Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jifunze Kutoka Katika Neno la Mungu

Kwa Nini Mungu Amewapanga Watu Wake kwa Utaratibu?

Kwa Nini Mungu Amewapanga Watu Wake kwa Utaratibu?

Makala hii inazungumzia maswali ambayo huenda umejiuliza na inakuonyesha mahali unapoweza kupata majibu katika Biblia yako. Mashahidi wa Yehova watafurahi kuzungumzia majibu hayo pamoja nawe.

1. Kwa nini Mungu aliwapanga Waisraeli kwa utaratibu?

Mungu aliwapanga wazao wa mzee wa ukoo Abrahamu kuwa taifa na kuwapa sheria. Alichagua taifa la Israeli na kulipatia daraka la kutunza ibada ya kweli na Neno lake, yaani, Maandiko Matakatifu. (Zaburi 147:19, 20) Hivyo, watu wa mataifa yote wamefaidika.​—Soma Mwanzo 22:18.

Mungu aliwachagua Waisraeli wawe mashahidi wake. Walipotii, walifaidika kwa kufuata sheria za Mungu. (Kumbukumbu la Torati 4:6) Kwa kuchunguza historia ya Waisraeli, tunaweza kujifunza mengi kumhusu Mungu wa kweli.​—Soma Isaya 43:10, 12.

2. Kwa nini Wakristo wa kweli wamepangwa kwa utaratibu fulani?

Baada ya muda, Waisraeli walipoteza kibali cha Mungu, hivyo Yehova akachagua kutaniko la Kikristo lichukue mahali pa taifa hilo. (Mathayo 21:43; 23:37, 38) Mwanzoni, Waisraeli walikuwa mashahidi wa Mungu. Leo, Wakristo wa kweli wanatumika wakiwa mashahidi wa Yehova.​—Soma Matendo 15:14, 17.

Yesu aliwapanga wafuasi wake kwa utaratibu ili watoe ushahidi kumhusu Yehova na kufanya wanafunzi kutoka katika mataifa yote. (Mathayo 10:7, 11; 24:14; 28:19, 20) Kazi hiyo inakaribia mwisho wake. Kwa mara ya kwanza, Yehova ameunganisha mamilioni ya watu kutoka katika mataifa yote kwenye ibada ya kweli. (Ufunuo 7:9, 10) Wakristo wa kweli ni kikundi cha watu ambao pia wamepangwa kwa utaratibu na hilo linawasaidia kutiana moyo na kusaidiana. Wanafurahia programu ileile ya mafundisho ya Biblia kwenye mikutano yao ulimwenguni pote.​—Soma Waebrania 10:24, 25.

3. Tengenezo la Mashahidi wa Yehova lilianza lini?

Tengenezo la kisasa la Mashahidi wa Yehova lilianza katika miaka ya 1870. Kikundi kidogo cha wanafunzi wa Biblia kilianza kufunua tena kweli za Biblia ambazo zilikuwa zimefichwa kwa muda mrefu. Walijua kwamba Yesu alikuwa amepanga kutaniko la Kikristo kwa utaratibu ili lihubiri. Hivyo, walianza kampeni ya kuhubiri Ufalme ulimwenguni pote. Katika mwaka wa 1931 walianza kutumia jina Mashahidi wa Yehova.​—Soma Matendo 1:8; 2:1, 4; 5:42.

4. Leo, Mashahidi wa Yehova wamepangwa kwa utaratibu gani?

Katika karne ya kwanza, makutaniko ya Kikristo katika maeneo mengi yalifaidika kutokana na baraza kuu linaloongoza ambalo lilimkubali Yesu kuwa Kichwa cha kutaniko. (Matendo 16:4, 5) Vivyo hivyo leo, Mashahidi wa Yehova wanamkubali Yesu kuwa Kiongozi wao. (Mathayo 23:9, 10) Wanafaidika pia kutokana na mwongozo wa Baraza Linaloongoza la wazee wenye uzoefu ambao wanatumia Maandiko kuongoza na kutia moyo makutaniko zaidi ya 100,000. Katika kila kutaniko, wanaume wanaostahili wanatumika wakiwa wazee, au waangalizi. Wanaume hao wanatunza kundi la Mungu kwa upendo.​—Soma 1 Petro 5:2, 3.

Mashahidi wa Yehova wamepangwa kwa utaratibu ili wahubiri habari njema na kufanya wanafunzi. Ili kuwasaidia watu kila mahali, Mashahidi wanatafsiri, kuchapa, na kusambaza machapisho ya Biblia katika lugha zaidi ya 500. Kama mitume, wanahubiri nyumba kwa nyumba. (Matendo 20:20) Wanajitolea kujifunza Biblia kibinafsi na watu wanyoofu wanaopenda ukweli. Kwa kuwa watu wa Yehova wanazingatia kumpendeza Mungu na kuwasaidia wengine, wao ni tengenezo la watu wenye furaha.​—Soma Zaburi 33:12; Matendo 20:35.

Kwa habari zaidi, ona sura ya 19 ya kitabu hiki, Biblia Inafundisha Nini Hasa?, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.