Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kweli Miujiza Hutukia? Vipingamizi Vitatu Ambavyo Hutokezwa

Je, Kweli Miujiza Hutukia? Vipingamizi Vitatu Ambavyo Hutokezwa

Je, Kweli Miujiza Hutukia? Vipingamizi Vitatu Ambavyo Hutokezwa

KIPINGAMIZI CHA 1: Miujiza haiwezi kutukia kwa sababu inapingana na sheria za asili. Ujuzi wetu wa sheria za asili unategemea mambo ambayo wanasayansi wamechunguza katika ulimwengu unaotuzunguka. Hata hivyo, sheria hizo ni sawa na sheria za lugha fulani—huenda kuna sehemu fulani ambapo sheria hizo hazitumiki. Vivyo hivyo labda hatuelewi kikamili sheria za asili. (Ayubu 38:4) Huenda mwanasayansi anayependa sana kazi yake akatumia miaka mingi kuchunguza sheria fulani ya asili. Lakini jambo moja tu “linalopingana” na sheria hiyo linaweza kumfanya afikirie tena jinsi anavyoielewa. Kama vile msemo mmoja unavyosema, “Unapoona bata mmoja mweusi, unaacha kuamini kwamba bata wote ni weupe.”

Hadithi moja ya kuchekesha inaonyesha jinsi ilivyo rahisi kufanya uamuzi tukiwa hatuna habari kamili. John Locke (1632-1704) alisimulia hadithi hii kumhusu balozi wa Uholanzi na mfalme wa Siam: Balozi alipokuwa akimweleza mfalme kuhusu nchi ya Uholanzi, alitaja kwamba nyakati fulani inawezekana ndovu atembee juu ya maji. Mfalme alikataa wazo hilo na akahisi kwamba balozi huyo alikuwa akimdanganya. Hata hivyo, balozi alikuwa tu akieleza kuhusu jambo ambalo mfalme alikuwa hajawahi kuona likitendeka. Mfalme hakujua kwamba maji yanapoganda na kuwa barafu, ndovu anaweza kutembea juu yake. Kulingana na maoni ya mfalme, jambo hilo halingewezekana kwa sababu hakuwa na habari za kutosha.

Fikiria baadhi ya uvumbuzi ambao miaka iliyopita ulionekana kuwa mambo yasiyowezekana:

● Ndege inaweza kubeba abiria zaidi ya 800 kutoka jijini New York hadi Singapore, bila kutua popote ikisafiri kwa mwendo wa kilomita 900 kwa saa moja.

● Watu walio katika mabara tofauti wanaweza kufanya mkutano wakionana kwa kutumia mfumo wa video.

● Nyimbo nyingi sana zinaweza kuhifadhiwa katika chombo kidogo hata kuliko kasha la kiberiti.

● Madaktari wanaweza kufanya upasuaji wa kupandikiza moyo na sehemu nyingine za mwili.

Tunaweza kufikia mkataa gani kwa kufikiria mambo kama hayo? Mkataa huu: Ikiwa wanadamu wanaweza kutimiza mambo mbalimbali ambayo miaka michache iliyopita yalionekana kuwa hayawezekani, basi ni wazi kwamba Mungu aliyeumba dunia na vyote vilivyomo anaweza kutenda mambo yenye kushangaza ambayo leo hatuyaelewi kikamili wala hatuwezi kuyafanya. *Mwanzo 18:14; Mathayo 19:26.

KIPINGAMIZI CHA 2: Biblia inatumia miujiza ili kuwafanya watu waamini. Biblia haituambii tuamini miujiza yote. Badala yake, inasema jambo tofauti. Inatuonya tuwe waangalifu inapohusu kuamini miujiza na ishara zenye nguvu. Ona onyo hili la wazi: “Huyo mwovu atakuja na nguvu za Shetani na kufanya kila namna ya miujiza na maajabu ya uwongo, na kutumia udanganyifu wa kila namna.”—2 Wathesalonike 2:9, 10, Biblia Habari Njema.

Pia, Yesu Kristo alionya kwamba watu wengi wangedai kuwa wafuasi wake lakini hawangekuwa wafuasi wa kweli. Hata wengine wangemwambia: “Bwana, Bwana! Kwa jina lako tulitangaza ujumbe wako, na kwa jina lako tuliwatoa pepo na kufanya miujiza mingi.” (Mathayo 7:22, BHN) Lakini Yesu alisema hangewakubali watu hao kuwa wafuasi wake. (Mathayo 7:23) Hivyo basi, ni wazi kwamba Yesu hakufundisha kuwa miujiza yote inatoka kwa Mungu.

Mungu hawaambii waabudu wake wawe na imani inayotegemea miujiza pekee. Badala yake, imani yao inapaswa kutegemea kabisa uthibitisho wa hakika.​—Waebrania 11:1.

Kwa mfano, acha tuchunguze muujiza mmoja ulio katika Biblia ambao unajulikana sana, ufufuo wa Yesu Kristo. Miaka mingi baada ya tukio hilo, Wakristo fulani huko Korintho walianza kutilia shaka ikiwa kweli Yesu alifufuliwa. Mtume Paulo aliwasaidiaje Wakristo hao? Je, aliwaambia tu, “Muwe na imani zaidi”? Hapana. Hebu ona jinsi alivyowakumbusha kuhusu uthibitisho wa hakika. Alisema kwamba Yesu “alizikwa, ndiyo, . . . alifufuliwa siku ya tatu kulingana na Maandiko; na kwamba alimtokea Kefa, kisha wale kumi na wawili. Baadaye aliwatokea ndugu zaidi ya mia tano kwa wakati mmoja, ambao walio wengi kati yao wapo mpaka sasa.”​—1 Wakorintho 15:4-8.

Je, lilikuwa jambo la maana kwa Wakristo hao kuamini muujiza huo? Paulo anaendelea kusema: “Ikiwa Kristo hakufufuliwa, hakika kuhubiri kwetu ni bure, na imani yetu ni bure.” (1 Wakorintho 15:14) Paulo hakuchukulia jambo hilo kijuujuu. Alijua ukweli wa mambo! Alijua kwamba muujiza huo ulikuwa wa kweli kwa sababu mamia ya watu waliojionea tukio hilo bado walikuwa hai wakati huo na walikuwa tayari kufa badala ya kusema uwongo kuhusu mambo waliyoona.​—1 Wakorintho 15:17-19.

KIPINGAMIZI CHA 3: Miujiza ni mambo ya asili tu ambayo watu wasio na elimu hawayaelewi. Wasomi fulani wanajaribu kueleza ya kwamba miujiza inayotajwa katika Biblia ni matukio ya asili ambayo yalitokea bila kutegemea nguvu za Mungu. Wanahisi kwamba matukio hayo yanafanya watu waamini masimulizi ya Biblia hata zaidi. Ingawa ni kweli kwamba matukio ya asili—kama vile matetemeko ya nchi, magonjwa ya kuambukiza, na maporomoko ya ardhi—yalihusika katika miujiza fulani, maelezo hayo huwa yanafanana kwa njia moja. Wasomi hao hupuuza wakati ambao muujiza ulitukia kama inavyoelezwa na Maandiko.

Kwa mfano, watu fulani wanasema kwamba pigo la kwanza lililopata nchi ya Misri, kule kugeuka kwa Mto Nile kuwa damu, kulitokea kwa sababu mchanga mwekundu ulibebwa na maji na kuingia ndani ya mto huo, pamoja na viumbe wekundu wanaoitwa flagellates. Hata hivyo, simulizi hilo la Biblia linasema kwamba mto huo uligeuka na kuwa damu wala si udongo mwekundu. Unaposoma kwa makini andiko la Kutoka 7:14-21 utaona kwamba muujiza huo ulitukia tu Haruni alipopiga maji ya Mto Nile kwa fimbo baada ya kuagizwa na Musa. Hata iwe kubadilika kwa mto huo kulisababishwa na mambo ya asili, basi wakati ambao Haruni alipiga maji ya mto huo ni muujiza!

Mfano mwingine unaoonyesha umuhimu wa wakati ambao muujiza ulitukia, ni jambo lililotukia taifa la Israeli lilipokuwa karibu kuingia katika Nchi ya Ahadi. Walizuiwa kuingia katika nchi hiyo kwa sababu Mto Yordani ulikuwa umefurika. Simulizi la Biblia linaeleza kilichotukia: “Mara tu wachukuaji wa lile Sanduku walipofika Yordani na miguu ya makuhani waliolichukua Sanduku ilipotumbukizwa katika maji ya ukingoni . . . , ndipo maji yanayoshuka kutoka juu yakaanza kusimama. Yakasimama kama ukuta wa maji mbali sana huko Adamu.” (Yoshua 3:15, 16) Je, muujiza huo ulitukia kwa sababu ya tetemeko la nchi au poromoko la ardhi? Simulizi hilo halitaji. Lakini wakati tukio hilo lilipotendeka ni muujiza. Lilitukia wakati tu ambao Yehova alikuwa amesema lingetukia.​—Yoshua 3:7, 8, 13.

Hivyo basi, je miujiza hutukia? Biblia inasema kwamba inatukia. Kulingana na mambo ambayo Biblia inatuambia, miujiza si mambo ya asili tu. Je, itakuwa jambo linalopatana na akili kusema kwamba miujiza haiwezi kutukia kwa sababu tu ni mambo ambayo hayafanyiki kila siku?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Ikiwa unatilia shaka kuwapo kwa Mungu, tafadhali ona broshua yenye kichwa Je! Kweli Mungu Anatujali? na Uhai—Ulitokana na Muumba? au mwombe mtu aliyekupa gazeti hili akueleze mengi zaidi.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Miaka kadhaa iliyopita watu waliona kuwa jambo lisilowezekana kwa watu kusafiri angani mamia ya kilomita kwa saa moja tu