Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wasomaji Wetu Wanauliza . . .

Ni Nani Aliyeituma ile “Nyota”?

Ni Nani Aliyeituma ile “Nyota”?

▪ Je, umewahi kuona michezo ya kuigiza ambayo inawaonyesha wafalme watatu, au wanaume wenye hekima, wakimtembelea mtoto aliyetoka kuzaliwa, Yesu, akiwa amelazwa ndani ya hori? Kulingana na hadithi hiyo, Mungu alitumia nyota kuwaongoza kwenye zizi fulani lililokuwa Bethlehemu. Hata watoto wengi wamekariri majina ya wafalme hao watatu, yaani, Melchior, Caspar, na Baltazar. Hata hivyo, je, hadithi hiyo inayojulikana sana inapatana na yale ambayo Biblia inasema? Hapana. Kwa kuwa katika njia nyingi, hadithi hiyo sio sahihi.

Kwanza, wanaume hao walikuwa akina nani? Katika Kigiriki cha awali, Biblia haiwataji kuwa wafalme wala wanaume wenye hekima. Walikuwa mamajusi au wanajimu. Kwa hakika wanaume hao walitumia ufundi wa kipagani wa kufanya uaguzi uliotegemea kutazama nyota. Masimulizi ya Biblia hayataji majina wala idadi ya wageni hao.

Pili, wanaume hao walikuja wakati gani? Si wakati Yesu alipokuwa mtoto katika hori. Tunajuaje jambo hilo? Mathayo, mwandikaji wa Injili alisema: “Walipoingia ndani ya ile nyumba wakamwona huyo mtoto mchanga pamoja na Maria mama yake.” (Mathayo 2:11) Ona kwamba Yesu hakuwa mtoto aliyetoka tu kuzaliwa, bali alikuwa “mtoto mchanga.” Kufikia wakati huo, Maria na Yosefu hawakuwa wakiishi katika zizi; badala yake, walikuwa wakiishi ndani ya nyumba.

Tatu, ni nani aliyeituma ile “nyota” iwaongoze wanajimu hao? Kwa kawaida, viongozi wa kidini hufundisha kwamba Mungu ndiye aliyeituma ile “nyota.” Je, kweli alifanya hivyo? Kumbuka ile “nyota” haikuwaongoza wanajimu hao kwenda Bethlehemu kwanza. Badala yake, iliwaelekeza kwa Mfalme Herode huko Yerusalemu. Walimwambia mfalme huyo mwenye wivu na muuaji mwenye nguvu kuhusu Yesu na hata wakamfanya awe na sababu ya kumchukia mtoto huyo ambaye angekuwa “mfalme wa Wayahudi.” (Mathayo 2:2) Kwa ujanja, Herode aliwaambia warudi kwake ili wamweleze mahali hususa ambapo mtoto huyo alikuwa, akidai kwamba yeye pia alitaka kumfanyia tendo la heshima. Kisha, ile “nyota” ikawaongoza wale wanajimu kwa Yosefu na Maria. Hivyo, jambo ambalo wanajimu hao walikuwa wakifanya lingesababisha kifo cha yule mtoto mdogo ikiwa Mungu hangeingilia kati. Inapendeza kwamba Mungu aliingilia kati. Kwa kuwa wale wanajimu hawakurudi, Herode alishikwa na ghadhabu sana hivi kwamba akaamuru wavulana wote wenye umri wa miaka miwili kwenda chini huko Bethlehemu na maeneo yaliyo karibu wauawe.—Mathayo 2:16.

Baadaye, Yehova alimwita Yesu “Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.” (Mathayo 3:17) Fikiria jambo hili: Je, Baba huyo mwenye upendo na mwadilifu angechagua wanajimu hao wapagani waliofanya uaguzi, jambo ambalo alilikataza katika Sheria yake, wawe wajumbe wake? (Kumbukumbu la Torati 18:10) Je, angetumia nyota kuwaongoza kwa muuaji hatari na mwenye nguvu zaidi katika nchi hiyo, wakiwa na ujumbe ambao bila shaka ungemfanya Herode awe na wivu wenye chuki? Je, baadaye Mungu angetumia wanajimu hao na nyota ileile kufunua mahali ambapo mwana wake mchanga alikuwa?

Kwa mfano: Kamanda wa jeshi mwenye ustadi anamtuma askari-jeshi wake aliye bora zaidi kwenye safari hatari katika eneo la adui. Je, anaweza kumfunulia adui mahali ambapo atampata huyo askari-jeshi? Bila shaka hawezi! Vivyo hivyo, Yehova alimtuma mwana wake katika ulimwengu huu hatari. Je, angemfunulia Mfalme Herode mwovu mahali ambapo Mwana Wake alikuwa akiishi pasipo ulinzi wowote? Haiwezekani!

Hivyo basi, ni nani aliyeituma ile “nyota,” au kile kitu kilichofanana na nyota? Ni nani aliyetaka sana Yesu auawe, na hivyo kumzuia asikue na kutimiza kazi aliyokusudiwa kuifanya duniani? Ni nani anayejaribu kuwadanganya wanadamu na kuendeleza uwongo, jeuri, na mauaji? Yesu mwenyewe alimtambulisha huyo ‘mwongo na baba ya uwongo,’ ambaye alikuwa “muuaji alipoanza,” yaani, Shetani Ibilisi.​—Yohana 8:44.