Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mazungumzo Pamoja na Jirani—Je, Yesu Ni Mungu?

Mazungumzo Pamoja na Jirani—Je, Yesu Ni Mungu?

Mazungumzo Pamoja na Jirani​—Je, Yesu Ni Mungu?

MASHAHIDI WA YEHOVA wanafurahia kuzungumza kuhusu Biblia pamoja na jirani zao. Je, kuna jambo lolote kuhusu Biblia ambalo limekuwa likikutatiza? Je, kuna jambo lolote ambalo Mashahidi wa Yehova wanaamini au kufanya ambalo ungependa kulifahamu zaidi? Ikiwa ndivyo, basi unapokutana tena na Shahidi wa Yehova usikose kumwuliza. Atafurahi kuzungumzia jambo hilo pamoja nawe.

Mazungumzo yafuatayo yanaonyesha jinsi Shahidi wa Yehova anavyoweza kuzungumza na jirani yake. Hebu tuwazie Shahidi anayeitwa Karen amemtembelea mwanamke anayeitwa Samantha nyumbani kwake.

Je, Ni Kweli Kwamba Ninyi Hammwamini Yesu?

Samantha: Mchungaji wetu husema kwamba Mashahidi wa Yehova hawamwamini Yesu. Je, ni kweli?

Karen: Acha nikuhakikishie kwamba tunamwamini Yesu. Hata tunaamini kwamba kumwamini Yesu ni jambo muhimu sana ili kupata wokovu.

Samantha: Mimi pia ninaamini hivyo.

Karen: Hivyo basi, hilo ni jambo ambalo mimi na wewe tunakubaliana. Jina langu ni Karen. Wewe unaitwa nani?

Samantha: Ninaitwa Samantha. Nimefurahi kukutana nawe.

Karen: Nimefurahi pia kukutana nawe, Samantha. Huenda ukajiuliza, ‘Ikiwa ni kweli kwamba Mashahidi wa Yehova wanamwamini Yesu, kwa nini watu husema hawamwamini?’

Samantha: Ndiyo, nimejiuliza swali hilo.

Karen: Samantha, kwa ufupi tunamwamini kabisa Yesu, lakini hatuamini kila kitu ambacho watu husema kumhusu.

Samantha: Unaweza kunipa mfano mmoja?

Karen: Ndiyo. Watu fulani husema kwamba Yesu alikuwa mtu mzuri tu. Lakini hatukubaliani na wazo hilo.

Samantha: Hata mimi siamini hivyo.

Karen: Basi hilo ni jambo lingine ambalo mimi na wewe tunakubaliana. Mfano wa pili ni kwamba Mashahidi wa Yehova hawakubaliani na mafundisho yanayopinga mambo ambayo Yesu mwenyewe alisema kuhusu uhusiano wake pamoja na Baba.

Samantha: Unamaanisha nini?

Karen: Dini nyingi zinafundisha kwamba Yesu ni Mungu. Labda umefundishwa hivyo.

Samantha: Ndiyo, mchungaji wetu husema kwamba Mungu ni sawa na Yesu.

Karen: Je, si ni kweli kwamba njia bora ya kujifunza ukweli kumhusu Yesu ni kwa kuchunguza mambo aliyosema kujihusu?

Samantha: Ndiyo, ninakubaliana nawe.

Yesu Alisema Nini?

Karen: Acha tuchunguze andiko fulani katika Biblia ambalo litatusaidia kuelewa jambo hili. Tafadhali ona maneno ya andiko la Yohana 6:38. Yesu alisema: “Nimeshuka kutoka mbinguni kufanya, si mapenzi yangu, bali mapenzi yake aliyenituma.” Maneno hayo yangetutatanisha ikiwa Yesu ni Mungu.

Samantha: Unamaanisha nini?

Karen: Ona kwamba Yesu alisema hakushuka kutoka mbinguni ili kufanya mapenzi yake mwenyewe.

Samantha: Ni kweli kwamba alisema alikuja kufanya mapenzi ya Yule aliyemtuma.

Karen: Lakini kama Yesu ni Mungu, ni nani aliyemtuma kutoka mbinguni? Kwa nini Yesu alitii na kufanya mapenzi ya Yule aliyemtuma?

Samantha: Ninaanza kuelewa unachomaanisha. Lakini sina uhakika kwamba andiko hilo moja linatosha kuthibitisha Yesu si Mungu.

Karen: Hata hivyo, ona maneno ambayo Yesu alisema katika pindi tofauti. Alisema maneno kama hayo katika sura inayofuata ya kitabu cha Yohana. Tafadhali soma Yohana 7:16.

Samantha: Acha nisome. “Yesu naye akawajibu na kusema: ‘Yale ninayofundisha si yangu, bali ni yake yeye aliyenituma.’”

Karen: Asante, Samantha. Kulingana na andiko hilo, je, Yesu alifundisha mawazo yake mwenyewe?

Samantha: La, alisema kwamba mafundisho yake yalitoka kwa Yule aliyemtuma.

Karen: Ni kweli. Tunajiuliza tena: ‘Ni nani aliyemtuma Yesu? Na ni nani aliyempa kweli alizofundisha?’ Je, Huyo hangekuwa mkuu kuliko Yesu? Kwa kawaida, mtu anayemtuma mwingine ana mamlaka kuliko yule anayetumwa.

Samantha: Hilo linapendeza. Sijawahi kamwe kusoma andiko hilo.

Karen: Pia, fikiria maneno ya Yesu kwenye Yohana 14:28: “Mlisikia kwamba niliwaambia, Ninaenda zangu nami nitakuja tena kwenu. Kama mngenipenda, mngeshangilia kwamba ninaenda kwa Baba, kwa sababu Baba ni mkuu kuliko mimi.” Kulingana na andiko hilo, unaweza kusema Yesu alikuwa na maoni gani kujihusu akilinganishwa na Baba?

Samantha: Alisema kwamba Baba ni mkuu kuliko yeye. Hivyo, ninadhani aliona kwamba Mungu ana mamlaka kuliko yeye.

Karen: Kweli kabisa. Ili upate mfano mwingine, ona maneno ambayo Yesu aliwaambia mitume wake kama tunavyosoma kwenye Mathayo 28:18. Andiko hilo linasema: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.” Je, Yesu alisema kwamba sikuzote alikuwa na mamlaka yote?

Samantha: Hapana, alisema kwamba alikuwa amepewa mamlaka.

Karen: Lakini kama Yesu ni Mungu, angewezaje kupewa mamlaka zaidi? Na ni nani aliyempa mamlaka hiyo?

Samantha: Nitalifikiria jambo hilo.

Yesu Alikuwa Akizungumza na Nani?

Karen: Kuna jambo lingine ambalo linatatanisha ikiwa kwa kweli Yesu ni Mungu.

Samantha: Ni jambo gani hilo?

Karen: Ni jambo tunalosoma kuhusiana na ubatizo wa Yesu. Ona simulizi lililoandikwa kwenye Luka 3:21, 22. Tafadhali soma andiko hilo.

Samantha: “Basi watu wote walipokuwa wamebatizwa, Yesu pia akabatizwa na, alipokuwa akisali, mbingu ilifunguliwa na roho takatifu katika umbo la njiwa ikashuka juu yake, na sauti ikatoka mbinguni: ‘Wewe ni Mwanangu, mpendwa; nimekukubali wewe.’”

Karen: Je, umeona jambo ambalo Yesu alikuwa akifanya alipobatizwa?

Samantha: Alikuwa akisali.

Karen: Ndiyo. Ni kweli huenda tukajiuliza, ‘Ikiwa Yesu ni Mungu, alikuwa akisali kwa nani?’

Samantha: Hilo ni swali zuri. Nitamuuliza mchungaji wetu.

Karen: Kuhusiana na jambo hilo, ona kwamba baada ya Yesu kutoka ndani ya maji, kuna mtu aliyezungumza kutoka mbinguni. Umeona alisema nini?

Samantha: Alisema kwamba Yesu ni Mwana Wake, Anampenda, na kumkubali.

Karen: Ni kweli. Lakini kama Yesu ni Mungu, ni nani aliyesema maneno hayo kutoka mbinguni?

Samantha: Sijawahi kufikiria jambo hilo.

Kwa Nini Majina “Baba” na “Mwana” Yanatumiwa?

Karen: Kuna jambo lingine ambalo tunahitaji kuchunguza: Tumesoma kwamba Yesu alizungumza na Mungu kama Baba yake wa mbinguni. Na Yesu alipobatizwa, sauti kutoka mbinguni ilimwita, Mwanangu. Kwa kweli, Yesu mwenyewe alijiita Mwana wa Mungu. Sasa, ikiwa ungetaka kunifundisha kwamba watu wawili wako sawa, ungetumia mfano gani wa uhusiano wa kifamilia ili kulinganisha jambo hilo?

Samantha: Labda, ndugu wawili.

Karen: Kweli kabisa—labda hata mapacha wanaofanana. Lakini Yesu alimwita Mungu Baba na akasema yeye ni Mwana. Basi, unafikiri Yesu alitaka tujue jambo gani?

Samantha: Ninaelewa unachomaanisha. Yesu anaeleza kwamba mmoja kati yao ni mkuu zaidi na ana mamlaka kuliko yule wa pili.

Karen: Ni kweli kabisa. Fikiria jambo hili: Umefikiria mfano huo unaofaa kabisa kuhusu kuwa sawa, mfano wa ndugu wawili au mapacha. Ikiwa kweli Yesu angekuwa Mungu, je, huoni kwamba akiwa Mwalimu Mkuu angetumia mfano kama huo, au mfano mwingine unaoeleweka vizuri hata zaidi kuhusu kuwa sawa?

Samantha: Bila shaka.

Karen: Badala yake alitumia maneno “Baba” na “Mwana” ili kueleza kuhusu uhusiano wake pamoja na Mungu.

Samantha: Umetaja jambo lenye kupendeza kwelikweli.

Wafuasi wa Mapema wa Yesu Walisema Nini?

Karen: Kabla sijaondoka, ningependa kuzungumzia jambo lingine pamoja nawe, ikiwa una wakati.

Samantha: Ndiyo, nina dakika chache.

Karen: Ikiwa Yesu ni Mungu, je, hungetazamia kwamba wanafunzi wake wangesema hivyo waziwazi?

Samantha: Inawezekana wangesema hivyo.

Karen: Hata hivyo, hakuna andiko lolote katika Biblia linalosema walifundisha jambo hilo. Badala yake, ona jambo ambalo mtume Paulo, mmoja kati ya wanafunzi wa mapema wa Yesu aliandika kwenye Wafilipi 2:9. Akieleza jambo ambalo Mungu alifanya baada ya Yesu kufa na kufufuliwa aliandika hivi: “Mungu alimpandisha [Yesu] kwenye cheo cha juu zaidi na kumpa kwa fadhili jina lililo juu ya kila jina lingine.” Kulingana na andiko hilo, Mungu alimpa Yesu nini?

Samantha: Linasema kwamba Mungu alimpandisha kwenye cheo cha juu.

Karen: Ndiyo. Lakini kama Yesu angekuwa sawa na Mungu kabla hajafa na baadaye Mungu ampandishe kwenye cheo cha juu zaidi, je, hilo halingefanya Yesu awe na cheo cha juu kuliko Mungu? Je, kuna mtu anayeweza kuwa na mamlaka kuliko Mungu?

Samantha: Hapana, haiwezekani.

Karen: Ninakubali. Basi, kulingana na uthibitisho huo wote, je, unaweza kusema kwamba Biblia inafundisha kuwa Yesu ni Mungu?

Samantha: Hapana, sioni kama ni kweli. Biblia inasema yeye ni Mwana wa Mungu.

Karen: Hilo ni kweli. Hata hivyo, Samantha, acha nikuhakikishie jambo hili, Mashahidi wa Yehova wanamheshimu sana Yesu. Tunaamini kwamba kifo chake akiwa Masihi aliyeahidiwa kilifungua njia ili wanadamu wote waaminifu waokolewe.

Samantha: Ninaamini hivyo pia.

Karen: Basi unaweza kujiuliza, ‘Tunawezaje kumwonyesha Yesu tunathamini kwamba aliutoa uhai wake kwa ajili yetu?’ *

Samantha: Nimewahi kujiuliza swali hilo.

Karen: Labda ninaweza kurudi tena ili tuzungumzie jibu kutoka katika Biblia. Je, utakuwa nyumbani wakati kama huu juma lijalo?

Samantha: Ndiyo, nitakuwapo.

Karen: Vizuri sana, tutaonana siku hiyo.

[Maelezo ya Chini]