Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, kweli watu walipiga filimbi kwenye mazishi katika siku za Yesu?

Biblia inataja kwamba filimbi zilipigwa kwenye sherehe mbalimbali. (1 Wafalme 1:40; Isaya 5:12; 30:29) Pia, inasema kwamba filimbi zilipigwa kwenye mazishi. Filimbi pekee ndizo zinazotajwa kuwa zilitumiwa kwenye mazishi. Injili ya Mathayo inasema kwamba mtawala fulani Myahudi alimwomba Yesu amponye binti yake, ambaye alikuwa karibu kufa. Hata hivyo, Yesu alipofika kwenye nyumba ya mtawala huyo, ‘aliwaona wapiga-filimbi na umati wa watu wakipiga kelele kwa kuvurugika,’ kwa kuwa yule mtoto alikuwa amekufa.​—Mathayo 9:18, 23.

Je, Mathayo aliandika kwa usahihi kuhusu zoea hilo? Mtafsiri wa Biblia William Barclay anasema: “Katika sehemu nyingi za ulimwengu wa kale, kama vile Roma, Ugiriki, Foinike, Ashuru, na Palestina, mlio wa kuomboleza wa filimbi ulihusianishwa na kifo na msiba.” Kulingana na Talmud, hata mwanamume Myahudi maskini zaidi aliyefiwa na mkewe katika karne ya kwanza W.K. angekodi wapiga-filimbi wawili na mwanamke mliaji ili kumwombolezea mkewe aliyekufa. Flavio Yosefo, mwanahistoria aliyeishi katika karne ya kwanza, aliandika kuwa habari zilipofika Yerusalemu kwamba Waroma wameteka Jotapata, katika eneo la Galilaya, na kuwaua wakaaji wake mwaka wa 67 W.K., “waombolezaji wengi walikodi wapiga-filimbi ili wajiunge nao kuimba nyimbo za maombolezo.”

Watenda-dhambi waliouwa pamoja na Yesu walikuwa wamefanya kosa gani?

Biblia inawaita watenda-dhambi hao “wanyang’anyi.” (Mathayo 27:38; Marko 15:27) Kamusi fulani za Biblia zinasema kwamba Maandiko yanatumia maneno mbalimbali ili kutofautisha aina za uhalifu. Neno la Kigiriki kleptes linarejelea mwizi anayeiba kisiri ili asishikwe. Neno hilo linatumiwa kumhusu Yuda Iskariote, ambaye aliiba kisiri kutoka katika sanduku la pesa za mitume. (Yohana 12:6) Kwa upande mwingine, neno lestes, kwa kawaida linarejelea mwizi aliyeiba kwa kutumia jeuri na pia lingeweza kurejelea mwanamapinduzi, mwasi, au mpiganaji wa kuvizia. Wahalifu waliouawa pamoja na Yesu walikuwa wa aina hii ya pili. Hata inatajwa kwamba mmoja wao alisema: “Tunapokea kwa ukamili kile tunachostahili kwa mambo tuliyofanya.” (Luka 23:41) Hilo linamaanisha kwamba hawakuwa tu na hatia ya kuiba.

Kama wanyang’anyi hao wawili, Baraba pia anaitwa lestes. (Yohana 18:40) Ili kuonyesha wazi kwamba Baraba hakuwa tu mwizi, andiko la Luka 23:19 linasema kwamba alikuwa “ametupwa gerezani kwa sababu ya uchochezi wa uasi fulani uliotukia katika jiji na kwa kuua.”

Kwa hiyo, ingawa watenda-dhambi waliouwa pamoja na Yesu walikuwa wanyang’anyi, inawezekana kwamba walihusika pia katika mauaji au hata kuchochea uasi. Hata iwe walikuwa wamefanya kosa gani, Gavana Mroma Pontio Pilato aliona kwamba wanastahili kuuawa kwa kutundikwa mtini.