Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Muwe na Upendo Kati Yenu Wenyewe’

‘Muwe na Upendo Kati Yenu Wenyewe’

‘Muwe na Upendo Kati Yenu Wenyewe’

“Ninawapa ninyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile ambavyo nimewapenda ninyi, ninyi nanyi mpendane vivyo hivyo. Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.”—YOHANA 13:34, 35.

Inamaanisha Nini? Kristo aliwaambia wafuasi wake wapendane jinsi alivyowapenda. Yesu aliwapenda jinsi gani? Aliwapenda watu ijapokuwa siku hizo ubaguzi wa kitaifa na kijinsia ulikuwa umeenea sana. (Yohana 4:7-10) Upendo ulimchochea Yesu kudhabihu wakati, nguvu, na pindi zake za kustarehe ili kusaidia wengine. (Marko 6:30-34) Mwishowe, Kristo alionyesha upendo kwa njia iliyo kubwa zaidi. Alisema: “Mimi ndiye mchungaji mwema; mchungaji mwema huitoa nafsi yake kwa ajili ya kondoo.”—Yohana 10:11.

Wakristo wa Mapema Walifanyaje Hivyo? Katika karne ya kwanza, Wakristo waliitana “ndugu” au “dada.” (Filemoni 1, 2) Watu wa mataifa yote walikaribishwa katika kutaniko la Kikristo, kwa maana waliamini kwamba “hakuna tofauti kati ya Myahudi na Mgiriki, kwa maana kuna Bwana yuleyule juu ya wote.” (Waroma 10:11, 12) Baada ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., wanafunzi huko Yerusalemu “wa[li]anza kuuza miliki na mali zao na kuwagawia wote mapato hayo, kulingana na vile yeyote alivyokuwa na uhitaji.” Kwa kusudi gani? Ili wale ambao walikuwa wametoka tu kubatizwa wakae Yerusalemu na kuendelea “kujitoa wenyewe kwa fundisho la mitume.” (Matendo 2:41-45) Ni nini kilichowachochea wafanye hivyo? Miaka isiyozidi 200 baada ya kifo cha mitume, Tertullian alinukuu mambo ambayo watu walisema kuhusu Wakristo: “Ona jinsi wanavyopendana . . . na jinsi walivyo tayari kufa kwa ajili ya mmoja na mwenzake.”

Ni Nani Wanaofanya Hivyo Leo? Kitabu The History of the Decline and Fall of the Roman Empire (1837) kinasema kwamba kwa karne nyingi watu wanaodai kuwa Wakristo “wametendeana kwa ukatili sana kuliko jinsi walivyotendewa na watu wasioamini.” Uchunguzi uliofanywa hivi karibuni huko Marekani ulifunua uhusiano mkubwa kati ya watu wanaofuata dini—wengi wao wakidai kuwa Wakristo—na ubaguzi wa kijamii. Katika nchi fulani, mara nyingi wafuasi wa dini fulani hawawafahamu wafuasi wa dini hiyohiyo wanaoishi katika nchi nyingine, na hivyo hawawezi au hawako tayari kuwasaidia waamini wenzao kunapokuwa na uhitaji.

Mwaka wa 2004, baada ya jimbo la Florida kukumbwa na vimbunga vinne katika kipindi cha miezi miwili, mwenyekiti wa Halmashauri ya Kushughulikia Hali ya Dharura huko Florida alifanya uchunguzi ili kuhakikisha kwamba misaada iliyotolewa ilitumiwa ifaavyo. Alisema kwamba hakuna kikundi kingine kilichokuwa na utaratibu kuliko Mashahidi wa Yehova, hivyo akajitolea kutoa misaada ambayo Mashahidi wangehitaji. Mapema katika mwaka wa 1997, kikundi cha wajitoleaji cha Mashahidi wa Yehova kilichokuwa kimebeba madawa, vyakula, na mavazi kilisafiri kwenda Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ili kuwasaidia ndugu zao Wakristo na watu wengine wenye uhitaji. Mashahidi wenzao barani Ulaya walikuwa wametoa michango mbalimbali yenye thamani ya dola zaidi ya milioni moja za Marekani.