Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mkaribie Mungu

“Mambo ya Zamani Hayatakumbukwa Akilini”

“Mambo ya Zamani Hayatakumbukwa Akilini”

KUMBUKUMBU zinaweza kuwa baraka. Inachangamsha moyo kukumbuka pindi nzuri tulizofurahia pamoja na wapendwa wetu. Lakini katika visa vingine, kumbukumbu zinaweza kuwa kama laana. Je, unasumbuliwa na kumbukumbu zenye kuumiza za mambo mabaya yaliyokupata wakati uliopita? Ikiwa ndivyo, huenda ukajiuliza, ‘Je, kumbukumbu hizo zenye kuumiza zitatoka akilini mwangu?’ Tunapata jibu lenye kutia moyo sana katika maneno ya nabii Isaya.—Soma Isaya 65:17.

Yehova anakusudia kuondoa kabisa chanzo cha kumbukumbu zenye kuumiza. Namna gani? Kwa kuuondoa ulimwengu huu mwovu pamoja na mateso yaliyomo na badala yake kuleta hali bora zaidi. Yehova anaahidi hivi kupitia Isaya: “Mimi ninaumba mbingu mpya na dunia mpya.” Kuelewa ahadi hiyo kunaweza kujaza mioyo yetu tumaini.

Mbingu mpya ni nini? Biblia inatoa madokezo mawili yanayoweza kutusaidia. Kwanza, wazo la mbingu mpya linatajwa na waandikaji wengine wawili wa Biblia, na katika visa vyote viwili mbingu mpya zinahusianishwa na mabadiliko makubwa yatakayotokea duniani. (2 Petro 3:13; Ufunuo 21:1-4) Pili, katika Biblia neno “mbingu” linaweza kuwakilisha utawala, au serikali. (Isaya 14:4, 12; Danieli 4:25, 26) Hivyo basi, mbingu mpya ni serikali mpya, ambayo ina uwezo wa kuleta hali zenye uadilifu duniani. Kuna utawala mmoja tu unaoweza kutimiza mambo hayo yote. Utawala huo ni Ufalme wa Mungu, yaani, serikali ya mbinguni ambayo Yesu alitufundisha tusali ije. Ufalme huo utafanya mapenzi ya Mungu ya uadilifu yatendeke katika dunia yote.—Mathayo 6:9, 10.

Dunia mpya ni nini? Fikiria mambo mawili yanayotajwa katika Maandiko ambayo yanatusaidia kufikia uamuzi unaofaa. Kwanza, katika Biblia nyakati nyingine neno “dunia” linarejelea watu, si dunia sayari. (Zaburi 96:1) Pili, Biblia ilitabiri kwamba chini ya utawala wa Mungu, wanadamu waaminifu watajifunza uadilifu, sifa ambayo itaenea duniani kote. (Isaya 26:9) Kwa hiyo, dunia mpya inarejelea jamii ya watu ambao watajitiisha chini ya utawala wa Mungu na kuishi kupatana na viwango vyake vya uadilifu.

Je, unaweza kuanza kuwazia jinsi Yehova atakavyoondoa chanzo cha kumbukumbu zenye kuumiza? Hivi karibuni, Yehova atatimiza kikamili ahadi yake ya mbingu mpya na dunia mpya na kuleta ulimwengu mpya wenye uadilifu. * Katika ulimwengu huo mpya, mambo yanayosababisha kumbukumbu zenye kuumiza—maumivu ya kimwili, kiakili, na kihisia—hayatakuwapo tena. Wanadamu waaminifu watafurahia maisha kikamili, na kila siku watafurahia kumbukumbu zenye kupendeza.

Namna gani mambo yenye kuumiza kihisia ambayo huenda tunakabili sasa? Ahadi ya Yehova kupitia Isaya inaendelea kusema: “Mambo ya zamani hayatakumbukwa akilini, wala hayataingia moyoni.” Hali yoyote yenye kuumiza ambayo huenda imetupata katika ulimwengu huu wa kale hatimaye itasahaulika. Je, unapendezwa na matazamio hayo? Ikiwa ndivyo, tunakutia moyo uchunguze jinsi unavyoweza kumkaribia Mungu ambaye anaahidi wakati ujao mzuri.

Usomaji wa Biblia unaopendekezwa kwa mwezi wa Machi:

Isaya 63-66Yeremia 1-16

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Kwa habari zaidi kuhusu Ufalme wa Mungu na yale utakayotimiza hivi karibuni, ona sura ya  3, 8, na 9 kwenye kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Blabu katika ukurasa wa 19]

Yehova anakusudia kuondoa kabisa chanzo cha kumbukumbu zenye kuumiza