hayo ya kikatili. (Esta 9:24-26) Bado miezi kadhaa ilibaki kabla ya siku hiyo kufika, lakini muda ulikuwa unayoyoma. Je, msiba huo ungeepukwa?

Esta alitenda bila ubinafsi na akahatarisha uhai wake tena kwa kwenda mbele ya mfalme bila kuitwa. Wakati huu, alilia kwa ajili ya watu wake, na kumsihi mume wake afutilie mbali agizo baya alilokuwa ametoa. Lakini sheria zilizopitishwa katika jina la mfalme wa Uajemi hazingeweza kufutiliwa mbali. (Danieli 6:12, 15) Hivyo, mfalme alimpa Esta na Mordekai mamlaka ya kuandika sheria mpya. Hivyo, tangazo la pili likatolewa, na kuwapa Wayahudi haki ya kujilinda wasishambuliwe. Wapanda-farasi walienda kwa kasi kila sehemu ya milki hiyo, na kuwapelekea Wayahudi habari hizo njema, hivyo wengi wakawa na tumaini. (Esta 8:3-16) Tunaweza kuwazia Wayahudi kotekote katika milki hiyo kubwa wakijihami kwa silaha, tayari kupigana, jambo ambalo hawangefanya ikiwa sheria hiyo mpya haingepitishwa. Hata hivyo, swali muhimu ni, je, “Yehova wa majeshi” angekuwa pamoja na watu wake?—1 Samweli 17:45.

Siku iliyochaguliwa ilipofika, watu wa Mungu walikuwa tayari. Hata maofisa wengi wa Uajemi sasa waliwaunga mkono, kwa kuwa habari zilikuwa zimesambaa kotekote kuhusu waziri mkuu mpya, Mordekai yule Myahudi. Yehova aliwapa watu wake ushindi mkubwa. Bila shaka, alihakikisha kwamba watu wake waliwashinda kabisa adui zao ili wasishambuliwe tena wakati mwingine. *Esta 9:1-6.

Zaidi ya hayo, Mordekai hangekuwa salama kusimamia nyumba ya Hamani huku wana kumi wa mwanamume huyo mwovu wakiwa hai. Wao pia waliuawa. (Esta 9:7-10) Hivyo, unabii wa Biblia ukatimia, kwa sababu Mungu alikuwa ametabiri mapema kwamba Waamaleki, ambao walikuwa maadui waovu wa watu wake, wangeangamizwa kabisa. (Kumbukumbu la Torati 25:17-19) Yaelekea wana wa Hamani ndio waliokuwa watu wa mwisho kuangamizwa kutoka taifa la Waamaleki lililolaaniwa.

Esta alilazimika kubeba fungu lake la mizigo mizito, kama vile maagizo ya kifalme yaliyotia ndani vita na mauaji. Halikuwa jambo rahisi. Lakini mapenzi ya Yehova yalikuwa kwamba watu wake walindwe ili wasiangamizwe; taifa la Israeli lingetokeza Masihi aliyeahidiwa, yule ambaye angekuwa chanzo pekee cha tumaini kwa wanadamu wote! (Mwanzo 22:18) Leo, watumishi wa Mungu wanafurahi kujua kwamba yule Masihi, Yesu, alipokuja duniani, aliwakataza wafuasi wake kutoka wakati huo na kuendelea wasishiriki katika vita vya kimwili.—Mathayo 26:52.

Hata hivyo, Wakristo wanashiriki katika vita vya kiroho; Shetani anatamani hata zaidi kuharibu imani yetu katika Yehova Mungu. (2 Wakorintho 10:3, 4) Ni baraka iliyoje kuwa na mfano kama wa Esta! Kama yeye, na tuonyeshe imani kwa kuwa wenye subira na hekima tunapotumia ushawishi, kuwa jasiri, na kuwa tayari kutenda bila ubinafsi katika kuwatetea watu wa Mungu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Katika makala iliyotangulia ya mfululizo huu, tuliona jinsi Esta aliyekuwa yatima alivyolelewa na Mordekai, binamu yake mkubwa, na baadaye akachaguliwa kuwa mke wa Ahasuero, mfalme wa Uajemi. Hamani, ambaye alikuwa mshauri wa mfalme, alipanga njama ya kuwaangamiza watu wa Mordekai, yaani, Wayahudi. Mordekai alimsadikisha Esta kwenda mbele ya mfalme ili kuwatetea Wayahudi.—Ona makala “Igeni Imani Yao—Aliwatetea Watu wa Mungu,” katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Oktoba 1, 2011.

^ fu. 32 Mfalme aliwaruhusu Wayahudi waendelee kupigana na adui zao kwa siku nyingine mbili ili wawashinde kabisa. (Esta 9:12-14) Mpaka leo, Wayahudi husherehekea ushindi huo kila majira ya kuchipua katika sherehe inayoitwa Purimu, ambayo ilipata jina kutokana na kura ambayo Hamani alipiga alipokuwa akipanga kuwaangamiza Waisraeli.

[Sanduku katika ukurasa wa 28]

Maswali Kumhusu Esta

Kwa nini Mordekai alikubali Esta aolewe na mpagani asiyemwamini Mungu?

Hakuna sababu zinazounga mkono maoni ya wasomi fulani kwamba Mordekai alitaka kujifaidi na kujipatia umaarufu kwa kumruhusu Esta aolewe na mfalme. Akiwa Myahudi mwaminifu, hangeruhusu ndoa kama hiyo ifanyike. (Kumbukumbu la Torati 7:3) Kulingana na mapokeo ya kale ya Wayahudi, Mordekai alijaribu kuzuia ndoa hiyo. Inaonekana kwamba kwa sababu Mordekai na Esta walikuwa wakaaji wageni katika nchi iliyotawaliwa na mtawala mwenye mamlaka kubwa ambaye alionwa kama mungu, hawakuwa na uwezo wowote wa kuzuia jambo hilo. Baada ya muda, ilikuwa wazi kwamba Yehova aliitumia ndoa ya Esta kuwalinda watu wake.—Esta 4:14.

Kwa nini kitabu cha Esta hakitaji jina la kibinafsi la Mungu, Yehova?

Ni wazi kwamba Mordekai ndiye aliyeongozwa na roho ya Mungu kuandika kitabu hicho. Labda kitabu hicho kiliwekwa pamoja na rekodi rasmi za Uajemi kabla ya kupelekwa Yerusalemu. Ikiwa jina la Yehova lingetumiwa, huenda waabudu wa miungu ya Uajemi wangechochewa kukiharibu kitabu hicho. Vyovyote vile, ni wazi kwamba Yehova alihusika katika simulizi hilo. Jambo la kupendeza ni kwamba jina la kibinafsi la Mungu limefichwa katika maandishi ya awali ya Kiebrania kwa njia ya kwamba maneno yamepangwa kimakusudi ili herufi za kwanza au za mwisho za kila neno zifanyize jina la Mungu.

Je, kitabu cha Esta ni sahihi kihistoria?

Wachambuzi wengi wanasema kwamba kitabu hicho si sahihi kihistoria. Hata hivyo, wasomi fulani wamesema kwamba mwandikaji wa kitabu hicho alikuwa na ujuzi mwingi kuhusu utawala, majengo, na tamaduni za Uajemi. Ni kweli kwamba hakuna maandishi yoyote ya kilimwengu yaliyobaki ambayo yanamtaja Malkia Esta, hata hivyo, kati ya washiriki wa nyumba ya mfalme si Esta tu ambaye habari zake ziliondolewa katika rekodi za umma. Zaidi ya hayo, rekodi za kilimwengu zinaonyesha kwamba mwanamume aliyeitwa Mardukâ, jina la Kiajemi linalomaanisha Mordekai, alitumika kama ofisa wa makao ya mfalme huko Shushani katika kipindi kinachotajwa katika kitabu hicho.

[Sanduku katika ukurasa wa 29]

Unabii Watimizwa

Walipokuwa wakiwapigania watu wa Mungu, Esta na Mordekai walitimiza unabii mwingine wa Biblia. Zaidi ya miaka 1,200 mapema, Yehova alimwongoza kwa roho takatifu mzee wa ukoo Yakobo kutabiri hivi kuhusu mmoja wa wanawe: “Benyamini ataendelea kurarua kama mbwa-mwitu. Asubuhi atakula mnyama aliyekamatwa na jioni atagawanya nyara.” (Mwanzo 49:27) Katika “asubuhi,” yaani, mwanzoni mwa utawala wa kifalme wa Israeli, wazao wa Benyamini walitia ndani Mfalme Sauli na wapiganaji wengine hodari wa watu wa Yehova. Katika “jioni,” yaani, mwishoni mwa utawala huo wa kifalme wa Israeli, Esta na Mordekai, ambao walikuwa washiriki wa kabila la Benyamini, walipigana na kuwashinda maadui wa Yehova. Kwa njia fulani, wao pia waligawanya nyara, kwa sababu walimiliki mali ya Hamani iliyokuwa nyingi.

[Picha katika ukurasa wa 25]

Esta alikubali kwa unyenyekevu huruma ya mfalme

[Picha katika ukurasa wa 26, 27]

Esta alitaja kwa ujasiri uovu wa Hamani

[Picha katika ukurasa wa 28, 29]

Esta na Mordekai walituma matangazo kwa Wayahudi katika Milki ya Uajemi