Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wasomaji Wetu Wanauliza . . .

Je, Utatu Ni Fundisho la Biblia?

Je, Utatu Ni Fundisho la Biblia?

▪ Fundisho la Utatu limefafanuliwa kwa njia nyingi, na moja kati ya ufafanuzi huo ni: “Miungu mitatu (Baba, Mwana, na Roho Mtakatifu), na kila mmoja anasemekana kuwa anaishi milele, ni mweza yote, na hakuna aliye mdogo au mkuu kuliko mwingine. Pia, kila mmoja anasemekana kuwa Mungu, na bado wote ni Mungu mmoja.” Je, hili ni fundisho la Biblia?

Kwa kawaida andiko la Mathayo 28:19 hutumiwa kuthibitisha fundisho hilo. Katika tafsiri ya Union Version andiko hili linatafsiriwa hivi: “Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na la Mwana, na Roho Mtakatifu.” Ni kweli kwamba maneno Baba, Mwana, na roho mtakatifu (roho takatifu) yanatajwa katika andiko hilo. Hata hivyo, andiko hilo halisemi kwamba wote ni kitu kimoja. Yesu alikuwa akiwaagiza wafuasi wake Wayahudi wawafundishe watu na kuwabatiza katika jina la Baba, Mwana, na roho takatifu. Wayahudi waliamini nini wakiwa taifa?

Wakati taifa la Israeli lilipopokea agano la Sheria, ambalo ni sehemu ya Biblia, waliamuriwa hivi: “Usiwe kamwe na miungu mingine dhidi ya uso wangu.” (Kumbukumbu la Torati 5:7) Ni miungu mingapi inayozungumza hapa? Andiko la Kumbukumbu la Torati 6:4 linataja hivi waziwazi: “Sikiliza, Ee Israeli: Yehova Mungu wetu ni Yehova mmoja”—si watatu katika mmoja. Taifa la Israeli lilikuwa limetoka tu kukombolewa kutoka Misri ambako miungu Osirisi, Isisi, na Horusi (inayoonyeshwa kushoto) iliabudiwa ikiwa mojawapo ya vikundi kadhaa vya miungu mitatu-mitatu. Hivyo, taifa la Israeli lilipewa amri ya kuabudu Mungu mmoja tu. Je, ilikuwa muhimu kwa watu kuelewa amri hiyo? Kulingana na Dakt. J. H. Hertz, ambaye ni rabi: “Tamko hilo lililo wazi la kuabudu Mungu mmoja tu lilikuwa tangazo la vita dhidi ya kuabudu miungu mingi . . . Katika njia hiyohiyo, Shema haitii ndani fundisho la utatu la imani ya Kikristo kwa kuwa linapinga Umoja wa Mungu.” *

Kwa kuwa Yesu alizaliwa akiwa Myahudi, aliagizwa afuate amri hiyohiyo. Baada ya kubatizwa, alipojaribiwa na Ibilisi, alisema: “Nenda zako, Shetani! Kwa maana imeandikwa, ‘Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.’” (Mathayo 4:10; Kumbukumbu la Torati 6:13) Tunaweza kujifunza angalau mambo mawili kutokana na kisa hicho. Kwanza, Shetani alikuwa akijaribu kumshawishi Yesu aabudu mungu mwingine mbali na Yehova, jaribu ambalo halingekuwa na maana yoyote kama Yesu angekuwa sehemu ya Mungu huyohuyo. Pili, Yesu alieleza waziwazi kwamba kuna Mungu mmoja tu anayepaswa kuabudiwa alipotumia maneno “yeye peke yake,” bali si “sisi,” neno ambalo angetumia kama angekuwa sehemu ya Utatu.

Watu wanapopata ujuzi sahihi kumhusu Mungu na wanataka kumtumikia, wao hubatizwa “katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu.” (Mathayo 28:19) Wanaelewa na wanakubali mamlaka ya Yehova na jukumu la Yesu Kristo katika kutimizwa kwa kusudi la Yehova. (Zaburi 83:18; Mathayo 28:18) Pia, wanatambua kazi na utendaji wa roho takatifu ya Mungu, ambayo ni nguvu yake ya utendaji.—Mwanzo 1:2; Wagalatia 5:22, 23; 2 Petro 1:21.

Watu wamechanganyikiwa kuhusu fundisho la Utatu kwa muda mrefu. Kwa upande mwingine, Yesu aliwafunulia wafuasi wake yule “Mungu wa pekee wa kweli,” Yehova na akawaongoza Kwake.—Yohana 17:3.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Kuungama kwamba Mungu ni mmoja kama inavyotajwa katika Shema, sala ambayo inategemea Kumbukumbu la Torati 6:4, ni sehemu muhimu ya ibada katika sinagogi.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 23]

Musée du Louvre, Paris