Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Igeni Imani Yao

“Uendako Nitaenda”

“Uendako Nitaenda”

RUTHU alitembea pamoja na Naomi kwenye barabara iliyopita katika nyanda ndefu za Moabu. Walikuwa peke yao, watu wawili wadogo katika eneo kubwa na lisilo watu. Wazia Ruthu akitambua kwamba ni jioni, kisha anamtazama mama mkwe wake na kuwaza ikiwa ni wakati wa kutafuta mahali pa kupumzika usiku. Alimpenda sana Naomi na alikuwa tayari kufanya lolote ili kumtunza.

Wote wawili walikuwa na huzuni nyingi. Tayari Naomi alikuwa mjane kwa miaka kadhaa, lakini sasa alikuwa akiomboleza misiba mingine, vifo vya wanawe wawili Kilioni, na Maloni. Ruthu pia alikuwa akiomboleza. Maloni alikuwa mume wake. Ruthu na Naomi walikuwa wanaelekea Bethlehemu, mji ulio huko Israeli. Hata hivyo safari zao zilitofautiana kwa njia fulani. Naomi alikuwa akirudi nyumbani. Ruthu alikuwa akienda mahali asipopajua, huku akiacha watu wake wa ukoo, nchi yake, na tamaduni zake, kutia ndani miungu ya nchi hiyo.​—Ruthu 1:3-6.

Ni nini kingemchochea mwanamke mchanga afanye mabadiliko makubwa hivyo? Ruthu angeanzaje maisha mapya na angewezaje kumtunza Naomi? Tunapochunguza majibu ya maswali hayo, tutapata mambo mengi tunayoweza kuiga kuhusu Ruthu Mmoabu. Kwanza, acheni tuone jinsi wanawake hao wawili walivyojipata kwenye barabara ya kwenda Bethlehemu.

Familia Iliyovunjwa na Misiba

Ruthu alilelewa huko Moabu, nchi ndogo iliyokuwa upande wa mashariki wa Bahari ya Chumvi. Nchi hiyo ilikuwa na maeneo yaliyoinuka yenye miti michache na mabonde marefu. Mara nyingi, “nchi ya Moabu” ilikuwa na mazao mengi, hata wakati nchi ya Israeli ilipokumbwa na janga la njaa. Hiyo ndiyo sababu iliyomfanya Ruthu akutane na Maloni na familia yao.​—Ruthu 1:1.

Janga la njaa katika nchi ya Israeli lilimfanya mume wa Naomi, Elimeleki, amchukue mkewe na wanawe kutoka nchi yao na kwenda kuishi Moabu wakiwa wakaaji wageni. Ni lazima hatua hiyo ilijaribu imani ya kila mshiriki wa familia, kwa kuwa Waisraeli walihitaji kuabudu kwa ukawaida kwenye mahali patakatifu ambapo Yehova alikuwa amechagua. (Kumbukumbu la Torati 16:16, 17) Naomi alifaulu kushikilia imani yake. Hata hivyo, bado aliomboleza baada ya mumewe kufa.​—Ruthu 1:2, 3.

Huenda aliomboleza tena wanawe walipooa wanawake Wamoabu. (Ruthu 1:4) Naomi alijua kwamba babu yao, Abrahamu, alijitahidi sana ili kumtafutia mwanawe Isaka mke kutoka kwa watu wake, ambao walikuwa waabudu wa Yehova. (Mwanzo 24:3, 4) Baadaye, Sheria ya Musa iliwaonya Waisraeli wasiwaruhusu wana na binti zao kufunga ndoa na watu wa mataifa ya kigeni, ili watu wa Mungu wasianze kuabudu sanamu.​—Kumbukumbu la Torati 7:3, 4. *

Licha ya hayo, Maloni na Kilioni walioa wanawake Wamoabu. Iwe jambo hilo lilimhangaisha Naomi au kumvunja moyo, bado alihakikisha kwamba aliwatendea wake za wanawe, Ruthu na Orpa, kwa fadhili ya kweli na upendo. Labda alitazamia kwamba siku moja watakuwa waabudu wa Yehova kama alivyokuwa. Kwa vyovyote vile, Ruthu na Orpa walimpenda sana Naomi. Uhusiano wao mzuri uliwasaidia walipopatwa na msiba. Hata kabla ya kuzaa watoto, wanawake hao walifiwa na waume zao.​—Ruthu 1:5.

Je, imani ya kidini ambayo Ruthu alikuwa nayo zamani ilimsaidia kukabiliana na msiba? Huenda isiwe rahisi kujua. Wamoabu waliabudu miungu mingi, Kemoshi ndiye aliyekuwa mungu wao mkuu. (Hesabu 21:29) Inaonekana dini ya Wamoabu ilikuwa pia na ukatili na mambo yenye kutisha yaliyokuwa ya kawaida siku hizo, kutia ndani kuwatoa watoto kama dhabihu. Jambo lolote ambalo Ruthu alijifunza kutoka kwa Maloni au Naomi kumhusu Yehova, Mungu wa Israeli mwenye upendo na rehema, kwa kweli lilimfanya aone tofauti kubwa. Yehova alitawala kwa upendo, bali si kwa vitisho! (Kumbukumbu la Torati 6:5) Baada ya kukabili msiba mkubwa, huenda Ruthu alisitawisha uhusiano wa karibu zaidi na Naomi na alimsikiliza mwanamke huyo mzee alipozungumza kumhusu Mungu mweza-yote, Yehova, kazi zake za ajabu, na jinsi alivyoshughulika na watu wake kwa upendo na rehema.

Kwa upande mwingine, Naomi alitamani sana kupata habari kutoka nyumbani kwao. Siku moja alisikia, labda kupitia mfanyabiashara msafiri, kwamba janga la njaa lilikuwa limekwisha huko Israeli. Yehova alikuwa amewakumbuka watu wake. Sasa mji wa Bethlehemu ulikuwa na maana yake kamili, yaani, “Nyumba ya Mkate.” Naomi akaamua kurudi nyumbani.​—Ruthu 1:6.

Sasa Ruthu na Orpa wangefanya nini? (Ruthu 1:7) Walikuwa wamesitawisha uhusiano wa karibu na Naomi kutokana na mambo yaliyowapata. Inaonekana, hasa Ruthu, alivutiwa na fadhili za Naomi na imani yake imara kwa Yehova. Wajane wote watatu waliondoka kuelekea Yuda pamoja.

Simulizi la Ruthu linatukumbusha kwamba misiba huwapata watu wote, wazuri na wabaya. (Mhubiri 9:2, 11) Pia, linatukumbusha kwamba tunapokabiliana na misiba mikubwa, ni jambo la hekima kutafuta faraja na kitulizo kutoka kwa watu wengine, hasa wale ambao wanatafuta kimbilio katika Yehova, Mungu ambaye Naomi alimwabudu.​—Methali 17:17.

Upendo Mshikamanifu wa Ruthu

Wajane hao watatu walipokuwa wakiendelea na safari yao, jambo lingine lilianza kumhangaisha Naomi. Aliwafikiria wanawake hao wawili waliokuwa wakiandamana naye na kuhusu upendo waliokuwa wamemwonyesha yeye na wanawe. Hakutaka kuwaongezea mizigo mingine. Ikiwa wangeacha nchi yao na kumfuata, angewasaidiaje huko Bethlehemu?

Mwishowe, Naomi akawaambia hivi: “Nendeni, rudini, kila mmoja nyumbani kwa mama yake. Yehova na awaonyeshe fadhili zenye upendo, kama vile tu mlivyowaonyesha wanaume hawa ambao sasa wamekufa na mimi pia.” Pia, alionyesha kwamba alitumaini kuwa Yehova angewabariki kwa kuwapa waume wengine na waanze maisha mapya. “Kisha akawabusu,” simulizi hilo linasema, “nao wakaanza kupaaza sauti zao na kulia.” Ni rahisi kuelewa kwa nini Ruthu na Orpa walikuwa na uhusiano wa karibu na mwanamke huyo mwenye fadhili na asiye na ubinafsi. Wote wawili waliendelea kusisitiza hivi: “Hapana, bali tutarudi pamoja nawe kwa watu wako.”​—⁠Ruthu 1:​8-10.

Hata hivyo, Naomi hakushawishiwa kwa urahisi. Aliwasadikisha kwamba hangeweza kuwasaidia huko Israeli, kwa sababu hakuwa na mume wa kumwandalia, wala wana ambao wangewaoa, wala tumaini lolote. Aliwaambia kwamba alikuwa na uchungu mwingi kwa sababu hakuwa na uwezo wa kuwaandalia.​—Ruthu 1:11-13.

Orpa alielewa kabisa maneno ya Naomi. Huko Moabu alikuwa na mama, watu wa familia, na makao. Lilikuwa jambo linalopatana na akili kubaki Moabu. Hivyo, shingo upande alimbusu Naomi, akamwambia kwaheri na kuondoka.​—Ruthu 1:14.

Namna gani Ruthu? Maneno ya Naomi yalimhusu pia. Hata hivyo, tunasoma hivi: “Bali Ruthu akashikamana naye.” Labda Naomi alikuwa ameanza kutembea tena barabarani lakini akatambua kwamba Ruthu alikuwa akimfuata. Akamwambia hivi: “Tazama! Shemeji yako amerudi kwa watu wake na kwa miungu yake. Rudi pamoja naye.” (Ruthu 1:15) Maneno ya Naomi yanatufunulia jambo fulani muhimu. Orpa hakuwa tu amerudi kwa watu wake, bali pia kwa “miungu yake.” Alikuwa tayari kuendelea kumwabudu Kemoshi na miungu mingine ya uwongo. Je, Ruthu alihisi hivyo pia?

Huku akimtazama Naomi wakiwa kwenye barabara hiyo isiyo na watu, Ruthu alikuwa na uhakika na utulivu moyoni. Moyo wake ulikuwa na upendo mwingi kumwelekea Naomi, na Mungu ambaye Naomi aliabudu. Hivyo akasema: “Usiniombe nikuache, nigeuke nisifuatane nawe; kwa maana uendako nitaenda, na mahali utakapokaa usiku kucha nitakaa. Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako Mungu wangu. Pale utakapokufa nitakufa nami, na hapo ndipo nitakapozikwa. Yehova na anitende hivyo na kuzidi ikiwa chochote isipokuwa kifo kitatutenganisha mimi na wewe.”​—⁠Ruthu 1:16, 17.

Maneno ya Ruthu yalikuwa ya pekee sana, hivi kwamba bado yanakumbukwa hata baada ya miaka elfu tatu kupita. Maneno yake yanafafanua vizuri sifa yenye thamani, yaani, upendo mshikamanifu. Ruthu alikuwa na upendo wenye nguvu na wenye ushikamanifu sana hivi kwamba alikuwa tayari kushikamana na Naomi na kwenda popote pale pamoja naye. Wangetenganishwa tu na kifo. Watu wa Naomi wangekuwa watu wake, kwa kuwa Ruthu alikuwa tayari kuacha kila kitu alichokijua huko Moabu, hata miungu ya Wamoabu. Tofauti na Orpa, Ruthu alisema kwa moyo wote kwamba alitaka Mungu wa Naomi, Yehova, awe Mungu wake pia. *

Basi, wakaendelea na safari wakiwa wawili tu, kwenye barabara ndefu ya kwenda Bethlehemu. Kulingana na mkadiriaji mmoja, huenda safari hiyo ilichukua juma moja. Bila shaka, ingawa walikuwa na huzuni kila mmoja wao alifarijiwa na mwenzake kwa kiasi fulani.

Bado watu wengi wanapatwa na huzuni katika ulimwengu wa leo. Katika Biblia, siku zetu zinaitwa “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” na tunakabili misiba na mambo mengi yenye kuhuzunisha. (2 Timotheo 3:1) Hivyo, sifa aliyoonyesha Ruthu ni muhimu hata zaidi. Upendo mshikamanifu, yaani, upendo ambao unashikamana na mtu au kitu bila kuacha, ni sifa muhimu katika ulimwengu huu wenye misukosuko. Tunauhitaji katika ndoa, katika uhusiano wa kifamilia, katika urafiki, na pia katika kutaniko la Kikristo. Tunapoendelea kusitawisha upendo kama huo, tunaiga mfano mzuri wa Ruthu.

Ruthu na Naomi Huko Bethlehemu

Bila shaka, ni rahisi kuzungumza kuhusu upendo mshikamanifu, lakini ni vigumu kuonyesha upendo huo kwa vitendo. Ruthu hakuwa na nafasi ya kumwonyesha tu Naomi upendo mshikamanifu bali pia Mungu aliyechagua kumwabudu, Yehova.

Hatimaye, wanawake hao wawili waliwasili Bethlehemu, kijiji kilichokuwa karibu kilomita 10 upande wa kusini wa Yerusalemu. Inaonekana Naomi na familia yake walijulikana sana katika mji huo mdogo, kwa kuwa habari kwamba alikuwa amerudi zilisambaa kila mahali. Wanawake katika eneo hilo walimtazama na kuulizana, “Je, huyu ni Naomi? ” Bila shaka, alikuwa amebadilika baada ya kutoka Moabu; kwa kutazama sura na umbo lake, watu wangeona kwamba alikuwa amekabiliana na matatizo na huzuni kwa miaka mingi.​—⁠Ruthu 1:19.

Naomi aliwafunulia wanawake hao wa ukoo na majirani wa zamani jinsi maisha yalivyokuwa machungu kwake. Hata alihisi kwamba jina lake linapaswa kubadilishwa lisiwe Naomi, linalomaanisha “Uzuri wangu” na kuwa Mara, linalomaanisha “Uchungu.” Maskini Naomi! Kama Ayubu aliyeishi kabla yake, alifikiri kwamba Yehova Mungu alikuwa amemletea matatizo.​—Ruthu 1:20, 21; Ayubu 2:10; 13:​24-26.

Wanawake hao walipoendelea na maisha huko Bethlehemu, Ruthu alianza kufikiria jinsi ambavyo angetimiza mahitaji yake na ya Naomi pia. Alijifunza kwamba Sheria ambayo Yehova alikuwa amewapa watu wake huko Israeli ilitia ndani mpango wenye upendo kwa ajili ya maskini. Waliruhusiwa kwenda mashambani wakati wa mavuno na kuwafuata wavunaji, huku wakikusanya masalio yaliyobaki na vilevile kuvuna nafaka iliyokua kwenye ukingo wa mashamba. *​—Mambo ya Walawi 19:9, 10; Kumbukumbu la Torati 24:19-21.

Ulikuwa wakati wa kuvuna shayiri, inaelekea ulikuwa mwezi wa Aprili kulingana na kalenda ya kisasa, na Ruthu alienda mashambani ili kuona kama kuna mtu ambaye angemruhusu akusanye masalio nyuma ya wavunaji. Aliingia katika shamba la mwanamume aliyeitwa Boazi, tajiri aliyekuwa na mashamba na ambaye alikuwa mtu wa ukoo wa Elimeleki, mume wa Naomi aliyekuwa amekufa. Ingawa Sheria ilimruhusu kukusanya masalio, hakuona kwamba ilikuwa haki yake, alimwomba ruhusa mwanamume aliyewasimamia wavunaji ili aanze kazi ya kukusanya. Alimruhusu, na Ruthu akaanza kazi.​—Ruthu 1:22–2:3, 7.

Wazia Ruthu akiwafuata wavunaji. Wavunaji hao walipokuwa wakikata shayiri wakitumia miundu yao, aliinama ili aokote masuke yaliyoanguka au waliyobakisha, akayakusanya katika miganda, na kuibeba mpaka mahali ambapo angeipiga-piga na kupata nafaka baadaye. Ilikuwa kazi ya polepole, yenye kuchosha, na ilikuwa ngumu zaidi kadiri jua lilivyozidi kuwa kali. Hata hivyo, Ruthu aliendelea, akisimama kidogo tu ili kupangusa jasho kwenye paji la uso wake na kula chakula chepesi cha mchana katika “nyumba”​—⁠inaelekea ni kibanda kilichotengenezwa ili kuwapa wafanyakazi kivuli.

Inaelekea Ruthu hakutazamia mtu yeyote amtambue, lakini kuna mtu aliyemtambua. Boazi alimwona na kumwuliza msimamizi fulani kijana kuhusu mwanamke huyo. Boazi, mwanamume mwenye imani thabiti, aliwasalimu wafanyakazi wake​—⁠huenda wengine walikuwa vibarua wa siku moja au hata watu wa mataifa ya kigeni​—⁠akiwaambia “Yehova na awe pamoja nanyi.” Nao wakaitikia kwa maneno kama hayo. Mwanamume huyo mwenye umri mkubwa aliyempenda Yehova alimtendea Ruthu kama bintiye.​—⁠Ruthu 2:​4-7.

Huku akimwita “binti yangu,” Boazi alimshauri Ruthu aendelee kurudi kwenye mashamba yake ili akusanye masalio na kwamba afanye kazi karibu na wanawake vijana wa nyumba yake ili asisumbuliwe na wafanyakazi wa kiume. Alihakikisha kwamba alipata chakula cha mchana. Zaidi ya hayo, alitafuta nafasi ya kumpongeza na kumtia moyo. Jinsi gani?​—⁠Ruthu 2:​8, 9, 14.

Ruthu alipomwuliza Boazi kwa nini alimtendea kwa fadhili hivyo, Boazi alimwambia alikuwa amesikia yote aliyokuwa amemfanyia Naomi, mama-mkwe wake. Inaelekea kwamba Naomi alikuwa amemsifu Ruthu aliyempenda mbele ya wanawake wa Bethlehemu, na habari hiyo ilikuwa imemfikia Boazi. Pia, alijua kwamba Ruthu alikuwa ameanza kumwabudu Yehova kwa kuwa alisema: “Yehova na akupe thawabu kwa sababu ya jinsi unavyotenda, na upate malipo kamili kutoka kwa Yehova Mungu wa Israeli, ambaye umekuja kutafuta kimbilio chini ya mabawa yake.”​—⁠Ruthu 2:12.

Maneno hayo yalimtia moyo sana Ruthu! Kwa kweli, alikuwa ameamua kutafuta kimbilio chini ya mabawa ya Yehova Mungu, kama ndege mdogo anavyojificha kando ya mama yake. Alimshukuru Boazi kwa kumtia moyo. Na akaendelea kufanya kazi mpaka jioni.​—⁠Ruthu 2:​13, 17.

Leo, sote tunaweza kuiga jinsi Ruthu alivyotenda kwa imani kwa sababu tunapambana na hali ngumu za kiuchumi. Hakutazamia kwamba watu wengine walipaswa kumtendea kwa fadhili, hivyo alithamini kila jambo alilofanyiwa. Hakuaibika kufanya kazi ngumu kwa saa nyingi ili kumwandalia mtu aliyempenda, ingawa ilikuwa kazi ya hali ya chini. Alikubali kwa furaha na akafuata mashauri yenye hekima kuhusu jinsi angefanya kazi akiwa salama na kushirikiana na watu wazuri. Jambo la maana zaidi ni kwamba hakusahau kamwe mahali ambapo angepata kimbilio la kweli, yaani, kwa Baba yake aliyemlinda, Yehova Mungu.

Tukionyesha upendo mshikamanifu kama wa Ruthu na kuiga mfano wake wa unyenyekevu, bidii, na kuonyesha uthamini, imani yetu pia itakuwa mfano mzuri wa kuigwa na wengine. Hata hivyo, Yehova aliwaandaliaje Ruthu na Naomi? Tutazungumzia jambo hilo wakati ujao katika mfululizo huu wa makala.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 22 Inapendeza kuona kwamba Ruthu hakutumia tu jina la cheo “Mungu” kama vile ambavyo watu wengi wa mataifa ya kigeni wangefanya; alitumia pia jina la kibinafsi la Mungu, Yehova. Tafsiri ya The Interpreter’s Bible inasema hivi: “Hivyo basi, mwandikaji anakazia kwamba mgeni huyo ni mfuasi wa Mungu wa kweli”

^ fu. 29 Ilikuwa sheria ya pekee sana, bila shaka, ilikuwa tofauti na mpango wowote ambao Ruthu alijua katika nchi yao. Zamani, katika Mashariki ya Karibu, wajane walitendewa vibaya. Kitabu kimoja cha marejezo kinasema hivi: “Baada ya kufiwa na mumewe, kwa kawaida mjane angetegemea wanawe ili kupata mahitaji; kama hakuwa na wana, huenda angejiuza awe mtumwa, angefanya ukahaba, au afe.”

[Sanduku katika ukurasa wa 26]

Kazi Ndogo ya Usanii

Kitabu cha Ruthu kimefafanuliwa kuwa jiwe dogo lenye thamani sana, yaani, kazi ndogo ya usanii. Kwa kweli, kitabu hicho hakina habari nyingi kama kitabu cha Waamuzi ambacho kinakitangulia katika orodha ya vitabu vya Biblia, na ambacho kinatusaidia kujua wakati ambao matukio ya kitabu cha Ruthu yalitukia. (Ruthu 1:1) Inaelekea kwamba vitabu vyote viwili viliandikwa na nabii Samweli. Hata hivyo, unaposoma Biblia, huenda ukakubali kwamba kitabu cha Ruthu kiko mahali panapofaa katika Biblia. Baada ya kusoma kuhusu vita, visa vya uvamizi, na uvamizi wa kulipiza kisasi vilivyorekodiwa katika kitabu cha Waamuzi, utapata kitabu kidogo ambacho kinatukumbusha kwamba Yehova hasahau kamwe watu wenye amani wanaojitahidi kukabiliana na matatizo ya kila siku. Simulizi hili la mambo ya kifamilia linatufunza mengi kuhusu upendo, kupoteza mpendwa katika kifo, imani, na ushikamanifu, mambo ambayo yanaweza kutunufaisha.

[Picha katika ukurasa wa 24]

Ruthu alitenda kwa hekima kwa kuwa karibu na Naomi wakati wa majonzi na msiba

[Picha katika ukurasa wa 2425]

“Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako Mungu wangu”

[Picha katika ukurasa wa 27]

Ruthu alikuwa tayari kufanya kazi ngumu na ya hali ya chini ili atimize mahitaji yake na ya Naomi pia