Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Si Sehemu ya Ulimwengu”

“Si Sehemu ya Ulimwengu”

“Si Sehemu ya Ulimwengu”

“Ulimwengu umewachukia, kwa sababu wao si sehemu ya ulimwengu.”—YOHANA 17:14.

Inamaanisha Nini? Yesu hakuwa sehemu ya ulimwengu, hivyo hakuunga mkono upande wowote wa mizozo ya kijamii na kisiasa katika siku zake. Alisema hivi: “Kama ufalme wangu ungekuwa sehemu ya ulimwengu huu, watumishi wangu wangepigana ili nisitiwe mikononi mwa Wayahudi. Lakini, kama ilivyo, ufalme wangu hautoki katika chanzo hiki.” (Yohana 18:36) Pia, aliwahimiza wafuasi wake waepuke mitazamo, usemi, na mwenendo unaoshutumiwa na Neno la Mungu.—Mathayo 20:25-27.

Wakristo wa Mapema Walifanyaje Hivyo? Kulingana na mwandishi wa mambo ya kidini, Jonathan Dymond, Wakristo wa mapema “walikataa kushiriki katika [vita]; bila kujali matokeo, iwe wangeshutumiwa, kufungwa gerezani, au kufa.” Walichagua kuteseka badala ya kuunga mkono upande wowote. Maadili yao yaliwafanya wawe tofauti pia. Wakristo waliambiwa: “Kwa sababu ninyi hamwendelei kukimbia pamoja nao katika mwendo huo kwenda kwenye dimbwi lilelile la chini la upotovu, wao wanashangaa na kuendelea kuwatukana ninyi.” (1 Petro 4:4) Mwanahistoria, Will Durant aliandika kwamba Wakristo “walisumbua dhamiri ya ulimwengu huo wa kipagani uliopenda anasa kwa sababu walimwogopa Mungu na walikuwa na mwenendo safi kiadili.”

Ni Nani Wanaofanya Hivyo Leo? Kitabu New Catholic Encyclopedia kinasema hivi kuhusu msimamo wa Wakristo wa kutounga mkono upande wowote: “Kupatana na maadili, ni hatia kukataa kushiriki vita kwa sababu ya dhamiri.” Makala moja katika gazeti Reformierte Presse inasema kwamba ripoti ya shirika fulani la haki za kibinadamu (African Rights) kuhusu maangamizi ya jamii nzima-nzima huko Rwanda mwaka wa 1994, ilionyesha kwamba dini zote zilihusika, “isipokuwa Mashahidi wa Yehova.”

Akizungumza kuhusu yale Maangamizi Makubwa ya Nazi, mwalimu mmoja wa sekondari alisema hivi kwa huzuni: “Hakuna kikundi au shirika la raia wa kawaida ambalo lilishutumu uwongo mwingi, ukatili, na uovu uliotokea.” Baada ya kuwasiliana na Jumba la Makumbusho la Maangamizi Makubwa la Marekani, aliandika hivi: “Sasa nilikuwa nimepata jibu.” Alitambua kwamba Mashahidi wa Yehova walishikamana kabisa na imani yao hata ingawa waliteswa vikali.

Namna gani maadili yao? Gazeti U.S. Catholic linasema: “Vijana wengi Wakatoliki hawakubaliani na mafundisho ya kanisa yanayopinga kuishi pamoja bila kufunga ndoa kisheria [na] kufanya ngono kabla ya ndoa.” Gazeti hilo linamnukuu mhudumu fulani wa kanisa hilo aliyesema: “Asilimia kubwa ninayoona—nadhani ni zaidi ya asilimia 50—tayari wanaishi pamoja wanapokuja kufunga ndoa kisheria.” Kitabu The New Encyclopædia Britannica kinasema kwamba Mashahidi wa Yehova “wanakazia kufuata viwango vya juu vya maadili maishani mwao.”