Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mazungumzo Pamoja na Jirani Je, Watu Wote Wazuri Huenda Mbinguni?

Mazungumzo Pamoja na Jirani Je, Watu Wote Wazuri Huenda Mbinguni?

Mazungumzo Pamoja na Jirani Je, Watu Wote Wazuri Huenda Mbinguni?

MASHAHIDI WA YEHOVA wanafurahia kuzungumza kuhusu Biblia pamoja na jirani zao. Je, kuna jambo lolote kuhusu Biblia ambalo limekuwa likikutatiza? Je, kuna jambo lolote ambalo Mashahidi wa Yehova wanaamini au kufanya ambalo ungependa kulifahamu zaidi? Ikiwa ndivyo, basi unapokutana tena na Shahidi wa Yehova usikose kumwuliza. Atafurahi kuzungumzia jambo hilo pamoja nawe.

Mazungumzo yafuatayo yanaonyesha jinsi Shahidi wa Yehova anavyoweza kuzungumza na jirani yake. Hebu tuwazie Shahidi anayeitwa Marcus amemtembelea mwanamume anayeitwa Robert nyumbani kwake.

Wale Wanaoenda Mbinguni Watafanya Kazi Gani Huko?

Marcus: Unapowazia wakati ujao, je unafikiri hali zitakuwa bora, mbaya kabisa, au mambo yataendelea jinsi yalivyo?

Robert: Ninafikiri mambo yatakuwa bora. Ninatazamia kwenda mbinguni niishi na Bwana.

Marcus: Hilo ni tumaini zuri ajabu. Biblia inazungumzia mengi kuhusu mbinguni na kuhusu pendeleo la kwenda huko. Je, umefikiria kwa makini wale wanaoenda mbinguni watafanya kazi gani huko?

Robert: Tutakuwa na Mungu na kumsifu milele.

Marcus: Bila shaka, hilo ni tumaini lenye kuvutia. Jambo la kupendeza ni kwamba Biblia haizungumzii tu kuhusu mapendeleo ambayo wale wanaoenda mbinguni watapewa, bali pia kuhusu jukumu muhimu ambalo watakuwa nalo.

Robert: Hilo ni jukumu gani?

Marcus: Ni jukumu linalotajwa hapa katika Ufunuo 5:10. Andiko hilo linasema: “Nawe [Yesu] ukawafanya kuwa ufalme na makuhani kwa Mungu wetu, nao watatawala wakiwa wafalme juu ya dunia.” Robert, umeona jukumu ambalo wale wanaoenda mbinguni watatimiza?

Robert: Andiko hilo linasema kwamba watatawala wakiwa wafalme juu ya dunia.

Marcus: Hilo ni jambo lenye kupendeza, sivyo?

Watatawala Nani?

Marcus: Je, sasa huoni kwamba ikiwa wale wanaoenda mbinguni watatawala wakiwa wafalme, basi ni lazima kuwe na watu watakaotawaliwa? Kwa kweli, haiwezekani kuwa na serikali bila raia.

Robert: Ninaelewa unachosema.

Marcus: Hivyo, swali linalopatana na akili ambalo tunapaswa kujiuliza ni, Watatawala nani?

Robert: Nafikiri tutatawala watu walio duniani ambao bado hawajafa na kwenda mbinguni.

Marcus: Hilo linawezekana ikiwa tu watu wote wazuri huenda mbinguni. Lakini tunapaswa kufikiria jambo lingine. Je, inawezekana kwamba watu fulani wazuri hawataenda mbinguni?

Robert: Sijawahi kamwe kusikia Mkristo anayeamini hivyo.

Marcus: Ninauliza swali hilo kwa sababu ya jambo tunalosoma kwenye Zaburi 37:29. Unaweza kusoma andiko hilo tafadhali?

Robert: Ni sawa. Linasema: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”

Marcus: Asante. Je, umeona watu wengi wazuri wataishi wapi?

Robert: Andiko hilo linasema kwamba wataishi duniani.

Marcus: Kweli kabisa—na si kwa muda mfupi tu! Ona jinsi andiko hilo linavyosema: “Watakaa milele juu yake.”

Robert: Huenda andiko hilo linamaanisha tu kwamba sikuzote kutakuwa na watu wazuri duniani. Tunapokufa na kwenda mbinguni, watu wengine wazuri huzaliwa na kuendelea kuishi duniani.

Marcus: Inaelekea kwamba hivyo ndivyo watu wengi wangeelewa andiko hilo. Lakini, je, inawezekana kwamba andiko hilo lina maana nyingine tofauti? Je, inawezekana kwamba linamaanisha watu wazuri peke yao ndio watakaoishi duniani milele?

Robert: Sina hakika, wewe nieleze.

Dunia Paradiso ya Wakati Ujao

Marcus: Hebu fikiria andiko lingine katika Biblia linavyosema jinsi maisha yatakavyokuwa duniani wakati ujao. Acha tusome Ufunuo 21:4. Mstari huo unasema hivi kuhusu watu watakaoishi wakati huo ujao,: “Naye [Mungu] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” Je, hilo si tumaini lenye kuvutia?

Robert: Ndiyo. Lakini nafikiri andiko hilo linazungumzia jinsi maisha yatakavyokuwa mbinguni.

Marcus: Ni kweli kwamba wale wanaoenda mbinguni watafurahia baraka kama hizo. Lakini hebu tazama mstari huo tena. Unasema itakuwaje kuhusu kifo?

Robert: Unasema kwamba “kifo hakitakuwapo tena.”

Marcus: Bila shaka. Sasa, nina hakika utakubaliana nami kwamba ili jambo lisiwepo tena, ni lazima liwe lilikuwapo.

Robert: Bila shaka.

Marcus: Lakini hakujawahi kamwe kuwa na kifo mbinguni, sivyo? Watu hufa hapa duniani.

Robert: Aha! Nitafikiria kuhusu jambo hilo.

Marcus: Unaona, Robert, Biblia inafundisha kwamba watu fulani wazuri wataenda mbinguni lakini wengine wengi wataishi milele hapa duniani. Kwa kweli, nina hakika kwamba umewahi kusikia maneno haya yanayojulikana sana: “Heri wenye upole, maana wao watairithi nchi.”​—Mathayo 5:5, Union Version.

Robert: Ndiyo, nimewahi kusikia andiko hilo likisomwa kanisani mara nyingi.

Marcus: Ikiwa wapole watairithi nchi, je, hilo halimaanishi kwamba watu wataishi hapa duniani? Wale watakaoishi duniani watafurahia baraka zilizotabiriwa katika kitabu cha Ufunuo. Wataona dunia ikibadilika kabisa kwa sababu Mungu ataondoa kila jambo baya, hata kifo.

Robert: Sasa ninaanza kuelewa unachosema, lakini sina hakika kwamba andiko moja au mawili tu katika Biblia yanathibitisha jambo unalosema.

Marcus: Bila shaka sivyo. Kwa kweli, kuna maandiko mengi yanayozungumzia jinsi maisha yatakavyokuwa hapa duniani wakati ujao. Ikiwa una wakati, ningependa kukuonyesha andiko moja ninalopenda zaidi.

Robert: Ndiyo, nina dakika chache.

“Mtu Mwovu Hatakuwako Tena”

Marcus: Mwanzoni tulisoma andiko la Zaburi 37:29. Acha tusome tena kitabu hicho. Wakati huu tutasoma mistari ya 10 na 11. Unaweza kusoma mistari hiyo tafadhali?

Robert: Ndiyo. “Na bado muda kidogo tu, na mtu mwovu hatakuwako tena; nawe hakika utapaangalia mahali pake, naye hatakuwapo. Bali wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”

Marcus: Asante. Ukitazama mstari wa 11, unafikiri “wapole,” au watu wazuri, wataishi wapi?

Robert: Mstari huo unasema “wataimiliki dunia.” Hata hivyo, ninafikiri mstari huo unatumika hata sasa, kwa sababu leo kuna watu wazuri wanaoishi duniani.

Marcus: Hilo ni kweli. Hata hivyo, ona pia mstari huo unasema kwamba watu wazuri watafurahia “wingi wa amani.” Je, leo tunaona amani nyingi duniani?

Robert: Hapana, hakuna amani.

Marcus: Hivyo basi, ahadi hiyo itatimizwaje? Labda naweza kutumia ulinganisho huu: Wazia kwamba una vyumba vya kukodisha. Wapangaji fulani ni watu wazuri, wanatunza vyumba vyao na kujitahidi kuwa majirani wema. Unafurahi kuwakodishia vyumba. Lakini wapangaji wengine ni wabaya, wanaharibu vyumba na kuwasumbua majirani wao. Sasa ikiwa wapangaji hao wabaya wangekataa kurekebisha tabia yao, ungefanya nini?

Robert: Ningewafukuza.

Marcus: Hivyo ndivyo Mungu atakavyowafanyia watu wabaya walio duniani leo. Tazama tena mstari wa 10. Unasema: “Mtu mwovu hatakuwako tena.” Kwa maneno mengine, Mungu “atawafukuza” watu wanaowasababishia wengine matatizo. Kisha watu wazuri watafurahia maisha duniani wakiwa na amani. Ninajua kwamba huenda wazo hilo la watu wazuri kuishi milele duniani likawa tofauti na jinsi ambavyo ulifundishwa wakati uliopita.

Robert: Ndiyo, sijawahi kamwe kusikia jambo hilo kanisani.

Marcus: Na kama ulivyotaja awali, haitoshi tu kuchunguza mstari mmoja au miwili pekee kuhusu jambo hilo. Kwa kweli, tunahitaji kuchunguza yale ambayo Biblia nzima inasema kuhusu wakati ujao wa watu wazuri. Lakini kulingana na maandiko ambayo tumesoma leo, je, unafikiri inawezekana kwamba watu fulani wazuri wataenda mbinguni, huku wengine wengi wazuri wakiishi hapa duniani?

Robert: Sina hakika. Lakini lazima nikubali kwamba inaonekana ni hivyo kulingana na maandiko ambayo umesoma. Nitafikiria jambo hilo zaidi.

Marcus: Unapofikiria jambo hilo zaidi, huenda utajiuliza maswali mengine. Kwa mfano, namna gani kuhusu watu wazuri ambao waliishi kabla yetu? Je, wote walienda mbinguni? Ikiwa hawakwenda, wako wapi sasa?

Robert: Hayo ni maswali yenye kupendeza.

Marcus: Labda ninaweza kukufanyia mambo mawili. Kwanza, acha nikuandikie maandiko machache ambayo yanazungumzia mambo hayo. * Pili, ningependa kurudi ili tuzungumzie maandiko hayo utakapokuwa umeyasoma na kuyafikiria. Ni sawa?

Robert: Sawa, linaonekana kuwa jambo zuri. Asante.

[Maelezo ya Chini]