Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mkaribie Msikiaji wa Sala

Mkaribie Msikiaji wa Sala

Mkaribie Msikiaji wa Sala

WATU wengi wanaodai kwamba wanaamini kuna Mungu hawawezi kuthibitisha kwa nini wana imani. Wala hawawezi kueleza kwa nini mara nyingi dini inatenda mabaya au kwa nini Mungu anaruhusu watu wateseke. Jambo wanaloweza tu kufanya ni kusali kwa Mungu ambaye hawamwelewi.

Hata hivyo, wewe unaweza kumkaribia Mungu hata zaidi. Unaweza kujenga imani yako juu ya msingi wa kumwelewa Mungu na hivyo kumpenda na kumthamini. Imani ya kweli inategemea mambo yaliyothibitishwa. (Waebrania 11:1) Ukijifunza ukweli kumhusu Mungu, unaweza kumjua na kuzungumza naye kama rafiki. Fikiria mambo ambayo watu fulani waliokuwa wakisali walijionea ingawa walikuwa na shaka ikiwa kuna Mungu.

Patricia aliyetajwa katika makala ya kwanza. “Siku moja nilikuwa na marafiki wangu kumi hivi tulipoanza kuzungumzia mambo ya dini. Niliwaambia kwamba niliondoka nyumbani ili kuhepa mazungumzo kati ya Shahidi mmoja wa Yehova aliyetutembelea nyumbani na baba yangu, ambaye hakuamini kuna Mungu. ‘Labda Mashahidi wa Yehova wana ukweli,’ akasema rafiki yangu mmoja.

“‘Kwa nini tusihudhurie mikutano yao ili tujionee? ’ akasema mwingine. Na hivyo ndivyo tulivyofanya. Ingawa tulikuwa na shaka, baadhi yetu tuliendelea kuhudhuria kwa sababu tu Mashahidi walituonyesha urafiki.

“Hata hivyo, Jumapili moja nilisikia jambo ambalo lilibadili mtazamo wangu. Msemaji alifafanua kwa nini watu huteseka. Sikuwahi kuwazia mbeleni kwamba mwanadamu aliumbwa mwanzoni akiwa mkamilifu na kwamba dhambi na kifo kilianza na mwanadamu mmoja na kuenea kwa wanadamu wote. Vilevile, msemaji alieleza kwa nini kifo cha Yesu kilihitajika ili kuwarudishia wanadamu hali ambayo mwanadamu wa kwanza alipoteza. * (Waroma 5:​12, 18, 19) Kwa ghafula, nilianza kuelewa kila kitu. ‘Kwa kweli kuna Mungu anayetujali,’ nikawaza. Niliendelea kujifunza Biblia na baada ya muda, kwa mara ya kwanza katika maisha yangu, nikatambua kwamba ningeweza kusali kwa Mungu aliye halisi.”

Allan, aliyetajwa pia katika makala ya kwanza. “Siku moja Mashahidi wa Yehova walitutembelea nyumbani, na mke wangu akawakaribisha kwa sababu alipendezwa na mambo waliyosema kuhusu kuishi milele duniani. Nilikasirika. Hivyo, nikawaacha wageni sebuleni na nikamwita mke wangu jikoni na kumwambia, ‘Usiwe mpumbavu. Huwezi kuamini mambo kama hayo! ’

“‘Basi, wewe rudi na uwathibitishie kwamba mambo wanayosema ni ya uwongo,’ akanijibu.

“Bila shaka, sikuwa na uthibitisho wowote. Lakini walikuwa wenye fadhili sana na wakaniachia kitabu ambacho kinafafanua ikiwa uhai ulitokana na uumbaji au mageuzi. Maelezo yake yalikuwa wazi na yenye kupatana na akili hivi kwamba nikaamua ninahitaji kujua mengi zaidi kumhusu Mungu. Nilianza kujifunza Biblia na Mashahidi, na muda si muda nikatambua kwamba mambo ambayo Biblia ilisema ni tofauti kabisa na mambo niliyowazia kuhusu dini. Nilipoendelea kujifunza kumhusu Yehova, nilianza kusali kwake nikimweleza mambo hususa. Nilikuwa na mitazamo fulani mibaya, hivyo, nilisali nikiomba msaada. Nina hakika kwamba Yehova alijibu sala zangu.”

Andrew, anayeishi Uingereza. “Ingawa nilishikilia sana maoni fulani na nilivutiwa na sayansi, niliamini nadharia ya mageuzi kwa sababu tu watu wengine walisema ilikuwa ya kweli. Sikuamini kuna Mungu kwa sababu ya mambo mabaya yanayotendeka duniani.

“Hata hivyo, nyakati fulani ningejiambia: ‘Ikiwa kuna Mungu mbinguni, basi ninahitaji kumjua. Kwa nini kuna vita na uhalifu mwingi?’ Nilipopata matatizo, nyakati fulani nilisali ili nipate msaada, lakini sikujua nilikuwa nikisali kwa nani.

“Kisha mtu fulani akampa mke wangu trakti iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova yenye kichwa Je, Ulimwengu Huu Utaokoka? Nilikuwa nikijiuliza swali hilo mara kwa mara. Trakti hiyo ilifanya nijiulize swali hili kuhusu Biblia, ‘Je, ni muhimu kuchunguza majibu yake?’ Baadaye, nilipokuwa likizoni, mtu fulani alinipa kitabu Biblia​—Neno la Mungu au la Binadamu? * Nilipotambua kwamba Biblia inakubaliana na sayansi ya kweli, nilihisi kuwa nilihitaji kujifunza mengi kuhusu Biblia. Hivyo, mmoja wa Mashahidi wa Yehova alipojitolea kunifundisha Biblia, nilikubali. Nilipoendelea kuelewa kusudi la Yehova, nilihisi nimemjua Mungu kuwa mtu halisi, mtu ambaye ningeweza kuzungumza naye kwa uhuru kupitia sala.”

Jan, aliyelelewa akiwa Mprotestanti huko London. “Unafiki wa dini na kuenea kwa matatizo kulinifanya niache kuwa mwanadini. Pia, niliacha kwenda chuoni na nikaanza kuimba na kucheza gitaa ili nipate pesa. Huo ndio wakati niliokutana na Pat. Alikuwa amelelewa akiwa Mkatoliki na kama mimi, hakufuata dini.

“Tuliishi katika nyumba fulani pamoja na vijana wengine walioacha masomo na ambao walipendezwa na dini za Mashariki. Tulitumia saa nyingi usiku tukizungumza kwa undani kuhusu kusudi la uhai. Ingawa mimi na Pat hatukuamini kuna Mungu, tulihisi kwamba lazima kuwe na nguvu fulani ‘zinazotegemeza uhai.’

“Baada ya kuhamia kaskazini mwa Uingereza ili tutafute kazi, mwana wetu alizaliwa. Siku moja usiku alishikwa na ugonjwa, na nikajipata nikisali kwa Mungu ambaye sikumwamini. Muda mfupi baadaye uhusiano kati yangu na Pat uliharibika, na nikamchukua mtoto wetu na kuondoka. Kwa mara nyingine, nilisali ili nipate msaada, nikitumaini kwamba kuna mtu aliyekuwa akinisikiliza. Sikujua kwamba Pat pia alikuwa akisali.

“Baadaye siku hiyo, Mashahidi wawili wa Yehova walimtembelea Pat na kumwonyesha mashauri fulani ya Biblia. Alinipigia simu na kuniuliza ikiwa ningetaka kujifunza Biblia pamoja naye na wale Mashahidi. Baada ya muda tulijifunza kwamba ili tumpendeze Mungu tulipaswa kuhalalisha ndoa yetu. Lilionekana kuwa jambo lisilowezekana kwa sababu uhusiano wetu ulikuwa na matatizo.

“Tulitaka kujua mengi zaidi kuhusu utimizo wa unabii wa Biblia, chanzo cha mateso, na maana ya Ufalme wa Mungu. Pole kwa pole, tulitambua kwamba Mungu anajali na tulitaka kufanya mambo anayosema. Tulifunga ndoa. Hekima inayopatikana katika Neno la Mungu imetusaidia kuwalea watoto wetu watatu. Tuna hakika kwamba Yehova alisikiliza sala zetu.”

Chunguza Uthibitisho

Kama mamilioni ya watu wengine, watu waliotajwa katika makala hii walitambua uwongo wa dini na wakagundua kwa nini Mungu anaruhusu watu wateseke. Je, umetambua kwamba katika kila kisa ujuzi sahihi wa Biblia ndio uliowasadikisha watu hao kuwa kwa kweli Yehova anasikiliza sala.

Je, ungependa kuchunguza mambo yanayothibitisha kwamba Mungu yupo? Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia ujifunze ukweli kumhusu Yehova na jinsi unavyoweza kumkaribia “Msikiaji wa sala.”​—Zaburi 65:2.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Ili upate habari zaidi kuhusu thamani ya kukomboa ya kifo cha Yesu, ona sura ya 5 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 12 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Blabu katika ukurasa wa 10]

“Nilipoendelea kuelewa kusudi la Yehova, nilihisi nimemjua Mungu kuwa mtu halisi, mtu ambaye ningeweza kuzungumza naye kwa uhuru kupitia sala”

[Picha katika ukurasa wa 9]

Imani ya kweli inategemea mambo yaliyothibitishwa na tamaa ya kujua ukweli kumhusu Mungu