Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wafundishe Watoto Wako

“Aliendelea Kushikamana na Yehova”

“Aliendelea Kushikamana na Yehova”

JE, UMEWAHI kuambiwa ushikamane na kitu fulani? * Wazazi na walimu wanaweza kuwaambia watoto washikamane na masomo yao. Hilo linamaanisha kuona masomo kuwa jambo la maana. Tunataka kuzungumza kuhusu mtu ambaye Biblia inasema kwamba ‘aliendelea kushikamana na Yehova,’ Mungu wa kweli. Mtu huyo anaitwa Hezekia. Hebu tuone mfano wake unatufundisha nini.

Maisha ya Hezekia alipokuwa mtoto hayakuwa yenye furaha. Baba yake, Ahazi, mfalme wa Yuda, aliacha kumtumikia Yehova. Ahazi aliongoza watu kuabudu miungu ya uwongo Hezekia alipokuwa angali mvulana mdogo. Hata Ahazi aliagiza mmoja kati ya watoto wake wa kiume, ambaye alikuwa ndugu ya Hezekia, auawe na kutolewa dhabihu kwa mungu ambaye Ahazi aliabudu!

Hata ingawa Ahazi aliendelea kufanya mambo mabaya, Hezekia hakuacha kumtii Yehova. Je, unafikiri ilikuwa vigumu kwa Hezekia kufanya hivyo?— Bila shaka, ilikuwa vigumu. Lakini Hezekia hakukata tamaa! Hebu tujifunze jinsi alivyofaulu kushikamana na Yehova, na jinsi tunavyoweza kumwiga.

Hezekia alijifunza kuhusu wengine ambao walishikamana na Yehova. Daudi alikuwa mmoja wao. Ingawa Daudi aliishi miaka mingi sana mapema, Hezekia angeweza kujifunza kumhusu kupitia Maandiko. Daudi aliandika: “Hata ikiwa baba yangu na mama yangu wangeniacha, Yehova mwenyewe angenichukua.”

Je, umetambua jambo lililomsaidia Daudi kumtii Yehova?— Ni imani yake! Daudi alikuwa na hakika kwamba kama angemtii Yehova, bila shaka Yehova angemsaidia. Daudi hakuwa na shaka kamwe kuhusu jambo hilo! Kwa kweli, kumfikiria Daudi kulimsaidia Hezekia ashikamane na Yehova kwa kumtii. Wewe pia unaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atakusaidia ikiwa utashikamana naye kwa kuendelea kumtii.

Namna gani ikiwa baba au mama yako hamwabudu Yehova?— Mungu anasema kwamba watoto wanapaswa kuwatii wazazi wao. Hivyo, unapaswa kuwatii wazazi wako. Hata hivyo, wazazi wako wanapokuambia ufanye jambo ambalo Mungu anasema usifanye, unaweza kuwaeleza ni kwa nini hutafanya jambo hilo. Hupaswi kudanganya, kuiba, au kufanya jambo lingine lolote baya ambalo Mungu anasema ni kosa, hata iwe ni nani anayekwambia ufanye hivyo. Kumtii Mungu ndilo jambo linalofaa!

Kuna mifano mizuri ambayo tunaweza kuiga. Mbali na Daudi, Hezekia alikuwa na mfano mwingine mzuri wa kuiga—babu yake, Yothamu. Ingawa Yothamu alikufa kabla ya Hezekia kuzaliwa, Hezekia angeweza kujifunza kumhusu, kama tu tunavyoweza kujifunza kumhusu katika Biblia. Je, unaweza kufikiria mifano mingine mizuri tunayoweza kuiga?

Ni kweli kwamba katika Biblia unaweza kujifunza kuhusu makosa fulani ambayo Hezekia, Daudi, Yothamu, na watu wengine ambao hawakuwa wakamilifu walifanya. Lakini wote hao walimpenda Yehova, walikubali makosa yao, na kujitahidi kufanya mambo yaliyokuwa sawa. Kumbuka kwamba Yesu, Mwana wa Mungu, ndiye tu aliyekuwa mkamilifu. Na tuendelee kujifunza hasa kumhusu na kujitahidi kuiga mfano wake.

^ fu. 3 Kama unasoma sehemu hii pamoja na mtoto, unapoona kistari kama hiki (—), tua na umtie mtoto moyo atoe maoni yake.