Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yesu Kristo—Maswali Yetu Yajibiwa

Yesu Kristo—Maswali Yetu Yajibiwa

Yesu Kristo​—Maswali Yetu Yajibiwa

“Umati unasema mimi ni nani?”​LUKA 9:18.

YESU aliwauliza wanafunzi wake swali hilo kwa sababu alijua watu walikuwa na maoni yaliyotofautiana kumhusu. Hata hivyo, hakukuwa na sababu nzuri ya kutatanishwa na jambo hilo. Yesu hakujitenga na watu wala kutenda kisirisiri. Badala yake alishirikiana na watu waziwazi katika miji na vijiji. Alihubiri na kufundisha hadharani kwa sababu alitaka watu wamjue.—Luka 8:1.

Maneno na matendo ya Yesu yanatusaidia kujua ukweli kumhusu. Mambo hayo yanazungumziwa katika vitabu vya Injili vya Biblia, yaani, Mathayo, Marko, Luka, na Yohana. Vitabu hivyo vilivyoongozwa na roho ya Mungu ndio msingi wa kujibu maswali yetu yanayomhusu Yesu. *​—Yohana 17:17.

SWALI: Je, kweli Yesu ni mtu aliyeishi zamani?

JIBU: Ndiyo. Wanahistoria kama vile Yosefo na Tasito walioishi katika karne ya kwanza walisimulia kuhusu maisha ya Yesu. Uthibitisho bora zaidi unapatikana katika vitabu vya Injili. Vitabu hivyo vinaonyesha wazi Yesu hakuwa mtu wa kuwaziwa tu. Vinataja mahali na wakati hususa wa matukio yanayosimuliwa. Kwa mfano, ili kuonyesha mwaka ambao Yesu alianza huduma yake Luka, mwandikaji wa kitabu cha Injili, alitaja watu saba waliokuwa mamlakani wakati huo, na wanahistoria wamethibitisha mambo hayo.—Luka 3:1, 2, 23.

Kuna uthibitisho usioweza kupingwa unaoonyesha kwamba Yesu ni mtu aliyeishi zamani. Kitabu kinachozungumzia uthibitisho wa kuwapo kwa Yesu (Evidence for the Historical Jesus) kinasema: “Wasomi wengi wanakubali kwamba mtu aliyeitwa Yesu wa Nazareti aliishi katika karne ya kwanza.”

SWALI: Je, Yesu ni Mungu?

JIBU: La. Yesu hakujiona kamwe kuwa sawa na Mungu. Nyakati zote, Yesu alionyesha kwamba alikuwa cheo cha chini kuliko Yehova. * Kwa mfano, alimwita Yehova “Mungu wangu” na “Mungu wa pekee wa kweli.” (Mathayo 27:46; Yohana 17:3) Yesu alipotumia maneno hayo alionyesha kwamba ana cheo cha chini kuliko Baba yake. Bila shaka, mfanyakazi ambaye anamwita mwajiri wake “mkubwa wangu” au “msimamizi” anajiona kuwa mwenye cheo cha chini kuliko mwajiri wake.

Yesu alionyesha pia kwamba yeye ni tofauti na Mungu. Wakati fulani Yesu aliwaambia wapinzani ambao walipinga mamlaka yake hivi: “Katika Sheria yenu wenyewe imeandikwa, ‘Ushahidi wa watu wawili ni wa kweli.’ Mimi ninatoa ushahidi juu yangu mwenyewe, na Baba aliyenituma hutoa ushahidi juu yangu.” (Yohana 8:17, 18) Bila shaka, Yesu ni tofauti na Yehova. La sivyo, wangewezaje kuonwa kuwa mashahidi wawili? *

SWALI: Je, Yesu alikuwa mtu mzuri tu?

JIBU: Hapana. Yesu alitambua majukumu yake muhimu kuhusiana na kutimizwa kwa mapenzi ya Mungu. Baadhi ya majukumu hayo ni:

“Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu.” (Yohana 3:18) Yesu alijua chanzo chake. Aliishi mbinguni kwa muda mrefu kabla ya kuzaliwa duniani. Alisema hivi: “Nimeshuka kutoka mbinguni.” (Yohana 6:38) Yesu ndiye aliyeumbwa kwanza na Mungu na alisaidia kuumba vitu vingine vyote. Kwa kufaa, Yesu anaitwa “Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu” kwa sababu yeye pekee ndiye aliyeumbwa na Mungu moja kwa moja.—Yohana 1:3, 14; Wakolosai 1:15, 16.

“Mwana wa binadamu.” (Mathayo 8:20) Mara nyingi, Yesu alijiita “Mwana wa binadamu.” Usemi huo unapatikana zaidi ya mara 80 katika vitabu vya Injili. Usemi huo unaonyesha kwamba Yesu alikuwa mwanadamu halisi na si Mungu katika mwili wa binadamu. Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu alizaliwa kama binadamu jinsi gani? Yehova alitumia roho takatifu kuhamisha uhai wa Mwana wake kutoka mbinguni na kuuweka katika tumbo la uzazi la bikira Myahudi Maria, na hivyo akapata mimba. Kwa hiyo, Yesu alizaliwa bila dhambi na alikuwa binadamu mkamilifu.—Mathayo 1:18; Luka 1:35; Yohana 8:46.

“Mwalimu.” (Yohana 13:13) Yesu alionyesha waziwazi kwamba kazi aliyopewa na Mungu ilikuwa ‘kufundisha na kuhubiri habari njema’ ya Ufalme wa Mungu. (Mathayo 4:23; Luka 4:43) Kwa njia rahisi na yenye kueleweka alieleza Ufalme wa Mungu ni nini na jinsi utakavyotimiza mapenzi ya Yehova.—Mathayo 6:9, 10.

“Neno.” (Yohana 1:1) Yesu alikuwa Msemaji wa Mungu, kwa maana alitumiwa na Mungu kuwasilisha habari na maagizo kwa wengine. Yehova alimtumia kufikisha ujumbe Wake kwa wanadamu duniani.—Yohana 7:16, 17.

SWALI: Je, Yesu alikuwa Masihi aliyeahidiwa?

JIBU: Ndiyo. Biblia ilitabiri kwamba Masihi, au Kristo, angekuja. Majina hayo mawili yanamaanisha “Mtiwa-Mafuta.” Masihi huyo aliyeahidiwa angetimiza majukumu muhimu katika kusudi la Yehova. Wakati fulani, mwanamke Msamaria alimwambia Yesu: “Ninajua kwamba Masihi anakuja, anayeitwa Kristo.” Ndipo Yesu alipomwambia waziwazi: “Mimi ninayesema nawe ndiye.”—Yohana 4:25, 26.

Je, kuna uthibitisho wowote kwamba Yesu ndiye Masihi? Ndiyo, kuna mambo matatu ambayo yanapochunguzwa pamoja yanatoa uthibitisho wenye kusadikisha. Mambo hayo ni kama alama za vidole zinazomtambulisha mtu mmoja tu. Je, Yesu alionyesha alama hizo? Fikiria mambo yafuatayo:

Nasaba yake. Biblia ilitabiri Masihi angekuwa uzao wa Abrahamu kupitia nasaba au ukoo wa Daudi. (Mwanzo 22:18; Zaburi 132:11, 12) Yesu alikuwa uzao wa Abrahamu na wa Daudi pia.—Mathayo 1:1-16; Luka 3:23-38.

Unabii uliotimia. Maandiko ya Kiebrania yana unabii mwingi unaohusu maisha ya Masihi duniani, kama vile kuzaliwa kwake na kifo chake. Unabii huo wote ulitimia katika maisha ya Yesu. Baadhi yake ni: Alizaliwa Bethlehemu (Mika 5:2; Luka 2:4-11), aliitwa kutoka Misri (Hosea 11:1; Mathayo 2:15), na aliuawa bila mifupa yake kuvunjwa (Zaburi 34:20; Yohana 19:33, 36). Yesu hakuwa na namna yoyote ya kupanga matukio ya maisha yake ili yapatane na unabii wote unaomhusu Masihi. *

Ushahidi uliotolewa na Mungu mwenyewe. Baada ya kuzaliwa kwa Yesu, Mungu aliwatuma malaika kuwaeleza wachungaji kwamba Masihi alikuwa amezaliwa. (Luka 2:10-14) Mara kadhaa katika huduma ya Yesu, Mungu mwenyewe alisema kutoka mbinguni, akionyesha kwamba amemkubali Yesu. (Mathayo 3:16, 17; 17:1-5) Isitoshe, ili kuthibitisha Yesu ni Masihi, Yehova alimpa uwezo wa kufanya miujiza.—Matendo 10:38.

SWALI: Kwa nini ilikuwa lazima Yesu ateseke na kufa?

JIBU: Yesu hakustahili kufa kwa sababu hakuwa na dhambi, wala hakustahili kutundikwa mtini kama mhalifu na kuachwa afe kifo cha aibu. Hata hivyo, Yesu alitarajia kwamba angetendewa vibaya na alikuwa tayari kuvumilia mateso hayo.—Mathayo 20:17-19; 1 Petro 2:21-23.

Unabii ulionyesha kwamba Masihi angeteswa na kuuawa ili kufunika dhambi za wanadamu. (Isaya 53:5; Danieli 9:24, 26) Yesu mwenyewe alisema alikuja ili ‘kutoa nafsi yake kuwa fidia kwa ajili ya wengi.’ (Mathayo 20:28) Watu wote wanaoamini kwamba kifo cha Yesu kina uwezo wa kukomboa, wanatumaini la kuwekwa huru kutoka katika dhambi na kifo na kuishi milele katika Paradiso duniani. *Yohana 3:16; 1 Yohana 4:9, 10.

SWALI: Je, kweli tunaweza kuamini Yesu alifufuliwa?

JIBU: Ndiyo. Yesu aliamini kabisa kwamba angefufuliwa. (Mathayo 16:21) Hata hivyo, Yesu mwenyewe na waandikaji wa Biblia hawakudai kamwe angefufuliwa bila msaada wa Mungu. Jambo hilo halingeaminika. Badala yake Biblia inasema hivi: “Mungu alimfufua kwa kuyafungua maumivu makali ya kifo.” (Matendo 2:24) Iwapo tunaamini kuna Mungu ambaye ameviumba vitu vyote, basi tuna kila sababu ya kuamini kwamba alikuwa na uwezo wa kumfufua Mwana wake.—Waebrania 3:4.

Je, kuna uthibitisho unaoonyesha kwamba Yesu alifufuliwa? Zingatia habari zifuatazo.

Ushahidi wa watu waliomwona. Miaka 22 hivi baada ya kifo cha Yesu, mtume Paulo aliandika kwamba watu zaidi ya 500 waliomwona Yesu aliyekuwa amefufuliwa, na wengi wao walikuwa hai wakati Paulo alipoandika maneno hayo. (1 Wakorintho 15:6) Huenda ushahidi wa mtu mmoja au wawili ukapuuzwa, lakini ni vigumu kupuuza ushahidi wa watu 500.

Mashahidi wenye kuaminika. Wanafunzi wa Yesu walioishi katika karne ya kwanza ambao walijua mambo hususa yaliyotukia, walitangaza kwa ujasiri ufufuo wa Yesu. (Matendo 2:29-32; 3:13-15) Waliona ufufuo kuwa fundisho muhimu kwa Wakristo. (1 Wakorintho 15:12-19) Wanafunzi hao walikuwa tayari kufa badala ya kukana imani yao katika Yesu. (Matendo 7:51-60; 12:1, 2) Ungemwonaje mtu yeyote ambaye angekuwa tayari kufa ili kutetea uwongo?

Tumechunguza majibu ya Biblia ya maswali sita muhimu kumhusu Yesu. Majibu yote hayo yanatueleza wazi Yesu ni nani. Lakini je, majibu hayo yana umuhimu wowote? Au mambo ambayo wewe unaamini kumhusu Yesu ni muhimu?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Ili kupata habari zaidi kuhusu jinsi vitabu vya Injili vya Biblia vinavyotofautiana na vitabu ambavyo vinadaiwa kuwa sehemu ya Biblia, ona makala “Injili za Apokrifa​—Je, Zina Ukweli Uliofichwa Kumhusu Yesu?” kwenye ukurasa wa 18-19.

^ fu. 9 Katika Biblia, Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu.

^ fu. 10 Ili kupata habari zaidi, ona makala “Mazungumzo Pamoja na Jirani​—Je, Yesu Ni Mungu?” katika ukurasa wa 20-22.

^ fu. 21 Ona orodha inayoonyesha unabii mbalimbali uliotimia kumhusu Yesu kwenye ukurasa wa 200 wa kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?

^ fu. 25 Ili kupata habari zaidi kuhusu jinsi kifo cha Yesu kinavyoweza kutukomboa, ona sura ya 5 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?