Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mahali Ambapo Mipaka Haina Maana

Mahali Ambapo Mipaka Haina Maana

Mahali Ambapo Mipaka Haina Maana

Mashahidi wa Yehova hujitahidi kushinda ubaguzi ambao huwatenganisha watu. Wanafuata kanuni muhimu iliyo katika maneno ambayo Yesu aliwaambia wanafunzi wake: “Ninyi nyote ni ndugu.” (Mathayo 23:8) Jambo hilo limethibitika katika maeneo mawili ya kuabudu ya Mashahidi wa Yehova—yaliyo Ureno na Hispania.

JIJI la Valença do Minho, linalozingirwa na ukuta, liko kaskazini mwa Ureno nalo lilijengwa wakati wa hatari. Ukiwa kwenye minara ya jiji hilo unaweza kuona Mto Minho unaogawanya nchi ya Hispania na Ureno. Ng’ambo ya mto huo kuna jiji la Hispania linaloitwa Tui. Katika jiji hilo kuna kanisa kubwa ambalo ni kama ngome. Ngome kuu za majiji ya Tui na Valença zimekuwapo kuanzia karne ya 17, wakati Hispania ilipopigana na Ureno.

Mwaka wa 1995, vizuizi vya mipakani na ofisi za forodha ziliondolewa kabisa katika nchi hizo mbili ambazo ni wanachama wa Muungano wa Ulaya. Lakini hilo halikuwaunganisha watu wa nchi hizo mbili. Muungano kama huo unapaswa kuhusisha akili na mioyo ya watu. Huko Valença kuna jengo dogo lenye kuvutia ambalo linaonyesha jinsi watu wanavyoweza kuunganishwa. Ni mahali pa ibada, yaani, Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova linalotumiwa na makutaniko ya Mashahidi kutoka Hispania na Ureno.

Hali hiyo ilitokea mwaka wa 2001, wakati Mashahidi wa Tui, Hispania, walipohitaji Jumba jipya la Ufalme. Walihitaji kuondoka katika jumba fulani walilokuwa wamekodi na hawakuwa na pesa za kutosha kujenga jumba jipya. Hata jumba hilo walilokuwa wamekodi lilikuwa ghali sana kwao, kwa sababu walikuwa wachache. Kwa hiyo, Mashahidi hao wa Hispania wakawaomba ndugu wa kutaniko la Valença wawaruhusu kutumia jumba lao, ambalo liko kilomita kadhaa kutoka jijini Tui.

“Tulizungumzia uamuzi huo katika mkutano fulani mnamo Desemba 2001,” anasema Eduardo Vila, mshiriki wa Kutaniko la Tui, huko Hispania. “Baada ya mkutano huo nilitambua kwamba Yehova alikuwa amegusa mioyo ya ndugu zetu Wareno. Walikuwa wamejidhabihu sana ili kujenga jumba hilo maridadi, na lilikuwa jambo lenye kuimarisha imani kuona kwamba walikuwa tayari kuturuhusu tutumie jumba hilo.”

“Tuliwakaribisha ndugu hao wa Hispania kutumia Jumba letu la Ufalme,” anasema Américo Almeida, Shahidi Mreno ambaye pia alikuwapo katika mkutano huo. “Tulikuwa na hakika kwamba Yehova atabariki mpango huo, na kila mtu alikubaliana nao.” Mashahidi hao kutoka nchi hizo mbili wanaendelea kushirikiana vizuri. “Huenda likaonekana kuwa jambo lisilo la kawaida, lakini hata hatutambui kwamba tumetoka nchi mbili tofauti. Sisi ni ndugu wa kiroho,” anasema Paolo kutoka Valença.

Jambo moja ambalo wageni hutambua mara moja wanapoingia katika Jumba la Ufalme ni saa mbili zinazofanana zilizo kwenye ukuta wa nyuma, ambazo zinaonyesha wakati tofauti. Hispania iko mbele ya Ureno kwa saa moja, lakini tofauti hiyo ya saa ndilo jambo pekee linalotofautisha ndugu wa Ureno na wa Hispania. Jumba hilo lilipohitaji kurekebishwa, Halmashauri ya Ujenzi wa Mkoa iliyo nchini Hispania ilisimamia wafanyakazi kutoka makutaniko yote mawili ambao walifanya kazi kwa bidii. “Ndugu wengi wenye ujuzi kutoka Hispania walikuja kutusaidia, na baadhi yao walisafiri zaidi ya kilomita 160,” anasema Paolo. “Kazi hiyo iliimarisha umoja na upendo kati ya ndugu wa makutaniko yote mawili.”

Acheni tuchunguze mfano wa pili katika kukabiliana na matatizo ya mipaka.

Umoja Katika Bonde Lililogawanyika

Puigcerdá ni jiji la Hispania lililo kwenye mpaka wa Hispania na Ufaransa. Jiji hilo liko katika bonde lenye rutuba lililozungukwa na milima ya Pyrenees yenye vilele virefu. Zamani bonde lote, ambalo linaitwa Cerdaña, lilikuwa sehemu ya Hispania. Lakini mwaka wa 1659, katika mkataba wa amani unaoitwa Mkataba wa Pyrenees, Hispania ilikubali Ufaransa imiliki nusu ya bonde hilo.

Leo, Wafaransa hununua bidhaa zao huko Puigcerdá, jiji kuu la bonde hilo. Na tangu mwaka wa 1997, Mashahidi wa Yehova wa Puigcerdá wamewaruhusu ndugu zao kutoka Ufaransa watumie Jumba lao la Ufalme lililo katika jiji hilo. Katika mwaka huo Mashahidi kutoka Ufaransa walilazimika kuacha kutumia jengo walilokuwa wamekodi. Ili kufika kwenye Jumba la Ufalme lililo karibu katika nchi ya Ufaransa, inachukua muda wa saa moja kwa gari, na katika majira ya baridi kali mara nyingi njia iliyo kwenye ile milima mirefu huwa haipitiki kwa sababu ya theluji.

Mashahidi kutoka Ufaransa walipowaeleza Mashahidi wa Hispania kuhusu uhitaji wao wa haraka wa kupata mahali pa kukutania, Mashahidi hao wa Hispania waliwaruhusu mara moja waanze kutumia Jumba lao la Ufalme. “Ndugu wote katika kutaniko la Hispania walifurahi kuturuhusu tutumie jumba lao,” anakumbuka Prem, Shahidi anayeishi katika eneo hilo. “Bila shaka, mtazamo huo ulitokana na mazoezi ya Kimaandiko ambayo tumepokea kwa miaka mingi. Majuma machache baadaye tulianza kutumia Jumba hilo moja la Ufalme, na tumefanya hivyo kwa miaka 13 sasa.”

“Puigcerdá ndipo mahali palipofaa kuwa na Jumba la Ufalme,” anaeleza Eric, mwangalizi katika kutaniko la Ufaransa. “Na bado ninakumbuka jinsi ndugu wa kutaniko la Kihispania walivyotukaribisha kwa uchangamfu. Walipamba jumba lao kwa shada kubwa la maua na kuweka bango lililoandikwa ‘Mnakaribishwa, enyi ndugu na dada zetu wapendwa.’”

“Watu walifikiri kwamba kufungwa kwa Jumba letu la Ufalme nchini Ufaransa kulimaanisha mwisho wa kutaniko letu,” Eric anaongeza. “Lakini kuhubiri kwetu kwa ukawaida katika eneo hilo—kulikotia ndani kusambaza mialiko ya kuhudhuria mikutano nchini Hispania—kulionyesha kuwa bado tunaendelea. Watu wanaopendezwa wanafurahia kuja kwenye jumba lililo Hispania. Zaidi ya hayo, tumekuwa na uhusiano wa karibu sana na ndugu zetu Wahispania kwa kuwa sote tunatumia jumba moja kwa ajili ya mikutano. Awali, tulijua kwamba kuna kutaniko la Kihispania upande ule mwingine wa mpaka, lakini hatukufahamiana sana na ndugu katika kutaniko hilo. Sasa kwa kuwa tunaonana kwa ukawaida, hatuhisi tukiwa peke yetu katika bonde hili la milimani lililo mbali.”

Je, tofauti za utamaduni zilifanya wawe na wasiwasi? “Niliposikia kwamba mikutano yetu itakuwa ikifanyiwa nchini Hispania, yaani, upande ule mwingine wa mpaka, nilikuwa na wasiwasi kidogo,” anasema dada kutoka Ufaransa aliye na umri wa miaka 80 hivi. “Lakini ndugu wa Puigcerdá walitukaribisha na kutuonyesha urafiki, hivyo hakukuwa na shida yoyote. Isitoshe, hiyo ilikuwa nafasi ya kuonyesha kwamba Mashahidi wa Yehova kutoka mataifa yote wana umoja.”

Msingi wa Muungano Wenye Nguvu Zaidi

Waanzilishi wa muungano wa Ulaya walisema kwamba nchi wanachama wa muungano huo “zimeazimia kuweka misingi ya muungano yenye nguvu zaidi kati ya watu wa bara Ulaya.” Kuondolewa kwa vizuizi vya mipakani katika miaka ya 1980 na 1990 kulikusudiwa kuharakisha mpango huo. Lakini mipaka pia inahitaji kuondolewa katika akili za watu.

Mashahidi wa Yehova hujitahidi sana kuondoa ubaguzi na hali ya kutoaminiana. Wanatambua kwamba ni muhimu kuchangamana na ndugu kutoka maeneo mbalimbali na kwamba “Mungu hana ubaguzi.” (Matendo 10:34) Kwenye makusanyiko yao ya kimataifa na katika Majumba yao ya Ufalme, wameona “jinsi ilivyo vyema na jinsi inavyopendeza ndugu kukaa pamoja kwa umoja!” (Zaburi 133:1) Umoja ambao umesitawi kati ya Mashahidi wa Valença na Puigcerdá na ndugu zao wanaotoka katika nchi zilizo karibu ni uthibitisho wa jambo hilo.

[Blabu katika ukurasa wa 13]

“Huenda likaonekana kuwa jambo lisilo la kawaida, lakini hata hatutambui kwamba tumetoka nchi mbili tofauti. Sisi ni ndugu wa kiroho”

[Blabu katika ukurasa wa 14]

“Kazi hiyo iliimarisha umoja na upendo kati ya ndugu wa makutaniko yote mawili”

[Blabu katika ukurasa wa 15]

“Jinsi ilivyo vyema na jinsi inavyopendeza ndugu kukaa pamoja kwa umoja!” ZABURI 133:1

[Picha katika ukurasa wa 12, 13]

Jinsi eneo la Tui na Mto Minho linavyoonekana kutoka kwenye jiji lililozingirwa na ukuta la Valença do Minho

[Picha katika ukurasa wa 14]

Kurekebisha Jumba la Ufalme

[Picha katika ukurasa wa 15]

Milima ya Pyrenees na bonde la Cerdaña

[Picha katika ukurasa wa 15]

Wazee wawili kutoka makutaniko mawili—la Kihispania na la Kifaransa—yanayokutana katika Jumba la Ufalme la Puigcerdá